• HABARI MPYA

    Saturday, September 27, 2014

    DANNY MRWANDA AIPOKONYA TONGE MDOMONI SIMBA SC, ASAWAZISHA KIPINDI CHA PILI 1-1 TAIFA

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imelazimishwa sare ya pili mfululizo katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya jioni hii kufungana bao 1-1 na Polisi Morogoro Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Hiyo ni sare ya pili mfululizo kwa kocha Mzambia, Patrick Phiri baada ya wiki iliyopita kutoka 2-2 na Coastal Union Uwanja wa Taifa, licha ya kuongoza 2-0 hadi mapumziko.
    Hadi mapumziko, tayari Simba SC ilikuwa inaongoza kwa bao 1-0 lililofungwa na Mganda, Emmanuel Okwi dakika ya 32 akimalizia pasi fupi ya Mohammed Hussein ‘Tshabalala’.
    Kipa Hussein Sharrif ‘Cassilas’ alifanya kazi nzuri baada ya kupangua mpira wa adhabu uliopigwa na Hassan Mganga dakika ya 36. 
    Makocha wa Simba SC, Patrick Phiri na Msaidizi wake, Suleiman Matola kulia wapo katika mgumu 

    Kipindi cha pili, Polisi inayofundishwa na Mohammed ‘Adoph’ Rishard ilibadilika na kuanza kusukuma mashambulizi langoni mwa Simba SC.
    Danny Mrwanda, mshambuliaji wa zamani wa Simba SC, aliisawazishia Polisi baada ya kumzidi mbio na maarifa beki Joseph Owino kabla ya kumchambua vizuri kipa Hussein Sharrif ‘Cassilas’.
    Baada ya kufunga bao hilo, Mrwanda alikwedna kwenye kibendera kushangilia kama mzee, kuashiria anawabeza Simba SC waliomtema mwaka juzi dakika za mwishoni kabla ya Ligi Kuu kuanza, wakimuita mzee, akatimkia Vietnam. 
    Mrwanda alifanya kitu ambacho Mcameroon Samuel Eto’o akifanya msimu uliopita alipokuwa Chelsea baada ya kufunga dhidi ya Manchester United na kushangilia kama mzee kumbeza kocha Jose Murinho aliyemuita kikongwe. 
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Hussein Sharrif ‘Cassilas’, Nassor Masoud ‘Chollo’/William Lucian ‘Gallas’dk56, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Hassan Isihaka, Joseph Owino, Jonas Mkude, Ramadhani Singano ‘Messi’, Pierre Kwizera, Amisi Tambwe/Elias Maguri dk74, Shaaban Kisiga na Emmanuel Okwi. 
    Polisi Moro; Abdul Ibad, Rogers Fred, Hassan Mganga, Anafi Suleiman, Lulanga Mapunda, Said Mkangu, Machaku Salum/Suleiman Kassim ‘Selembe’ dk64, James Ambrose, Edgar Charles/Edward Christopher dk39, Danny Mrwanda na Nocholas Kabipe/Nahoda Bakari dk46.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DANNY MRWANDA AIPOKONYA TONGE MDOMONI SIMBA SC, ASAWAZISHA KIPINDI CHA PILI 1-1 TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top