Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
MIAMBA ya soka Tanzania, Simba na Yanga iligawana pointi Jumamosi baada ya sare ya bila kufungana katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Sare hiyo inaifanya Simba SC itimize pointi nne baada ya awali kutoa sare tatu pia, wakati Yanga SC inafikisha pointi saba baada ya mechi nne, ikiwa nyuma ya Azam FC na Mtibwa Sugar zenye pointi 10 kila moja kileleni mwa Ligi.
Pamoja na kushinda 2-1 mara mbili dhidi ya Prisons na JKT Ruvu, lakini Yanga SC ilikutana na upinzani mkali na matokeo yangeweza kuwa kinyume kama si bahati yao.
Kiungo wa Yanga SC, Andrey Coutinho akimiliki mpira mbele ya beki wa Simba SC, William Lucian 'Gallas' katika mchezo baina ya watani hao wa jadi Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
Yanga SC sasa watasafiri hadi Shinyanga kuwafuata Stand United waliopanda Ligi Kuu msimu huu, mchezo utakaofanyika Jumamosi Uwanja wa Kambarage.
Stand imeonyesha ni timu imara ikifanikiwa kuvuna pointi tano katika mechi za ugenini, kutokana na sare mbili dhidi ya Simba SC na Kagera Sugar na ushindi wa 1-0 dhidi ya JKT Mgambo.
Stand ilipoteza mchezo wa kwanza nyumbani kwa kufungwa 4-1 na Ndanda FC ya Mtwara iliyopanda pia Ligi Kuu msimu huu, lakini baada ya hapo imecheza mechi tatu ugenini bila kufungwa.
Pata picha Yanga SC wanakwenda kukutana na upinzani wa aina gani katika mchezo huo Jumamosi.
Simba SC sasa. Watacheza na Prisons ya Mbeya Jumamosi Uwanja wa Sokoine, Mbeya.
Prisons ilionyesha upinzani ikifungwa na Yanga SC 2-1 na pia ilishinda ugenini 2-0 dhidi ya Ruvu Shooting kabla ya kutoa sare ya 0-0 na Azam FC Mbeya.
Jana, Prisons wamefungwa 2-1 na JKT Ruvu Mbeya na baada ya mchezo huo, kocha Juma Mwambusi akasema amekubali matokeo na anaelekeza nguvu zake katika mchezo ujao.
Simba SC ambayo haijashinda mechi msimu huu kwa kutoa sare nne, unafikiri inakabiliwa na mechi ya aina gani mwishoni mwa wiki?
0 comments:
Post a Comment