![]() |
Kinatra wa mabao wa Azam FC, John Bocco kushoto |
KWA mara ya pili katika kipindi
cha miezi miwili, jana refa aliyechezesha mechi iliyoihusisha Azam FC alipigwa
na mashabiki baada ya mechi.
Azam ilishinda 1-0, beo pekee la
beki wake wa kati wa kimataifa wa Tanzania, Aggrey Morris Ambroce dakika ya 83
katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya wenyeji Polisi
Dodoma.
Ushindi huo, unaifanya Azam
itimize pointi 50, sawa na Simba SC ambayo sasa inaongoza ligi hiyo kwa mabao
tu zaidi ya kufunga.
Yanga inabaki nafasi ya tatu kwa
pointi zake 44 na haitaweza kupanda hata ikishinda leo dhidi ya Toto Africa
mjini Mwanza.
Simba inaweza kuiacha Azam kwa
pointi tatu, iwapo itaifunga Ruvu Shooting leo Uwanja wa Taifa.
Katika mchezo wa jana, Polisi
Dodoma, ilipata pigo baada ya beki wake, Bakari Omari kutolewa nje kwa kadi
nyekundu, dakika ya 57 baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano.
Refa wa mchezo huo alipigwa na mashabiki kwa madai
ya kuwapendelea Azam, baada ya mpambano kukamilika, lakini askari walifanikiwa
kumuokoa asipokee kipondo zaidi.
Mwezi uliopita, refa aliyechezesha
mechi kati ya Yanga na Azam, Israel Nkongo alipigwa na Stefano Mwasyika na
angeweza kupigwa pia na mashabiki wa Yanga.
Kwa nini apigwe? Kisa kutuhumiwa
kuipendelea Azam. Mechi zinazochezwa kwenye Uwanja wao, timu nyingi zimekuwa
zikilalamika Azam inabebwa.
Kwa muda mrefu wapenzi wa soka Tanzania
wamekuwa wakilalamikia desturi ya klabu kongwe nchini Simba na Yanga kutamba
nyumbani, kudaiwa kushinda kwa kununua mechi.
Hii inasababisha timu zetu
zinakuwa dhaifu kwenye michuano mikubwa na ndiyo maana zinashindwa japo kucheza
hatua ya makundi tu ya michuano ya Afrika.
Watu wanataka timu ishinde kwa
uwezo, ili idhihirishe ubora ambao utakwenda kuifanya ishiriki vyema michuano
ya Afrika.
Kwa sababu hiyo, ujio wa Azam FC
timu inayomilikiwa na Milionea Said Salim Bakhresa ulipokewa kwa furaha na wadau
wa soka nchini, wakijua amepatikana mkombozi wa kweli.
Azam imewekeza fedha nyingi
kuanzia kwenye usajili, ajira za makocha, Uwanja wake kule Chamazi- na kwa
ujumla ni timu ambayo ukiangalia inapoelekea unajenga matumaini.
Azam haina wanachama wa kuleta
mizengwe ya kuvuruga timu, wanaweza kujivuruga wao kwa wao tu.
Mchezaji wa Azam hachezi kwa
presha ya kutukanwa na mashabiki akikosea kama mchezaji wa Yanga au Simba. Azam
imesajili wachezaji nyota kuanzia ndani na nje ya nchi.
Azam inaongoza kutumia fedha
nyingi na kusajili wachezaji bora nchini. Hivyo timu hii inastahili kuwa bingwa
wa nchi kulingana na jinsi ilivyowekeza.
Lakini wasiwasi ni kwamba, mechi
zao zinatiliwa shaka sasa nao kama wanatumia mbinu chafu ikiwemo kuhonga marefa
ili kushinda.
Kama kweli watakuwa wanafanya
hivyo, ina maana watakuwa wanaiga Simba na Yanga, ambazo kimsingi zinanyooshewa
kidole kwa kudumaza maendeleo ya soka ya nchi hii.
Kama Azam wanaiga Simba na Yanga
kununua mechi, wanaweza wakafanikiwa kuwa mabingwa, lakini swali la kujiuliza
soka ya Tanzania itakuwa kweli imepata mkombozi?
Napata shaka sana juu ya
mustakabali wa soka ya nchi hii, ikiwa Azam nayo inakuja kwa staili hii-
dhahiri bado tuna kazi ngumu na safari
ndefu kufikia japo karibu na mafanikio.
Kwa sababu mchezaji akishajua
kwamba kuna unafuu katika mchezo kutokana na mabosi wao kuhonga, hawezi
kujituma tena kwa sababu anajua ushindi upo tu.
Mwaka 2007, baada ya Yanga
kutolewa katika Ligi ya Mabingwa Afrika na Esperance ya Tunisia, aliyekuwa kipa
wa timu hiyo, Ivo Mapunda aliwashauri viongozi wa klabu yake wakati huo, wawe
wanafanya mipango na marefa kurahisisisha mechi.
Tayari mchezaji kujenga dhana
hiyo- inamaanisha amefikia mwisho wa uwezo wake, wakati suluhisho ni kufanyia
kazi mapungufu ili wakati mwingine ufanye vizuri.
Mwaka juzi, Simba ilifungwa 5-0
na Haras El Hodood nchini Misri katika mchezo wa Kombe la Shirikisho, mwaka ilifungwa 3-0 na Wydad Cassablanca,
mara zote ikitolewa katika michuano ya Afrika.
Mwaka huu, imefungwa 3-1 ikitoka
kushinda 2-0 nyumbani na ES Setif moja ya timu tishio tu Afrika na kuingia
hatua ya 16 Bora ya Kombe la Shirikisho.
Hii nini maana yake? Simba
imefanyia kazi mapungufu kutoka kufungwa 5-0, 3-0 na 3-1 sambamba na kusonga
mbele.
Lakini desturi ya kutaka kurahisisisha
kazi kwa kununua mechi- maana yake hatuwezi kufanyia kazi mapungufu.
Kweli wapenzi wa soka Tanzania wanaitegemea
Azam iijengee heshima nchi hii katika michuano ya Afrika, lakini kwa staili
ambayo wanataka kwenda nayo. Hakuna hakika kama watafanikiwa.
Yapo maneno tayari yanasemwa
semwa kuhusu Azam na harakati zao za ubingwa na mbinu wanazodaiwa kutumia hadi
watu wanaodaiwa kutumiwa kutoka kwenye mamlaka husika- japo kwa sasa
tunayachukuliwa kama maneno ya mtaani tu, lakini ipo haja ya kuiangalia Azam
kwa jicho la tatu.
Na tufanye hivyo zaidi kwa
maslahi ya Azam yenyewe na mustakabali wa soka yetu kwa ujumla- kwani wakubwa
hawana cha ziada zaidi ya kufikiria kuchukua chao mapema- lakini inayosulubika
ni soka yetu. Tunasemaje sasa?
Tuendelee kufurahia Azam
ikishinda marefa wa mechi zao wakisulubiwa, au tuambiane ukweli mambo yaende? Tutafakari kwa makini.
0 comments:
Post a Comment