• HABARI MPYA

    Wednesday, August 08, 2012

    YANGA MAZOEZINI ASUBUHI YA LEO MABIBO

    Yanga mazoezini

    Na Prince Akbar
    MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, Yanga SC ya Dar es Salaam leo wanatarajiwa kuanza tena mazoezi ya kujiandaa na Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya mapumziko ya siku mbili, yaliyotokana na ziara yao ya Bungeni Dodoma Jumatatu.
    Yanga, ambao juzi walionyesha Kombe lao ubingwa wa Kagame, katika ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mjini Dodoma, walirejea Dar es Salaam jana lakini kutokana na wachezaji wake kuchoka, hawakufanya mazoezi.
    Yanga, waliotwaa Kombe hilo mara mbili mfululizo sasa, walifanya mazoezi ya mwisho Jumapili asubuhi kabla ya safari ya Dodoma na sasa watafanya tena mazoezi leo, saa 3:00 asubuhi katika Uwanja wa Loyola, Mabibo, Dar es Salaam.
    Yanga ilitwaa Kombe la Kagame kwa mara ya pili mfululizo wiki iliyopita, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Azam FC mabao 2-0, ambayo yalitiwa kimiani na Hamisi Kiiza ‘Diego Milito’ na Said Bahanuzi ‘Spider Man’.
    Hiyo kwa ujumla ilikuwa mara ya tano mfululizo, Yanga inatwaa Kombe hilo, baada ya awali kuchukua mwaka jana, wakiifunga Simba katika fainali bao 1-0, Uwanja wa Taifa mfungaji Kenneth Asamoah ambaye ametemwa, ingawa siku hiyo Kiiza pia alifunga bao safi, ambalo refa alilikataa.
    Yanga ilichukua kwa mara ya kwanza Kombe hilo, mwaka 1975 ikiifunga tena Simba katika fainali, mabao 2-0 wafungaji Sunday Manara ‘Computer’ na Gibson Sembuli (sasa marehemu) Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Ikachukua tena mwaka 1993, Uwanja wa Nakivubo, Kampala, Uganda kwa kuifunga SC Villa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na Said Nassor Mwamba ‘Kizota’ (sasa marehemu) na Edibily Jonas Lunyamila.
    Ilichukua tena mwaka 1999, ikiifunga tena SC Villa, Uwanja wa Nakivubo, kwa penalti 5-3, kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 120, Yanga ikisawazisha bao kupitia kwa Lunyamila, baada ya Hassan Mubiru kutangulia kuifungia Villa, siku hiyo Manyika Peter akicheza penalti mbili za Waganda.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA MAZOEZINI ASUBUHI YA LEO MABIBO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top