• HABARI MPYA

    Wednesday, October 01, 2014

    ILIVYO NGUMU SIMBA SC KUEPUKA KUUA KIPAJI CHA MANYIKA JR WANAJUA KABAL FARAJ NA ABUU HASHIMU

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MWAKA 2001, waliokuwa makocha wa timu za taifa za vijana, Mnigeria Ernest Mokake na mzalendo Juma Matokeyo (wote marehemu) walifanikiwa kuibua vipaji vingi, ambavo vilikuwa tegemeo la taifa kwa karibu muongo wote uliopita.
    Miongoni mwa nyota waliobuliwa ni kipa Juma Kaseja, viungo Haruna Moshi ‘Boban’, Nico Nyagawa na mshambuliaji Mussa Hassan Mgosi.
    Kaseja akiwa na wenzake hao baada ya kung’ara na timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, kwa uwezo wao wakasajiliwa na timu za Ligi Kuu.
    Peter Manyika kipa chipukizi wa Simba SC anayehitaji kukuza kiwango chake, lakini anakabiiwa na changamoto ya ushindani wa namba dhidi ya makipa wazoefu, Ivo Mapunda na Hussein Sharrif 'Cassilas'
    Kaseja alikwenda Moro United, Haruna alikwenda Coastal Union ya Tanga wakati Mgosi na Nico walikwenda Mtibwa Sugar.
    Mwishoni mwa mwaka 2002, Kaseja akasajiliwa Simba SC na kuanza kudaka msimu wa 2003. Simba SC ilimsajili Kaseja baada ya aliyekuwa kipa wao hodari enzi hizo, Mwameja Mohamed kustaafu.
    Mwameja alistaafu vizuri akiiacha Simba SC na mataji matatu, Kombe la Tusker, ubingwa wa Ligi Kuu ya Muungano na Kombe la Kagame au Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati.
    Katika msimu wake wa kwanza, Kaseja aliifikisha Simba SC Fainali ya Kombe la Kagame mjini Kampala, Uganda, ikafungwa 1-0 katika fainali na wenyeji SC Villa.
    Tangu hapo, Kaseja akawa ‘Simba One’ na akaiongoza vyema klabu hiyo katika Ligi ya Mabingwa Afrika akiifikisha hatua ya makundi kwa mara ya kwanza na ya mwisho hadi sasa.
    Kabla ya hapo, klabu ya Tanzania kuwahi kucheza hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ilikuwa Yanga SC mwaka 1998.
    Kaseja amekuwa kipa kipenzi cha wana Simba na tegemeo kwa muongo wote uliopita- kabla ya mwaka 2009 kuhamia Yanga SC kwa Mkataba mnono wa mwaka mmoja, ambao ulipoisha akarejea Msimbazi.
    Amedaka Simba SC na kuendelea kuipa mataji hadi mwaka jana alipotemwa na kwa bahati nzuri akasajiliwa tena Yanga SC.
    Kaseja ameingia kwenye orodha ya makipa wenye mafanikio Tanzania akiwa ameshinda mataji na klabu mbili kubwa, Simba na Yanga pamoja na timu ya taifa.
    Juma Kaseja kushoto aliiongoza Simba SC kucheza hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa Afrika katika msimu wake wa kwanza 2003 kabla ya gwiji wa klabu hiyo 

    Kaseja alipata bahati ya aina yake, kutoka U17 kwenda Moro United ambako aliaminiwa na kupewa nafasi akang’ara hadi kuonekana Simba SC alikoingia na kufanya vizuri hadi sasa anaitwa gwiji.
    Katika kikosi cha sasa cha Simba SC, wachezaji 11 wanapokuwa uwanjani, kwenye benchi anakuwapo kipa mmoja chipukizi, anaitwa Peter Manyika.
    Huyo ni mtoto wa kipa maarufu na bora wa zamani nchini, Manyika Peter aliyewika Taifa Stars na klabu za Yanga SC na Mtibwa Sugar.      
    Manyika mdogo ana umbo zuri la ukipa, anajua kudaka na unaweza kumuita hodari awapo langoni.
    Lakini katika Simba SC, ni kipa wa tatu baada ya Ivo Mapunda na Hussein Sharrif ‘Cassilas’.
    Huyo huwezi kumfikiria kudaka leo wala kesho, labda itokee bahati mbaya sana wakati huu ambao kipa namba moja, Ivo ni majeruhi, na Cassilas naye apate udhuru wa kuumia au kusimamishwa.
    Lakini kama haitatokea bahati mbaya hiyo- ina maana Manyika mdogo ataendelea kudaka mazoezini tu na labda mwishoni mwa mwaka ataidakia Simba B katika Kombe la Uhai.
    Amepitia kwenye msingi mzuri wa soka akianzia kuwa kipa namba moja wa U17 na kipa namba moja wa U20- na uwezo wake umewavutia wengi.
    Kabali Faraj alikuwa kipa namba moja wa U20 ya nchi ambayo ilikuwa inaundwa na akina Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu, wakati huo huo kipa wa kwanza wa timu ya vijana ya Simba SC. Alikuwa miongoni mwa nyota waliokuwa wakiibukia vizuri wakati huo na akatabiriwa kufika mbali.
    Na wakati huo, kikosi cha kwanza cha Simba SC kilikuwa ina makipa Kaseja na Ally Mustafa ‘Barthez’ ambao wote sasa wapo Yanga SC- leo hii Samatta na Ulimwengu wakiwa TP Mazembe, sijui Kabali yuko wapi. Hasikiki tena kwenye viwanja vya soka.
    Abuu Hashim ameipa mataji Simba B na alidaka vizuri timu hiyo ikicheza na timu za wakubwa za Ligi Kuu zikiwemo Mtibwa Sugar na Azam FC katika michuano ya BancABC mwaka juzi na kuipa timu Kombe hilo lililofanyika mara moja.
    Baada ya hapo, akapandishwa Simba A na kuna wakati alipewa mechi za Ligi Kuu na kudaka vizuri. Leo sijui yuko wapi Abuu.
    Ukweli ni kwamba ni vigumu mno kwa chipukizi kuanzia timu kubwa na kufanikiwa- wachache sana wanaofanikiwa, kwa sababu viongozi wetu hawana subira.
    Mbaya zaidi klabu zetu kubwa hazifikirii sana kumpandisha mchezaji, ingawa Simba SC na Azam FC kwa sasa wanajaribu hiyo- ukiwa kipa wa pili au wa tatu, daima utaendelea kuchukuliwa hivyo. 
    Kipa wa kwanza akiyumba kidogo, watu hawafikirii kipa wa pili au wa tatu, wanatafuta kipa mwingine kutoka nje na ndiyo maana leo Kabal na Abuu hawapo Simba SC kuna Ivo na Cassilas.
    Ili kukuza kiwango chake, Manyika mdogo anahitaji kupata mechi za kucheza akusanye uzoefu, nafasi ambayo ni vigumu kuipata Simba SC kwa sasa. Lakini huyo ni kipa ambaye ukiondoa Simba yenyewe, Azam na Yanga SC- klabu nyingine yoyote ya Lgi Kuu itatamani huduma zake.
    Ni juu yao Simba SC kumtoa kwa mkopo mchezaji huyo akapate uzoefu timu nyingine, au kuendelea kuwa naye ili baadaye ije kumtupia virago kama ilivyokuwa kwa Kabal Faraj na Abuu Hashimu. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ILIVYO NGUMU SIMBA SC KUEPUKA KUUA KIPAJI CHA MANYIKA JR WANAJUA KABAL FARAJ NA ABUU HASHIMU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top