• HABARI MPYA

    Sunday, March 01, 2015

    KIGOGO HUYU WA CAF NDIYO JEURI YA EL MERREIKH, WANAWEZA KUFANYA WATAKALO NA WASICHUKULIWE HATUA YOYOTE

    Na Mwandishi Wetu, KHARTOUM
    WATU wa El Merreikh mjini Khartoum, Sudan wamewaambia Azam FC, hata waende kulalamika wapi, Shirikisho la Soka Afrika haliwezi kuwasikiliza kwa kuwa kuna mtu anaitwa Magdi Shams El Din (pichani juu).
    Azam FC jana imeaga mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, baada ya kufungwa mabao 3-0 na El Merreikh ya Sudan katika mchezo wa marudiano wa Raundi ya Awali uliofanyika Uwanja wa Marreikh mjini Khartoum.
    Marefa wa mchezo huo kutoka Zambia Wellington Kaoma aliyesaidiwa na Romeo Kasengele na Amos Nanga walionekana wazi kuiuma Azam FC katika mchezo huo.
    Pamoja na kupewa penalti ambayo ilipigwa na Augustine Okran na kuokolewa na kipa Aishi Manula, Merreikh ilimaliza dakika 45 za kwanza inaongoza kwa bao 1-0 lililofungwa ba Bakr dakika ya 16.
    Kipindi cha pili marefa wa Zambia waliongeza mbeleko kwa Merreikh na ikafanikiwa kupata mabao mawili zaidi yaliyofungwa na Ahmed Abdallah dakika ya 85 na Alan Wanga dakika ya 90.
    Azam FC inatolewa kwa jumla ya mabao 3-2 baada ya awali kushinda 2-0 katika mchezo wa kwanza nyumbani, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Kwa kujua mbinu walizopanga na marefa hao, Merreikh walizuia mchezo huo usionyeshwe na Televisheni yoyote.
    Na baada ya mchezo huo, Azam FC walianza jitihada za kuwasilisha malalamiko yao kwa Kamisaa, Ahmed Mohamed Magahed Osman wa Misri lakini hawakusikilizwa.
    Kamisaa huyo alikuwa akiongea kwa kicheko na furaha na viongozi wa Merreikh na watu wa timu hiyo ya Sudan wakawaambia kwa Kiingereza viongozi wa Azam FC; “Mtakwenda popote hamtafanikiwa, kuna Magdi Shams El Din,”.
    Magdi Shams El Din ni Msudan, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Marefa ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) ambayo inahusika kupanga marefa kwenye mashindano.
    Hakuna refa ambaye anaweza kupuuza agizo la Magdi Shams El Din kwa sababu anajua ataishia kuchezesha Ligi za nchini mwao na kwa sababu hiyo kuna uwezekano marefa wa Zambia waliweka pembeni sheria 17 za soka katika mchezo wa jana ili ‘kumfurahisha’ bosi wao, Magdi Shams El Din.
    Lakini pamoja na ‘mikwara’ hiyo, Mtendaji Mkuu wa Azam FC, Saad Kawemba mwenye uzoefu wa kuanzia kufanya kazi Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) amesema wanapelekea kesi na ushahidi wote CAF juu ya udhalimu waliofanyiwa na Merreikh na marefa wa Zambia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KIGOGO HUYU WA CAF NDIYO JEURI YA EL MERREIKH, WANAWEZA KUFANYA WATAKALO NA WASICHUKULIWE HATUA YOYOTE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top