![]() |
Mashabiki wa Yanga |
Na Princess Asia
KIINGILIO cha chini katika mashindano ya Kombe la Kagame
yanayoanza Jumamosi (Julai 14 mwaka huu) vitakuwa sh. 5,000 kwa mechi za Yanga
na Simba, na sh. 2,000 kwa mechi ambazo hazihusishi timu hizo. Yanga ni bingwa
mtetezi wakati Simba ni makamu bingwa mtetezi.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniphace
Wambura Mgoyo ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, mechi
zinazohusisha Yanga na Simba viingilio vitakuwa ni viti vya bluu na kijani sh.
5,000, viti vya rangi ya chungwa sh. 7,000, viti vya VIP C sh. 10,000, viti vya
VIP B sh. 15,000 na viti vya VIP A ni sh. 20,000.
Wambura amesema kwamba, siku ambazo Simba na Yanga
hazichezi, viingilio vitakuwa sh. 2,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na
kijani, sh. 5,000 kwa viti vya VIP C, sh. 10,000 kwa viti vya VIP B na sh.
15,000 kwa viti vya VIP A. Mshabiki akikata tiketi moja anaona mechi zote
mbili; mechi ya saa 8 na ile ya saa 10.
Amesema timu za El Salam Wau ya Sudan Kusini na Atletico ya
Burundi zimewasili Dar es Salaam jana usiku (Julai 11 mwaka huu) tayari kwa
mashindano hayo wakati nyingine zote zilizobaki kutoka nje zinawasili leo
katika muda tofauti.
CECAFA leo imetangaza marekebisho madogo ya ratiba ya michuano
hiyo na mechi ya Simba na URA ya Uganda iliyokuwa ichezwe Jumatatu (Julai 16
mwaka huu) sasa itafanyika Jumapili (Julai 15 mwaka huu) kwenye Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam.
CECAFA imefanya mabadiliko hayo kutokana na fainali ya Copa
Coca-Cola 2012 iliyokuwa ichezwe kwenye uwanja huo kuhamishiwa Uwanja wa
Kumbukumbu ya Karume.
Kutokana na mabadiliko hayo, mbali ya mechi ya Simba na URA
itakayoanza saa 10 kamili jioni, mechi nyingine Jumapili itakuwa kati ya Vita
Club ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) dhidi ya Ports ya Djibouti
itachezwa saa 8 kamili mchana Uwanja wa Chamazi.
Pia siku hiyo hiyo ya Jumapili kwenye Uwanja wa Chamazi
kutakuwa na mechi nyingine itakayoanza saa 10 kamili jioni. Mechi hiyo
itazikutanisha timu za Azam ya Tanzania Bara na Mafunzo kutoka Zanzibar.
Mechi za ufunguzi wa mashindano hayo Jumamosi (Julai 14
mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam zitabaki kama zilivyopangwa
awali. Mechi ya kwanza saa 8 mchana itakuwa kati ya APR ya Rwanda na El Salam
Wau ya Sudan Kusini wakati saa 10 kamili jioni Yanga itaoneshana kazi na
Atletico ya Burundi.
0 comments:
Post a Comment