• HABARI MPYA

    Thursday, December 13, 2012

    UGANDA ONE KULIPWA MILIONI 2 KWA MWEZI SIMBA SC, AAHIDI SHANGWE MSIMBAZI

    Dhaira kulia akiwa na Hans Poppe baada ya kusaini miaka miwili Simba SC 

    Na Mahmoud Zubeiry
    KIPA namba moja wa Uganda, Abbel Dhaira mbali na kusaini mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya dola za Kimarekani 40,000, pia atakuwa akipokea mshahara wa Sh. Mlioni 2 kwa mwezi.
    Dhaira alisaini mkataba jana katika hoteli ya JB Belmonte, Dar es Salaam mbele ya Katibu wa Simba, Evodius Mtawala na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu hiyo, Zacharia Hans Poppe.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana, baada ya kumsajili kipa huyo, Hans Poppe alisema kwamba huyu ni kipa wa kwanza mwenye umbo kubwa tangu, kumalizika kwa zama za Mwameja Mohamed katika klabu hiyo.
    “Naamini tumepata mtu sahihi na katika wakati mwafaka, hakuna asiyejua umahiri wa Dhaira langoni, sasa tunasubiri kuvuna matunda ya kumsajili,”alisema Hans Poppe, Kapteni wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania(JWTZ), ambaye leo anapanda ndege kwenda Uingereza kwa mapumziko ya Krisimasi na mwaka mpya.
    Hans Poppe aliyepigana vita dhidi ya Uganda, alisema kwamba Dhaira ni kipa ambaye amependekezwa na kipa wao wa kwanza hivi sasa, Juma Kaseja hivyo anaamini wawili hao wataishi vizuri na kushirikiana.
    Kwa upande wake, Dhaira ambaye anarejea leo kwao Uganda kwenda kuchukua vifaa vyake vya kazi kwa ajili ya kuja kuanza kumtumikia mwajiri wake mpya, alisema kwamba amefurahi kusaini Simba SC na atafanya vizuri ili kuwafurahisha mashabiki wa klabu hiyo.
    “Simba ni klabu kubwa Afrika na inacheza Ligi ya Mabingwa Afrika, kuna wachezaji rafiki zangu na ndugu zangu, Mussa Mudde na Emmanuel Okwi, lakini Afrika Mashariki ni moja, wachezaji wote wa Simba ni ndugu zangu, nitajisikia nipo nyumbani kabisa”alisema Dhaira, anayetua Simba akitokea I.B.V FC ya Iceland.
    Dhaira aliyeibukia Express ya Uganda mwaka 2006, mwaka 2008 alihamia U.R.A. pia ya Uganda, ambayo aliichezea hadi mwaka 2010 alipohamia Ulaya.
    Kwa kumpata Dhaira, Simba SC imepata kipa wa uhakika wa kusaidiana na kipa wake wa kwanza, Juma Kaseja ambaye amekuwa akisoteshwa peke yake bila kupumzika. Na hiyo inafuatia makipa wengine, Wilbert Mweta na Hamadi Waziri kushindwa kuonyesha uwezo wa kumsaidia Kaseja.
    Katika mechi za mwishoni za mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara, Kaseja alionekana kuchoka na kudaka chini ya kiwango chake, jambo ambalo lilisababisha mashabiki wenye ‘akili mbovu’ wamfanyie fujo baada ya kufungwa mabao mawili katika mechi dhidi ya Mtibwa Sugar, Simba ikilala 2-0.
    Kwa sababu hiyo, Kaseja alikasirika na kujiengua kwenye kikosi cha timu hiyo akisema hataki tena kuchezea Simba.
    Lakini pamoja na matatizo hayo, Kaseja aliitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ambako ameendelea kufanya vizuri na kuonyesha yeye ni Tanzania One wa ukweli.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: UGANDA ONE KULIPWA MILIONI 2 KWA MWEZI SIMBA SC, AAHIDI SHANGWE MSIMBAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top