YUSSUF Mehboob Manji (pichani kushoto), ameibuka tena Yanga, baada ya kimya
cha muda mrefu akijitokeza kwa nia ya kuokoa jahazi kutokana hali mbaya ya
kiuchumi inayoikabili klabu kwa sasa.
Waajiriwa wa Yanga, wakiwemo makocha, wachezaji na watendaji
hawajalipwa mishahara kwa takriban miezi minne, hali inayoashiria uongozi wa
klabu hiyo, chini ya Mwenyekiti wake, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga umeelemewa.
Lakini mfanyabiashara kijana anayemiliki mamilioni ya fedha,
Manji yu tayari kuokoa jahazi kwa kurejesha udhamini katika klabu.
Hata hivyo, ili kurejea kuidhamini Yanga, Manji ametoa masharti
matano.
Masharti hayo ni; kufanyika uhakiki wa mahesabu ya akaunti
za Yanga ndani ya siku 90 na wakaguzi wa hesabu wa kujitegemea kukagua hesabu
za kipindi cha kuanzia mwaka 2006 hadi 2012 kwa ajili ya fedha zilizoingia
klabuni.
Sharti la pili ni kuchapishwa magazetini kwa akaunti za
Yanga siku 15 baada ya kumalizika kwa robo ya mwaka, tatu ni
kuendeshwa zoezi la kura ya maoni ndani ya siku 60 na kuamua kama wanachama wa Yanga wanataka
klabu iwe Yanga au la na sharti la nne ni mabadiliko ya Katiba ndani ya siku 90.
Kwa mujibu wa barua ya Manji kwa Mwenyekiti wa Yanga, Nchunga
ambayo BIN ZUBEIRY imeipata nakala yake, ameutaka pia uongozi kuidhinisha
mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa klabu, nafasi ambayo iko wazi baada ya Davis
Mosha kujiuzulu mwaka jana.
Sharti la mwisho la Manji ni kutaka kufanyika kwa Mkutano Mkuu
wa wanachama ndani ya siku 30, ili kujadili mustakabali wa klabu.
0 comments:
Post a Comment