• HABARI MPYA

    Friday, August 17, 2012

    MEXIME ATOA RAI KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU WAZAWA


    Mecky Mexime
    Na Princess Asia
    KOCHA wa Mtibwa Sugar ya Morogoro, Mecky Mexime ameshauri vyombo vya habari nchini viache kushobokea wachezaji wa kigeni, badala yake visaidie kupromoti wachezaji wa nyumbani, ambao anaamini wana uwezo mkubwa kuliko hata hao wageni.
    Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, Nahodha huyo wa zamani wa timu ya taifa, Taifa Stars, alisema kwamba hapendi kuona wachezaji wa kigeni wanashobokewa kupita kiasi wakati Tanzania kuna wachezaji wazuri.
    “Tumeona vijana wadogo wa Simba wakicheza soka nzuri na kuifunga Azam iliyokuwa na wachezaji wa kigeni na kocha wa kigeni pia. Lakini pia mfano mwingine ni sisi Mtibwa, tunatumia wachezaji wa kigeni na kila mwaka Simba na Yanga zinakuja kwetu kuchukua wachezaji kule,”alisema beki huyo wa zamani hodari nchini.
    Mexime alimtolea mfano mshambuliaji Said Bahanuzi, akisema kwamba kijana huyo ametokea Mtibwa kwenda Yanga ambako moja kwa moja ameibuka mfungaji bora wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
    Maxime juzi aliiwezesha Mtibwa Sugar kutinga Fainali ya michuano ya BankABC Sup8R kwa kishindo, baada ya kuinyuka Jamhuri ya Pemba, mabao 5-1, ambayo yalitiwa kimiani na Babu Ally Seif dakika ya 15, Salvartoy Ntebe dakika ya 17, Mfaume Shaaban aliyejifunga dakika ya 38, Vincent Barnabas dakika ya 43 na Awadh Juma dakika ya 85 wakati la kufutia machozi la Jamhuri lilifungwa na Mbarouk Chande dakika ya 62.
    Mtibwa ambayo itacheza na Simba SC kwenye fainali kesho, ndio timu pekee ambayo haijapoteza pointi hata moja kwenye mashindano hayo baada ya kushinda mechi zake zote tatu za Kundi B, 2-1 dhidi ya Polisi Moro, 2-0 dhidi ya Azam na 5-0 dhidi ya Super Falcon na jana 5-1 dhidi ya Jamhuri katika Nusu Fainali.
    Simba B yenyewe ilitoa sare moja tu ya kufungana 1-1 na Jamhuri katika mchezo wa kwanza, lakini mechi zake nyingine ilizifunga 2-0 kila timu, Mtende na Zimamoto ya Zanzibar. 

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MEXIME ATOA RAI KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU WAZAWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top