• HABARI MPYA

    Thursday, September 06, 2012

    AZAM FC YAUA 4-0 CHAMAZI

    Azam FC

    Na Princess Asia
    KATIKA kujiandaa na mchezo wa Ngao ya Jamii, dhidi ya Simba SC Jumanne ijayo, Azam FC jana walicheza mechi ya kujipima nguvu na timu ya vijana ya klabu yao, Azam Academy na kuibuka na ushindi wa mabao 4-0.
    Mabao ya Azam katika mchezo huo kwenye Uwanja wa Chamazi, yalifungwa na Abdi Kassim Sadallah ‘Babbi’, Kipre Herman Tcheche na Kipre Michael Balhou.
    Kocha wa Azam Academy, Iddi Cheche alisema kipigo hicho ni kwa sababu alikosa wachezaji wake 10 wa kikosi cha kwanza, wanane wakiwa na timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa mikaka 17, Serengeti Boys na wawili majeruhi.  
    Wakati huo huo, hali ya viungo Ibrahim Mwaipopo na Salum Abubakar ‘Sure Boy Jr.’, Jabir Aziz na Hamisi Mcha ‘Vialli’ na beki wa kushoto, Salum Waziri ambao ni majeruhi inaendelea vizuri na kesho wanaweza kuanza mazoezi.
    Wachezaji wote hao watano wanaendelea vizuri na tiba na kuna matumaini wanaweza kuwa fiti kwa mechi ya Ngao ya Jamii, Septemba 11 dhidi ya Simba, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Wachezaji hao wamekuwa wakifanya mazoezi mepesi, wakiongozwa na daktari wa timu hiyo, Dk Mwanandi Mwankemwa kuanzia gym hadi uwanjani. Dk. Mwanandi anasema wachezaji hao hali zao zinatia matumaini kwa sasa na wataendelea kuwaangalia hadi mwishoni mwa wiki ili kujua maendeleo yao.
    Azam inatarajiwa kuivaa Simba katika mechi ya Ngao ya Jamii ya kuashiria kufunguliwa kwa pazia la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Septemba 11, mwaka huu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ikiwa ni mchezo wake wa kwanza katika historia ya Ngao hiyo.
    Kihistoria hiyo itakuwa mechi ya tano ya Ngao ya Jamii kuchezwa nchini na ya pili kuishirikisha timu nje ya wapinzani wa jadi wa soka ya Tanzania, Simba na Yanga.
    Mtibwa ilicheza na Yanga mwaka 2009, baada ya Simba kugoma na ikashinda mabao 2-1 na kutwaa Ngao, wakati kabla ya hapo, mwaka 2001, Ligi Kuu ya Tanzania ikiwa bado inadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia ya Safari Lager, ilichezwa mechi ya kwanza ya Ngao kihistoria.
    Katika mechi hiyo, Yanga ilishinda mabao 2-1 dhidi ya Simba na mwaka juzi Yanga iliifunga tena Simba kwa penali 3-1 kufuatia sare ya 0-0 na mwaka jana, Simba ilitwaa Ngao ya kwanza katika historia yake, kwa kuifunga Yanga mabao 2-0.
    Ikumbukwe mara ya mwisho Simba SC ilipokutana na Azam FC, katika Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame mwezi uliopita Dar es Salaam, ilifungwa mabao 3-1, yote yakifungwa na Bocco na lile la kufutia machozi kwa wekundu hao Msimbazi liliwekwa kimiani na beki mahiri Shomari Kapombe, aliyemajeruhi kwa sasa. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAUA 4-0 CHAMAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top