• HABARI MPYA

    Friday, September 21, 2012

    YANGA WAHAMISHA KAMBI JANGWANI

    Ally Mustafa 'Barthez' akiteremka kwenye basi Uwanja wa Jamhuri, Morogoro juzi.

    Na Mahmoud Zubeiry
    KAMBI inahama. Yanga waliingia kambini jana, makao makuu ya klabu yao, makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, lakini leo hawatalala hapo tena.
    Habari kutoka ndani ya Yanga zimesema kwamba kambi inahama kwa sababu mazingira ya hosteli hiyo ya klabu kwa ujumla si mazuri- na zaidi kuwaepushia wachezaji usumbufu kutoka kwa baadhi ya wanachama wenye desturi mbaya.
    Hatua ya Yanga kuingia kambini  inafuatia kuambulia pointi moja katika mechi mbili za Ligi Kuu, ikitoa sare na Prisons 0-0 mjini Mbeya Jumamosi na kufungwa 3-0 na Mtibwa Sugar mjini Morogoro jana.
    Meneja wa Yanga, Hafidh Saleh aliwataja wachezaji 30 walioingia kambini hiyo jana kujiandaa na mchezo wa Jumamosi dhidi ya JKT Ruvu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuwa ni Nizar Khalfan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Shamte Ally Kilalile, Said Rashid Bahanuzi, Haruna Niyonzima Fadhili, Didier Kavumbagu Fortine, Juma Seif Dion ‘Kijiko’, Nadir Haroub Ally ‘Cannavaro’, Nurdin Bakari Hamad, Said Mohamed, Rashid Omary Gumbo, Juma Jaffar Abdul, Omega Sunday Seme na Kevin Yondan Patrick.
    Wengine ni Jerson John Tegete, Idrisa Rashid Abdallah, Godfrey Taita Magina, Oscar Joshua Nkulula, David Charles Luhende, Ibrahim Job Isaac, Ladislaus Mbogo Mahendeka, Ally Mustafa Mtinge ‘Barthez’, Shadrack Joel Nsajigwa, Hamisi Friday Kiiza, Yaw Koffi Berko, Stephano Asangalwisye Mwasyika, Mbuyu Twite Banza, Simon Msuva, Frank Domayo na Issa Ngao.
    Wakati Yanga wanakumbuka kambi baada ya kupoteza pointi tano katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu, tangu wamerejea kutoka Arusha wiki wiki mbili zilizopita, wapinzani wao wa jadi, Simba SC wamekuwa kambini hoteli ya Sapphire, Kariakoo, Dar es Salaam.
    Kuanza vibaya kwa Yanga katika Ligi Kuu kumeibua maswali na maoni mengi, kocha akisema wachezaji wamevimba vichwa na hawajitumi tena, jambo ambalo limeungwa mkono na uongozi ambao sasa unawaweka chini ya uangalizi maalum wachezaji hao.
    Saintfiet alisema kwamba wachezaji wake wamelewa sifa baada ya mwanzo mzuri wa msimu na kila mmoja sasa anajiona ‘staa’ kiasi cha kutocheza kwa kujituma, hali ambayo imechangia timu yake kuanza vibaya katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana, Mtakatifu Tom alisema kwamba wachezaji wanatakiwa kubadilika haraka, vinginevyo mabadiliko yatahitajika katika timu.
    “Nimesononeshwa mno tena, na ninaomba radhi kwa mashabiki, wanastahili ushindi, tuna mashabiki wazuri, katika mechi (ya juzi) tulipata nafasi nane nzuri asilimia 100, mita tano kutoka langoni kwa wapinzani, tulipoteza hadi penalti. Si kawaida,”.
    “Mtibwa Sugar si timu mbaya, walipata nafasi nne na wakafunga mabao matatu, mashuti mawili ya kiwango cha dunia. Kama tusingetengeneza nafasi, ingekuwa rahisi kwangu kama kocha kulaumiwa, lakini sasa sisi makocha hatuwezi kupiga mpira kupeleka nyavuni, na wachezaji ndio wanatakiwa kufanya hivyo,”.
    “Hii inauma, kufanya vizuri Kombe la Kagame na kuanza vibaya katika ligi, wachezaji fulani si wachezaji tena, wanajiona mastaa, hivyo wanatakiwa kuzinduka haraka, vinginevyo mabadiliko yanahitajika,”alisema Mtakatifu Tom.
    Mechi ya juzi ilikuwa ya pili kwa Yanga kufungwa chini ya Saintfiet tangu aanze kazi Julai mwaka huu, akirithi mikoba ya Mserbia, Kostadin Bozidar Papic aliyetupiwa virago, katika mechi 14 alizoiongoza timu hiyo hadi sasa, ambazo ndani yake zipo sita za Kombe la Kagame, aliloiwezesha timu hiyo kutwaa. 
    Yanga iliyoanza ligi kwa sare ya bila kufungana na Prisons mjini Mbeya, juzi ilifungwa 3-0 na Mtibwa Sugar katika mchezo wake wa pili, kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WAHAMISHA KAMBI JANGWANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top