• HABARI MPYA

    Sunday, May 03, 2015

    SIMBA SC WABISHA HODI ANGA ZA KIMATAIFA, WAICAPA AZAM 2-1 TAIFA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imeweka hai matumaini ya kucheza michuano ya Afrika mwakani, kufuatia ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Simba SC sasa inafikisha pointi 44 baada ya kucheza mechi 25, wakati Azam inabaki na pointi zake 45 za mechi 24 katika nafasi ya pili. Tayari Yanga SC imekwishajihakikishia ubingwa baada ya kufikisha pointi 55 za mechi 24
    Simba SC sasa itaanza kuiombea dua mbaya Azam FC ipoteze mechi zake zote mbili zilizobaki dhidi ya Yanga na Mgambo- na wenyewe (Simba SC) washinde mechi yao ya mwisho, ili kumaliza katika nafasi ya pili waweze kucheza Kombe la Shirikisho Afrika mwakani.
    Ramadhani Singano 'Messi' akishangilia baada ya kuifungia bao la ushindi Simba SC

    Katika mchezo huo, uliochezeshwa na refa Israel Nkongo wa Dar es Salaam aliyesaidiwa na Frerdinand Chacha wa Mwanza na Soud Lila wa Dar pia, mabao ya Simba SC yalifungwa na Ibrahim Hajibu na Ramadhani Singano ‘Messi’, wakati la Azam FC lilifungwa na Mudathir Yahya.
    Dalili za Azam FC kupoteza mchezo huo zilianza kuonekana mapema tu baada ya dakika ya 38, kiungo wake tegemeo, Salum Abubakar ‘Sure Boy’ kutolewa kwa kadi nyekundu kufuatia kumchezea rafu Mohammed Hussein ‘Tshabalala’.
    Na mwishoni mwa kipindi cha kwanza, Frank Domayo akaumia na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake ikichukuliwa na Brison Raphael.
    Emmanuel Okwi kulia akimtoka Serge Wawa wa Azam FC leo

    Simba SC ilipata bao lake la kwanza dakika ya 48, mfungaji Hajibu aliyemalizia kwa kichwa krosi ya kiungo Said Ndemla.
    Mudathir Yahya akaisawazishia Azam FC dakika ya 57 akimalizia pasi ya Kipre Herman Tchetche na dakika ya 74, Messi wa Msimbazi akaifungia Simba SC bao la pili kwa shuti la mbali.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Ivo Mapunda, Hassan Kessy, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Joseph Owino, Juuko Murusheed, Jonas Mkude, Ramadhani Singano ‘Messi’/William Lucian ‘Gallas’ dk85, Said Ndemla/Elias Maguri dk75, Ibrahim Hajib, Emmanuel Okwi na Awadh Juma.
    Azam FC; Aishi Manula, Shomary Kapombe, Gardiel Michael, Agrey Morris, Serge Wawa/Mudathir Yahya dk46, Himid Mao, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Frank Domayo/ Brison Raphael dk45, Didier Kavumbagu/John Bocco dk77, Kipre Tchetche na Brian Majwega.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC WABISHA HODI ANGA ZA KIMATAIFA, WAICAPA AZAM 2-1 TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top