• HABARI MPYA

    Tuesday, September 18, 2012

    YANGA WAIFUATA MTIBWA SUGA LEO

    Yanga SC

    Na Mahmoud Zubeiry
    YANGA SC inatarajiwa kuondoka leo saa nane mchana kwa njia ya basi kwenda Morogoro, tayari kwa mchezo wa kesho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, dhidi ya wenyeji Mtibwa Sugar, kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
    Huo utakuwa mchezo wa pili kwa Yanga katika ligi hiyo, baada ya awali kulazimishwa sare ya bila kufungana na Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya Jumamosi.
    Kocha Mkuu wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintfiet jana aliwaomba radhi mashabiki wa Yanga kwa sare ya Jumamosi kwenye Uwanja wa Sokoine na akawatupia lawama viongozi wa klabu hiyo, kwa maandalizi mabovu.
    Lakini Mbelgiji huyo amesema leo anapeleka wachezaji 18 Morogoro kwa ajili ya mechi ya pili ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar, akiwa ana matumaini makubwa ya ushindi.
    Saintfiet alilalamikia kulala kwenye hoteli mbaya, yenye vitanda vichache na vidogo, vilivyosababisha watu wakalala mzungu wa nne, na chakula kibaya na kwa ujumla alisema hawakuwa vizuri kabla ya mechi hiyo.  Alisema yeye alilala kitanda kimoja na Louis Sendeu na Mbuyu Twite alibanana na Didier Kavumbangu na hoteli haikuwa na mabomba vyooni wala bafuni, hivyo kulazimika kuingia na ndoo na kuogea kata.
    Alisema pia hoteli hiyo ilikuwa katikati ya mji na karibu na stendi ya mabasi, kila alfajiri kelele nyingi na kwa ujumla timu iliingia uwanjani ikiwa haiku vizuri.
    “Mimi kwa mfano sijaoga siku mbili, kwa kweli tulikuwa katika mazingira magumu na wapinzani wetu walicheza soka ya kuudhi tangu mwanzo, kupoteza muda, na marefa hawakuchukua hatua, tulipoteza nafasi kupitia kwa Kiiza (Hamisi) na Msuva (Simon), siwezi kulaumu mchezaji wangu yeyote, lakini hiyo ndiyo hali halisi,”alisema Saintfiet.
    Baada ya mazoezi ya asubuhi kwenye Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam na saa 8:00 mchana watasafiri kwa njia ya barabaraba kwenda Morogoro ambako wakifika watatafuta hoteli nzuri mapema.
    Alisema anajua hata Uwanja wa huko, Jamhuri si mzuri na mechi itakuwa ngumu kwa sababu Mtibwa Sugar nao walitoka sare ya bila kufungana na Polisi katika mchezo wao wa kwanza Jumamosi na anaiheshimu timu hiyo kama moja ya timu tano kubwa Tanzania, pamoja na Simba, Azam na Coastal Union.
    “Lakini pamoja na kwamba Simba wamependelewa kupangiwa ratiba ya kuanza kucheza nyumbani mechi tano mfululiuzo, nakuambia Mei mwaka 2013 Yanga ndio itavishwa taji la ubingwa wa Ligi Kuu, acha wafurahie sasa hivi, watalia mwisho,”alisema Mtakatifu Tom.
    Kuhusu wachezaji 18 anaokwenda nao Morogoro, Mtakatifu Tom alisema atawataja baada ya mazoezi ya leo na hiyo inaonekana ni kwa sababu ya kufuatilia hali za wachezaji ambao kwa sasa hawako vizuri, akiwemo kiungo Haruna Niyonzima.
    Wachezaji aliokwenda nao Mbeya walikuwa ni makipa; Yaw Berko, Ally Mustafa ‘Barthez’, mabeki Shadrack Nsajigwa, Juma abdul, Godfrey Taita, Mbuyu Twite, Kevin Yondan,  Nadir Haroub ‘Cannavaro’, David Luhende, Oscar Joshua na Stefano Mwasyika.
    Aliwataja viungo ni Athumani Iddi ‘Chuji’, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Rashid Gumbo, Nizar khalfan, Shamte Ally na Simon Msuva, wakati washambuliaji ni Jerry Tegete, Didier Kavumbangu, Said Bahanuzi na Hamisi Kiiza, wakati waliobaki walikuwa ni  kipa Said Mohamed, mabeki Ladislaus Mbogo, Job Ibrahim, viungo Juma Seif ‘Kijiko’, Salum Telela, Omega Seme, Nurdin Bakari, Idrisa Assega na Issa Ngao wa Yanga B, anayekomazwa kikosi cha kwanza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WAIFUATA MTIBWA SUGA LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top