Kiiza |
Na Mahmoud Zubeiry,
Kampala
MSHAMBULIAJI
wa Uganda, Hamisi Kiiza ‘Diego’ amesema John Raphael Bocco ‘Adebayor’ wa
Tanzania Bara ni mkali, lakini ajue The Cranes ina ukuta ambao haujaruhusu hata
bao moja, hivyo asitarajie kufunga bao kesho katika Nusu Fainali ya Kombe la
Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Tusker Challenge.
Akizungumza
na BIN
ZUBEIRY jana, Uwanja wa Mandela, Namboole, Kiiza alisema kwamba
anamfahamu Bocco na kwenye Challenge ya mwaka huu anang’ara sana, lakini kesho
atakutana na ukuta wa wanaume wa shoka.
“Tunaiheshimu
Tanzania ni timu nzuri, na zaidi mfumo wao wanaocheza hivi sasa ni mzuri sana, lakini
hata sisi ni wazuri, hiyo mechi itakuwa kali sana,”alisema mshambuliaji huyo wa
klabu ya Yanga SC ya Dar es Salaam.
Kiiza
alisema mbali na Bocco, Tanzania Bara ina mchezaji mwingine hatari, Mrisho
Ngassa lakini wote wajue kwamba watakutana na ukuta wa Uganda, ambao katika
mechi nne haujaruhusu hata bao moja.
Uganda jana
ilifuzu kuingia Nusu Fainali ya Challenge, baada ya kuifunga Ethiopia mabao
2-0, ambayo yalitiwa kimiani na Geoffrey Kizito dakika ya nne na Robert
Ssentongo dakika ya 60.
Kwa ushindi
huo, Uganda itamenyana na Tanzania Bara katika Nusu Fainali Alhamisi usiku,
mchezo ambao utatanguliwa na Nusu Fainali nyingine kati ya Kenya na Zanzibar,
itakayoanza saa 10:00 jioni.
Kenya ilifuzu
Nusu Fainali jana, baada ya kuifunga Malawi 1-0, bao pekee la Mike Barasa dakika
ya 56.