![]() |
| Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Simba SC; Zakaria Hanspop |
Na Mahmoud Zubeiry
MABINGWA wa soka Tanzania, Simba SC, hivi sasa wanakwenda
mbio kwa kasi ya Usain Bolt kukamilisha usajili wao, kabla ya dirisha kufungwa
kesho.
Azam FC wanataka Sh. Milioni 50 kabla ya dirisha la usajili
kufungwa saa 6:00. usiku kesho ili kumuachia kiungo Ramadhan Chombo ‘Redondo’
kesho na hivi sasa Simba SC wapo kwenye kikao kizito kujadili namna ya
kukamilisha usajili wao, kabla ya dirisha hilo kufungwa.
Mapema leo, asubuhi BIN ZUBEIRY iliripoti kwamba, Azam
imekubali kupokea Sh. Milioni 15 kutoka Simba SC ili kumuuza Redondo wa Ngomati
kwa Wekundu hao wa Msimbazi, lakini baada ya kuzama ndani, upande wa pili,
imegundua zinatakiwa Milioni 50 za Tanzania.
BIN ZUBEIRY ilijaribu kumpigia simu, Mwenyekiti wa Kamati ya
Usajili ya Simba SC, Zakaria Hanspop ambaye ‘amecheza bonge la Pele’ dakika za
lala salama kuokoa usajili wa klabu hiyo, ambao ulivurundwa vibaya na ‘Maamuma
wa soka’ waliomo ndani ya klabu hiyo, lakini akasema; “Nipo kwenye kikao,
nipigie baada ya saa moja,”.
Habari za ndani ambazo BIN ZUBEIRY imezipata, zimesema
kwamba Azam wako tayari kupokea fedha kumuuza Redondo, kufuatia viongozi wa
Simba SC kuwaangukia Azam kwa kitendo chao cha kumsajili kiungo huyo bila
kuwasiliana nao, wakati bado alikuwa ana mkataba na Wana Lamba Lamba.
Awali, Azam walikerwa na kitendo hicho hadi wakataka kusitisha
dili la kumtoa kwa mkopo kwa Mrisho Khalfan Ngassa Simba SC.
Azam walimtoa kwa mkopo Ngassa, baada ya kukerwa na kitendo
cha mchezaji huyo kubusu jezi ya timu yake ya zamani, Yanga, katika Nusu
Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, dhidi ya AS
Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) mwezi uliopita.
Alifanya hivyo, baada ya kufunga bao la ushindi akitokea
benchi na kuiwezesha Azam kutinga fainali ya michuano hiyo, ambako walifungwa
na Yanga 2-0, naye kwa mara nyingine akitokea benchi na kushindwa kufunga,
hivyo kutuhumiwa kucheza kinazi.
Ilielezwa kwamba Simba walitoa Sh. Milioni 25 kumnunua kwa
mkopo mchezaji huyo, ingawa baadaye Simba wakasema waliununua mkataba wa mwaka
mmoja aliobakiza mchezaji huyo Azam FC, nao wakamuongezea wa mwaka mmoja kwa
kumsainisha kwa Sh. Milioni 30, kati ya hizo Milioni 12 akipewa taslimu na 18
akipewa gari.
Inavyoonekana, Redondo aliwadanganya Simba kwamba amemaliza
mkataba na Azam, wakaingia mkenge na kumpa Sh. Milioni 30 wakimsainisha mkataba
wa miaka miwili, wakati mkataba wake na Azam unamalizika Juni mwakani.
Hili ni kosa sawa na ambalo Simba walilifanya katika usajili
mwingine wa mchezaji wa Azam, Ibrahim Rajab ‘Jeba’, miezi mitatu iliyopita
ambaye alikuwa kwa mkopo Villa Squad wao wakaenda kumsajili bila kuwasiliana na
klabu yake kujua kuhusu mkataba wake, matokeo yake baadaye mchezaji huyo
akarejea Azam.
Simba nao wana lalamiko kama hilo, dhidi ya watani wao wa
jadi, Yanga wanaowatuhumu kumsajili beki Kevin Yondan, wakati bado ana makataba
na Wekundu hao wa Msimbazi, ingawa TFF iliweka sawa kwa kusema Yondan hakuwa na
mkataba na Simba SC.
Baadaye Simba ilitoa ufafanuzi, kwamba ilimuongezea mkataba
Yondan baada ya ule wa awali kumalizika na ikawa inasubiri muda wa usajili
ufike wauwasilishe TFF. Lakini katika kesi ya awali, Simba walipoupeleka
mkataba wao mpya na Yondan, ulionyesha mchezaji huyo anatakiwa kuanza
kuutumikia mkataba huo, Desemba mwaka huu, hivyo TFF ikasema kwa wakati ambao
yuko huru, aichezee Yanga.
Sakata la Yondan litarudi Desemba, wakati ambao atatakiwa
kuanza kuutumikia mkataba wake na Simba, wakati yupo ndani ya mkataba wa miaka
miwili na Yanga.
Simba pia inafikiria kuvunja mkataba na kiungo Mganda, Mussa
Mudde wakati ikiwa kwenye mazungumzo na wachezaji wanne wengine wa kigeni beki,
wawili kutoka Mali, mmoja Tusker ya Kenya na mshambuliaji kutoka Ivory Coast,
ambao imeelezwa wanaweza kuwasili leo kujiunga na timu hiyo.
Tayari Simba imeacha kiungo mmoja wa kigeni, Kanu Mbivayanga
kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na kusajili beki Paschal Ochieng
kutoka AFC Leopard ya Kenya na mshambuliaji Daniel Akuffo kutoka Hearst Of Oak
ya Ghana, ambaye pia raia wa Ivory Coast.
Habari kutoka Arusha, ambako Simba imeweka kambi kujiandaa
na msimu mpya wa Ligi Kuu, zimesema kwamba katika siku ya kwanza ya mazoezi yao
na kikosi hicho leo, wachezaji wote hao wawili wameonyesha viwango vya hali ya
juu.
Imeelezwa kwamba, mshambuliaji Akuffo ni hatari mno na kwa
haraka haraka hakuna wa kumfananisha naye kati ya washambuliaji wote waliopo
Tanzania kwa sasa.
Anasifiwa kuwa na uwezo mkubwa wa kumiliki mpira, kasi,
nguvu, ufundi na mbinu za kimchezo- maana yake Wekundu wa Msimbazi wamelamba
dume. Kama wachezaji wapya wanaotua leo watamridhisha kocha Mserbia, Profesa
Milovan Cirkovick, Simba itamtema Mudde na kubaki na idadi ya wachezaji wa
kigeni watano kama inavyoelekeza kanuni ya usajili ya Ligi Kuu kuhusu wachezaji
wa kigeni.
Wachezaji wengine wa kigeni kwenye kikosi cha Simba SC ni
washambuliaji Mganda Emmanuel Okwi na Mzambia Felix Sunzu.



.png)
0 comments:
Post a Comment