• HABARI MPYA

    Wednesday, September 19, 2012

    HATA VITANDA VYA UWANJA WA FISI MANJI NA JESHI LAKE WAPEWE MUDA YANGA!


    JULAI 14, mwaka huu, mfanyabiashara maarufu nchini, mwenye asili ya Kiasia, Yussuf Mehboob Manji aliingia madarakani Yanga, kufuatia uchaguzi mdogo uliofanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
    Na Mahmoud Zubeiry
    Manji alishinda kwa kishindo kwa pamoja na watu wanne kati ya watano aliopendekeza aingie nao madarakani, Abdallah Ahmed Bin Kleb, George Manyama na Mussa Katabaro, alikosekana Lameck Nyambaya tu katika timu yake, iliyobatizwa jina Jeshi la Miamvuli ambaye badala yake aliingia Aaron Nyanda.
    Watu hawa watano hakika walibeba na bado wamebeba matumaini makubwa ya wana Yanga juu ya taswira mpya ya klabu, kulingana na sera zao wakati wa kampeni- na kwa sababu wote wanaonekana watu wenye uelewa mkubwa, wenye uwezo wa kifedha na kwa ujumla wenye dhamira fulani ya kuifanyia kitu klabu.
    Wiki hii, hawa jamaa wametimiza miezi miwili ya kuwa madarakani na katika kipindi hicho si vibaya kuwapongeza kwa kazi nzuri ya awali waliyofanya ikiwemo kusajili wachezaji wa gharama, kocha wa gharama na kuboresha baadhi ya mambo ndani ya klabu, ikiwemo maslahi ya wachezaji.
    Jeshi la Miamvuli...Hapa Manni anampigia debe Bin Kleb. Wengine kulia ni Manyama na Nyambaya. Kushoto ni Sanga. 
    Lakini kubwa ni kuiwezesha klabu kutwaa kombe la tano la Klabu Bingwa ya soka Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame- kitu ambacho kwa hakika kimewafariji wapenzi wa klabu hiyo kwa kuukosa ubingwa wa Bara msimu uliopita na kufungwa 5-0 na wapinzani wao wa jadi, Simba SC.
    Lakini bado pamoja na hayo, kulingana na hali halisi ya klabu hiyo kwa sasa, yapo mambo ambayo hakika yalitarajiwa kupewa kipaumbele na mabwana wakubwa hawa baada ya kuingia madarakani.
    Natambua hata Rome haikujengwa siku moja, hivyo sitaki kuamini kwa sababu lipo ‘Jeshi la Miamvuli’ Yanga, basi ndani ya siku mbili Yanga itakuwa na hadhi sawa na Tout Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)- la hasha, jamaa wanahitaji muda.
    Pamoja na ukweli huo, lakini yapo baadhi ya mambo madogo madogo yalistahili kupewa kipaumbele, kama ukarabati wa vyumba vya jengo la klabu, kuweka fenicha mpya zenye hadhi.
    Mambo mengine kama uboreshaji wa gym, iwe gym kweli ya kimichezo, ukarabati wa jengo na Uwanja kwa ujumla, kweli hayo yanahitaji muda na hata baada ya miaka miwili watu wanaweza kufanya subira.
    Lakini kutoa zile fenicha zinzofanana na za gesti za Uwanja wa Fisi na kuweka fenicha za kisasa, kutengeneza mabomba yaweze kupandisha maji hadi vyumbani, makabati ya kuhifadhia nguo, Televisheni vyumbani- haya kwa kweli kwa hadhi ya Jeshi la Miamvuli hayahitaji muda.
    Sera kubwa ya Jeshi la Miamvuli ni kubana matumizi, na ukarabati wa vyumba vya wachezaji ni njia mojawapo ya kubana matumizi, ili timu iwe inaweka kambi klabuni na kuepuka gharama za mamilioni ya kulipia hoteli.
    Lazima Manji na jeshi lake wajitofautishe na aina ya viongozi wengine wababaishaji waliowahi kutokea Yanga kwa kuhakikisha wanafanya mambo ambayo yatabadilisha taswira ya klabu.
    Juzi, Kocha Mkuu wa Yanga SC, Mbelgiji Tom Saintefiet alilalamikia kulala kwenye hoteli mbaya, mjini Mbeya yenye vitanda vichache na vidogo, vilivyosababisha watu wakalala mzungu wa nne, na chakula kibaya wakati wa mechi yao ya kwanza ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, dhidi ya wenyeji Prisons, ambayo iliisha kwa sare ya bila kufungana.
    Alisema yeye alilala kitanda kimoja na Louis Sendeu na Mbuyu Twite alibanana na Didier Kavumbangu na hoteli haikuwa na mabomba vyooni wala bafuni, hivyo kulazimika kuingia na ndoo na kuogea kata.
    Alisema pia hoteli hiyo ilikuwa katikati ya mji na karibu na stendi ya mabasi, kila alfajiri kelele nyingi na kwa ujumla timu iliingia uwanjani ikiwa haiko vizuri.
    “Mimi kwa mfano sijaoga siku mbili, kwa kweli tulikuwa katika mazingira magumu na wapinzani wetu walicheza soka ya kuudhi tangu mwanzo, kupoteza muda, na marefa hawakuchukua hatua, tulipoteza nafasi kupitia kwa Kiiza (Hamisi) na Msuva (Simon), siwezi kulaumu mchezaji wangu yeyote, lakini hiyo ndiyo hali halisi,”alisema Saintfiet.
    Baadhi ya watu wanaweza kuchukulia kauli za Mtakatifu Tom kama visingizio baada ya kushindwa kuanza na ushindi katika Ligi Kuu, huku wapinzani wake wakuu, Simba na Azam wakibeba pointi, lakini ukweli ni kwamba tangu anafika Mbeya, Mbelgiji huyo alikerwa na hali hiyo.
    Binafsi nilipofanya naye mahojiano baada ya kufika Mbeya alinielezea hali hiyo, nami nilimfariji tu kwamba hiyo ni hali halisi ya nchi yetu na anapaswa kuvumilia huku akiwaelewesha taratibu viongozi wake.
    Ubingwa wa Kagame ni matunda ya Jeshi la Miamvuli
    Lakini ukweli ni kwamba, Saintfiet alikuwa ana hoja hasa pale aliposema huwezi kusajili mchezaji kwa dola za Kimarekani 60,000 halafu ukamlaza kwenye chumba cha Sh. 15,000.
    Lazima Yanga iendane na hadhi ya viongozi wake- sitaki kuamini akina Seif Ahmad Magari na Abdallah Ahmad Bin Kleb waliopkwenda kwenye mechi hiyo nao walilala katika hoteli hiyo za kuoga na kata.
    Dharau ni neno lenye maana pana sana- na wakati mwingine hata kupuuza ni dharau na mara nyingi dharau husababisha madhara na hii inaonekana kama kuwa desturi ya Yanga kwa miaka ya karibuni.
    Mwaka jana, Yanga walichukua Kombe la Kagame, wakajiona wao ndio wao, wakashindwa kuiandaa timu yao vizuri kwa ajili ya ligi, matokeo yake mwakani hawatashiriki michuano ya Afrika.
    Mwaka huu pia wamechukua Kombe la Kagame, kweli timu ilikuwa na maandalizi ya muda mrefu na ilikwenda kucheza mechi mbili za kujipima nguvu Rwanda- lakini bado kuna mambo madogo madogo ambayo viongozi wanapaswa kuyatilia mkazo na kuacha kudharau.
    Katabaro peke yake akiamua anabadilisha fenicha Yanga nusu saa tu
    Naweza kusema dharau ndiyo iliyosababisha hali iliyotokea Mbeya- na kama wataendelea nayo, Yanga wajue kabisa haitakuwa tofauti na msimu uliopita kwa sababu ligi ya sasa si ile ya bingwa akiwa Simba, Yanga atakuwa wa pili- hapana. Ligi ya sasa ina Azam na washindani wengine wanaonekana kuibuka msimu huu.
    Haya nilikuwa natolea mfano tu, lakini hoja yangu ya msingi leo ni kwamba, yapo mambo ambayo Manji na Jeshi lake la Miamvuli wanaweza kupewa muda, ila baadhi ya mambo hakika hayahitaji muda kama kubadilisha vile vitende vya Uwanja wa Fisi. Alamsiki!
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HATA VITANDA VYA UWANJA WA FISI MANJI NA JESHI LAKE WAPEWE MUDA YANGA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top