• HABARI MPYA

    Saturday, September 15, 2012

    SUPER FALCON YAENDELEA KUGAWA POINTI LIGI KUU ZANZIBAR


    Na Ally Mohamed, Zanzibar
    LIGI Kuu ya Zanzibar, maarufu Zanzibar Grand Malt Premier League, leo imeingia katika mzunguko wa pili kwa kushuhudia michezo miwili katika viwanja viwili tofauti, kwenye Uwanja wa Amaan, Mabaharia wa KMKM wakiibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Malindi.
    Malindi, ndio waliokuwa wa kwanza kupata bao sekunde ya 57 lililofungwa na mshambuliaji, Issa Hamad ambaye ameandika histotia kwa kufunga bao la mapema zaidi tangu ligi hiyo kuanza wiki iliyopita. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko na kipindi cha pili KMKM iliwachukua dakika mbili tu tangu KMKM kusawazisha kupitia kwa Mudrik Muhib.
    KMKM wakiendelea kulisakama lango la Malindi hatimaye juhudi zao zikazaa matunda katika dakika ya 90 kufuatia bao la pili na la ushindi lililofungwa na Maulid Kapenta.
    Katika mchezo mwingine uliopigwa kwenye Uwanja wa Gombani, Pemba Super Falcon ambao ni wawakilishi wa Zanzibar katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika walikubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Duma, mabao yote mawili ya Duma yakifungwa na Vuai Abdallah katika dakika ya 55 na 66, huku bao pekee la Super Falcon likifungwa na Mohammed Salum.
    Ligi hiyo itaendelea tena kesho kwa michezo miwili, ambapo katika uwanja wa Amaan kisiwani Unguja, Mafunzo wataikaribisha timu ya Bandari iliyopanda daraja msimu huu, na huko kisiwani Pemba, Chipukizi watacheza na washindi wa pili wa ligi iliyopita klabu ya Jamhuri ambao wana tiketi ya kushiriki katik kombe la Shirikisho hapo mwakani mechi itakayochezwa katika uwanja wa Gombani.
    Wakati huo huo: Wadau wa soka visiwani Zanzibar wamepata mashaka juu ya ushiriki wa klabu ya Super Falcon ambayo itaiwakilisha Zanzibar katika Ligi ya Mabingwa mwakani kutokana na kiwango kibovu kinachooneshwa na timu hiyo katika mechi zake za hivi karibuni.
    Itakumbukwa kuwa mpaka sasa klabu ya Super Falcon, ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Zanzibar,  wameshacheza mechi saba bila kupata pointi hata moja, wakipoteza mechi zote tatu za hatua ya makundi ya michuano ya BancABC Super8, kabla ya kufungwa 3-1 na Jamhuri katika mechi ya kuwania Ngao ya Jamii, kabla ya kufungwa mabao 2-0 na Coastal Union katika mechi ya kirafiki kujiandaa na ligi kuu ya Zanzibar, wakifungwa mabao 2-0 katika mechi yao ya kwanza ya Ligi Kuu ya Zanzibar na leo wakilala mabao 2-1 kutoka kwa Duma.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SUPER FALCON YAENDELEA KUGAWA POINTI LIGI KUU ZANZIBAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top