• HABARI MPYA

    Thursday, January 02, 2014

    PONDAMALI KOCHA MPYA YANGA SC, KUANZA KAZI KESHO JANGWANI

    Na Mahmoud Zubeiry, Zanzibar
    JUMA Nassor Pondamali, ndiye kocha mpya wa makipa wa klabu ya Yanga SC ya Dar es Salaam, anayechukua nafasi ya Mkenya, Razack Ssiwa aliyetupiwa virago.
    Yanga imetimua benchi zima la Ufundi baada ya kufungwa mabao 3-1 na mahasimu wao, Simba SC katika mechi ya Nani Mtani Jembe, Desemba 21, mwaka huu.
    Tayari nafasi ya Kocha Msaidizi, Freddy Felix Minziro imechukuliwa na aliyekuwa kocha Mkuu wa Ruvu Shooting, Charles Boniface Mkwasa ‘Master’.
    Amerudi Jangwani; Juma Pondamali akiwa kazini Taifa Stars, sasa anarejesha utaalamu wake Yanga SC

    Kwa sasa, Pondamali pamoja na kuwa kocha wa makipa wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, pia alikuwa kocha wa makipa wa klabu ya Coastal Union ya Tanga hadi mwishoni mwa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Pondamali baada ya kustaafu soka, amewahi kuwa Kocha Msaidizi wa Yanga mara kadhaa, ingawa siku za karibuni ameelekeza nguvu zake katika kuwanoa makipa pekee.
    Pondamali ni kati ya makipa hodari waliowahi kutokea Tanzania, ambaye alikuwa miongoni mwa makipa watatu kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichocheza Fainali pekee za Mataifa ya Afrika mwaka 1980 nchini Nigeria pamoja na Iddi Pazi ‘Father’ na Athumani Mambosasa, sasa marehemu. 
    Father Pazi kwa sasa ndiye kocha wa makipa wa Simba SC, ambayo ipo visiwani Zanzibar kwenye Kombe la Mapinduzi. 
    Harakati za kumsaka mbadala wa aliyekuwa kocha Mkuu, Mholanzi Ernie Brandts bado zinaendelea na viongozi wa klabu hiyo wapo katika mchakato mkali wa kusaka kocha wa kigeni mwenye sifa.
    Yanga imeshindwa kufanya mazoezi leo kwa sababu ilikuwa bado haijamalizana na walimu wapya Wasaidizi, Mkwasa na Pondamali, lakini leo jioni wataalamu hao wapya waliowahi kuichezea klabu hiyo kwa mafanikio, wanatarajiwa kukabidhiwa timu, ili kesho waanze kazi. 
    Yanga SC imeshindwa kushiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi kwa mara ya pili mfululizo mwaka huu visiwani Zanzibar, kutokana na kutokuwa na benchi la Ufundi.
    Mwaka jana, Yanga ilijitoa kwenye michuano hiyo kwa sababu ilikwenda kwenye ziara ya mafunzo nchini Uturuki.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: PONDAMALI KOCHA MPYA YANGA SC, KUANZA KAZI KESHO JANGWANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top