![]() |
| Simba SC; Mabingwa watetezi |
Na Mahmoud
Zubeiry
HATIMAYE
michuano mikubwa kabisa ya soka nchini, ijulikanayo kama Ligi Kuu ya Vodacom
Tanzania Bara inarejea tena kwa mara ya 49 tangu ilipoanzishwa mwaka 1965 kwa
wigo finyu na hali dunia kabisa, ikishirikisha klabu za Dar es Salaam pekee. Aliyekuwa
kocha wa timu ya taifa ya Tanganyika kutoka Yugoslavia, Milan Celebic,
aliposhauri kuwapo kwa michuano ya kusaka klabu bingwa ya taifa, ili kujenga
mazingira ya kupata wachezaji wazuri zaidi wa timu ya taifa.
Alisema
kama kutakuwa na ligi, ina maana wachezaji watakuwa wamepata mazoezi ya muda
mrefu katika kujiandaa na ligi, hivyo kuwa rahisi kwake kama mwalimu wa taifa
wakati huo kuona wachezaji walio fiti na kuwachukua kwenye timu ya taifa.
FAT
ilikubali ushauri huo na kuanzisha Klabu bingwa ya taifa, ambayo ilifanyika kwa
mara ya kwanza mwaka 1965, ikishirikisha timu sita tu zilizoteuliwa ambazo ni
TPC ya Moshi, Sunderland (sasa Simba SC), Yanga na Tumbaku ya Kurasini, Dar es
Salaam, Coastal Union na Manchester United, zote za Tanga.
Michuano
hiyo ya kwanza ilifanyika katika viwanja vya Ilala (sasa Karume) na Manispaa wa
Tanga, sasa Mkwakwani na tatizo kubwa lililojitokeza na viongozi wa klabu,
wachezaji na hata viongozi wa FAT, ni kutozielewa vyema kanuni na sheria za
mchezo, hata ikasababisha Yanga wakajitoa na ubingwa ukatolewa kwa Sunderland
(Simba) walioweka historia ya kuwa mabingwa wa kwanza nchini.
Lakini
awali ya hapo, historia inasema kwamba ligi ilikuwa inachezwa Dar es Salaam
pekee tangu mwaka 1929, ikishirikisha timu za Cosmopolitan, Battalion King's
African Rifles (KAR), Gymkhana Club, Tanganyika Territorial Police, Tanganyika
Railways, Government School na Government Services.
Kwa
muhtasari hivyo ndivyo ilivyoanzishwa Ligi Kuu ya nchi hii, ambayo ilianza kwa
mfumo wa mtoano hadi 1982 ilipoanza kuchezwa kama Ligi Daraja la Kwanza na
mwaka 1996 ikabadilishwa na kuwa Ligi Luu.
Mwaka
1997 ilipata udhamini wa kwanza wa Safari Lager Beer hadi 2001 na tangu mwaka
2002 imekuwa ikidhaminiwa na Vodacom Tanzania. BIN ZUBEIRY inakuletea
wasifu wa timu 14 zinazoshiriki ligi hiyo kwa muhtasari.
AZAM FC:
Ilipanda
Ligi Kuu kwa mara ya kwanza mwaka 2008 na moja kwa moja kuwa moja ya timu za
ushindani katika ligi hiyo, msimu uliopita ikiipiku Yanga na kushinda nafasi ya
pili hivyo kujikatia tiketi ya kucheza Kombe la Shirikisho Afrika mwakani.
Linapokuja
swali nani atatwaa ubingwa wa Ligi Kuu, timu zitakazotangulizwa, mbali na
‘wenye ligi yao’ Simba na Yanga, Azam itafuatia na hilo limetokana mwendelezo
mzuri wa timu hiyo katika kutoa ushindani kwenye ligi hiyo.
Mafanikio
mengine makubwa kwa Azam msimu uliopita, mbali na kutwaa Medali ya Fedha katika
Ligi Kuu, ni kutwaa Kombe la Mapinduzi na kushika nafasi ya pili katika Kombe
la Urafiki na Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
![]() |
| Azam FC |
Msimu
huu itakuwa chini ya kocha Mserbia, Boris Bunjak aliyerithi mikoba ya
Muingereza Stewart John Hall aliyefukuzwa baada ya Kombe la Kagame, Julai,
mwaka huu.
KAGERA SUGAR:
Hii
ni timu imara na yenye sifa tatu za kipekee- inazalisha vipaji vingi ambavyo
vinachukuliwa na timu kubwa, haijawahi kushuka daraja tangu ipande mwaka 2005
na ni timu pekee, inayohofiwa na “Top Three’ wote wa Ligi Kuu, Simba, Azam na
Yanga, iwe kwa mechi za nyumbani au ugenini, Kagera Sugar ni wazuri.
Mafanikio
makubwa zaidi kwa Kagera Sugar yalikuja msimu wa 2006, ilipoweza kutwaa Kombe
la Tusker, linaloshirikisha timu za Afrika Mashariki, ikiifunga Simba kwenye
fainali mabao 2-1, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambao sasa umebadilishwa jina
na kuwa Uhuru na wakati wote imekuwa na kocha mmoja anayefanya kazi chini ya
makocha wakuu, winga wa zamani wa Simba, Mrage Kabange.
![]() |
| Kagera Sugar |
Msimu
uliopita Kabange alifanya kazi chini ya Mganda, Mayanja Jackson, lakini msimu
huu atakuwa chini ya mshambuliaji bora wa zamani wa kimataifa wa Tanzania,
Abdallah ‘King’ Kibadeni, babu mmoja mtaalamu sana na mwenye kuijua soka ya
Tanzania kinagaubaga, lakini anatolewa dosari chache tu za kibinadamu.
MTIBWA SUGAR:
Ngumu
kujua kuna tatizo Mtibwa Sugar hata imeondoka katika orodha ya timu za upinzani
Ligi Kuu na kubaki washiriki wa kawaida tu, wanaocheza ili kutoshuka daraja.
Inatoa wachezaji wazuri kila msimu ambao wanapapatikiwa na timu kubwa, lakini
imeshindwa kabisa kurejesha makali yake iliyoingia nayo kwenye soka ya
Tanzania.
Hii
ni timu pekee nje ya Simba na Yanga kuwahi kutetea ubingwa wa Ligi Kuu msimu wa
1999 na 2000, ambayo pia imewahi kuiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya
Afrika, lakini kwa sasa imekuwa ya kufungwa hadi na Simba B kwenye fainali ya
Kombe. Kuna nini pale Manungu?
![]() |
| Mtibwa Sugar |
Pamoja
na yote, Mtibwa inabakia kwenye orodha ya timu zenye heshima katika Ligi Kuu na
kulingana na mabadiliko ya benchi la ufundi iliyofanya msimu huu, Nahodha wake
wa zamani, Mecky Mexime akipewa Ukocha Mkuu- badala ya Mkenya Thom Olaba, kuna
matarajio mapya.
TOTO AFRICAN:
Sifa
kubwa ya Toto African katika Ligi Kuu ni kuitoa nishai Simba, ingawa msimu
uliopita ‘waliwachenjia’ hadi baba zao, Yanga SC. Hawa ndio wakombozi wa soka
ya Mwanza kwa sasa, ambao kwa muda mrefu ilikuwa inabebwa na Pamba FC ‘TP
Lindanda’, iliyopotea kabisa katika ramani ya soka ya Tanzania.
Kitu
kimoja tu, Toto haijafikia makali ya Pamba na ina kazi kubwa ya kupambana
kufikia heshima hiyo, jambo ambalo ukiitathmini kwa kina timu hiyo, unagundua
inaweza iwapo itaamua, kwa maana ya kujipanga vizuri.
Mwanza
ni mkoa ambao una matajiri wengi ambao kama wangeamua kuwekeza kwenye timu
hiyo, ingekuwa tishio, ila katika hilo, kikwazo kinatajwa kuwa ni ‘Uyanga wao’.
Ndio, Uyanga- kwa sababu timu hiyo inamilikiwa na tawi la Yanga mkoani Mwanza,
liliopo Mtaa wa Kishamapanda, ingawa Yanga yenyewe haina msaada wowote wa maana
kwa timu hiyo.
![]() |
| Toto African |
Msimu
huu, Toto itaendelea kuwa chini ya kocha John Tegete ambaye msimu uliopita
alipitia wakati mgumu sana akiwa na timu hiyo kutokana na matokeo mabaya,
yaliyofanya iponee chupuchupu kushuka daraja.
POLISI MOROGORO:
Tangu
kupotea kwa zama za utawala wa Reli katika soka ya Morogoro, Polisi ilikuwa
timu nyingine rasmi iliyorithi joho hilo, lakini bado imekosa msingi imara wa
kuifanya iwe timu ya kudumu katika ligi hiyo.
Polisi
imerejea msimu huu katika ligi hiyo, baada ya kushuka misimu miwili iliyopita
na ikiwa chini ya kocha mkongwe, John Simkoko ambaye aliipa Mtibwa Sugar
ubingwa wa Ligi Kuu msimu wa 1999/2000 na yeye mwenyewe alitwaa ubingwa huo kama
mchezaji mwaka 1975 akiwa na Mseto FC ya Morogoro.
Kwa
kuwa Simkoko ni mtaalamu wa kufundisha soka ya kitabuni, hapana shaka Polisi
itakuwa kivutio katika ligi, haswa ikiongozwa na mfungaji bora wa zamani wa
Ligi Kuu, Abdallah Juma inatarajiwa kabisa kutoa ushindani.
JKT MGAMBO:
Hii
ni timu mpya kabisa katika historia ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara,
ambayo inatarajiwa kuleta changamoto mpya katika ligi hiyo.
Kwa
mara ya kwanza baada ya muda mrefu, Tanga itakuwa na timu mbili tena katika Ligi
Kuu tangu kutoweka enzi za Coastal Union na African Sports.
Tofauti
tu ni kwamba, safari hii timu moja inatoka nje ya mji, wilaya ya Muheza, Mgambo
JKT na wengine, Coastal wapo barabara ya 13 Tanga mjini.
Mgambo
inafundishwa na kocha maarufu wa timu za Jeshi la Wananchi, Matata Steven
aliyewahi kuinoa Transit Camp katika Ligi Kuu miaka minne iliyopita, Steven
Matata.
JKT OLJORO:
Inaingia
katika msimu wake wa pili kwenye Ligi Kuu tangu ipande, ikiibeba soka ya Arusha
kwa sasa baada ya AFC, zamani Ndovu kufulia.
Msimu
uliopita Oljoro ilitisha kidogo baada ya kuanza vizuri mzunguko wa kwanza wa
Ligi Kuu, lakini mzunguko wa pili ikapoteza makali yake na kumaliza ligi kwa
kusuasua.
Ni kama
wamejipanga upya hivi, na msimu huu ikiwa chini ya kocha mpya, kipa wa zamani
wa Yanga na Tukuyu Stars ya Mbeya, Mbwana Makatta, Oljoro inatarajiwa kufanya
vizuri.
JKT RUVU:
R.I.P.
Jackson Lema, Meja wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ)
aliyeipandisha JKT Ruvu na kuunda timu imara, ambayo ilizaa timu nyingine ya
Ligi Kuu, Ruvu Shooting, enzi zake JKT ilikuwa inatisha katika soka ya
Tanzania.
Lakini
tangu kufariki kwa Meja Lema timu hizo zote za JKT zimepoteza makali yake-
japokuwa zimeendelea kuzalisha wachezaji bora, wanaopapatikiwa na timu kubwa,
mfano kiungo chipukizi Frank Domayo aliyesajiliwa Yanga msimu huu.
![]() |
| JKT Ruvu |
Labda
msimu huu, JKT inayofundishwa na mchezaji wa zamani wa Yanga, Charles Kilinda
itabadilika na kuonyesha ushindani katika ligi hiyo.
RUVU SHOOTING:
Msimu
uliopita kidogo ilisisimua katika Ligi Kuu kutokana na kuonyesha soka safi na
ushindani pia, ingawa iliishia kuchezea kubaki Ligi Kuu.
Hii
ni timu ambayo ilitoka ubavuni mwa JKT Ruvu enzi za Meja Jackson Lema, ambaye
baada ya kuna wachezaji wengi, akaamua kuunda timu B, ambayo baadaye iliingia
kwenye ligi na kuopanda hadi Ligi Kuu.
Kwa
sasa timu hii inafundishwa na Nahodha wa zamani wa Yanga, Charles Boniface
Mkwasa ambaye misimu mitatu iliyopita alishindwa kutekeleza majukumu yake
vizuri jeshini kutokana na majukumu ya timu ya taifa ya wanawake, Twiga Stars.
![]() |
| Ruvu Shooting |
Lakini
Mkwasa amebwaga manyanga Twiga Stars, maana yake sasa anapata muda wa kutosha
wa kuiandaa Ruvu Shooting na pia kuifanya iwe ya ushindani Ligi Kuu.
AFRICAN LYON:
Ni
timu yenye historia ya kusimulika ingawa haijawahi kutwaa taji lolote, kutokana
na hadi sasa kuwa imepitia mikononi mwa wamiliki watatu, wafanyabiashara wa
soko la Mbagala, Mbunge Mohamed Dewji na sasa Rahim Kangezi ‘Zamunda’, ambaye
inadaiwa anapewa sapoti na Seattle Sounders FC ya Marekani.
Kwa
mara ya kwanza, African Lyon itakuwa chini ya kocha wa kigeni, Muargentina
Pablo Ignacio Velez, ambaye kihistoria anakuwa Mzungu wa pili tangu, Mreno Eduardo Arroja Almeida
aliyeletwa na Mo Dewji mara timu hiyo ilipopanda tu Ligi Kuu mwaka 2009.
![]() |
| African Lyon |
Msimu
huu, Lyon imekuja na sera mpya ya kutumia vijana zaidi, na imefukuza wachezaji
wengi wakongwe, ili kujenga msingi mpya. Zamunda ni mtu mwenye mipango mingi
sana na kama ataendelea hivyo, iko siku Lyon itakuwa ‘habari nyingine’.
COASTAL UNION:
Siyo
Coastal ile walioizoea wengi, tarajia Coastal mpya kabisa msimu huu, ikiwa
inajivunia udhamini wa Nassor Bin Slum na Simba Cement, imewekeza mno kwa ajili
ya msimu huu wa Ligi Kuu.
Kwanza,
Coastal imesajili mseto mzuri wa wachezaji, wakongwe na chipukizi, wakiwemo
hata kutoka nje ya nchi.
Na
hata katika maandalizi, Coastal ilikuwa na maandalizi mazuri na itakumbukwa
ilikwenda Kenya, Morogoro, Dar es Salaam na kumalizia na Zanzibar, ikicheza
mechi zisizopungua 10 za kujipima nguvu.
![]() |
| Coastal Union |
Ikiwa
chini ya Kocha Mkuu, mshambuliaji wake wa zamani, Juma Mgunda, anayesaidiwa na
Habib Kondo, beki wa zamani wa Pan African, Coastal inatarajiwa kuingilia kati
anga za Azam, Simba na Yanga pale juu.
PRISONS:
Imerudi
Ligi Kuu baada ya kupotea kwa misimu mitatu na kutokana na jinsi ilivyosota
kurejea kwenye ligi hiyo, hapana shaka Prisons wamejipanga ili kutorudia
makosa.
Prisons
ilikuwa tishio miaka ya 1990 hadi mwanzoni mwa Milenia mpya, lakini taratibu
makali yake yalienda yakipungua na zaidi ilitokana na kila ilipozalisha
wachezaji wazuri, walikuwa wakichukuliwa na timu kubwa.
Hilo
lilikuwa shamba zuri sana la mavuno ya wachezaji kwa Simba na Yanga enzi hizo
na kama itarudi Ligi Kuu kwa mtazamo huo huo, dhahiri Prisons itarejesha hadhi
yake haraka iwezekanavyo.
Safari
hii Prisons inarudi Ligi Kuu ikiwa chini ya kocha mzoefu, Jumanne Challe,
kiungo wa zamani wa kimataifa Tanzania, ambaye msimu uliopita aliifundisha
African Lyon.
SIMBA SC:
Hawa
ni mabingwa watetezi wa ligi hiyo ambao wakati tunaingia kwenye msimu mpya
wanajivunia kuanza kama walivyouanza msimu uliopita, kwa ushindi wa Ngao ya
Jamii. Msimu uliopita mabao ya Haruna Moshi ‘Boban’ na Felix Sunzu yaliipa
Simba ushindi wa 2-0 dhidi ya Yanga katika mechi ya Ngao na msimu huu tena,
mabao ya Mghana Daniel Akuffo, Mganda Emanuel Okwi na mzalendo Mwinyi Kazimoto,
yaliitoa Simba nyuma kwa 2-0 na kushinda 3-2 dhidi ya Azam Jumanne wiki hii,
hivyo kutwaa Ngao.
Hakuna
shaka katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu, Simba SC ni miongoni mwa farasi
wanaotarajiwa kuwa na kasi nzuri kwenye marathoni ta taji. Ikiwa inaendelea kuwa
chini ya kocha wake Mserbia, Profesa Milovan Cirkovick, Simba iliyofanya
usajili baab kubwa, inatarajiwa kutetea taji pamoja na upinzani unaotarajiwa
kutoka kwa Yanga na Azam.
![]() |
| Simba SC |
YANGA SC:
Hawa
ni mabingwa wa kihistoria wa Ligi Kuu, wakiwa wanaongoza kutwaa mara nyingi
zaidi taji hilo, ambao msimu huu wanaonekana kabisa kujipanga vema, baada ya
majanga ya msimu uliopita, yaliyowafanya wakose hata tiketi ya kucheza michuano
ya Afrika.
Yanga,
inaingia katika msimu mpya kama ambavyo iliingia kwenye msimu uliopita, ikitoka
kutwaa ubingwa wa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, lakini tofauti tu
msimu huu hadi sasa hakuna dalili za mgogoro.
Ikumbukwe
msimu uliopita, Yanga ilipitia katika mgogoro mkubwa, ambao hasara zake ni
matokeo mabaya katika Ligi Kuu, ikiwemo kipigo kinachoingia kwenye historia cha
mabao 5-0 kutoka wapinzani wa jadi, Simba SC.
Lakini
baada ya kupata safu mpya ya uongozi chini ya Mwenyekiti msomi na tajiri,
Yussuf Manji, Yanga iliyoajiri pia kocha mpya, Mbelgiji, Tom Saintfiet ambaye
anaonekana ni mwajibikaji mzuri, msimu huu inatarajiwa kufanya vizuri katika
Ligi Kuu.
![]() |
| Yanga SC |
MABINGWA WA JUMLA LIGI KUU:
1965
: Sunderland (Dar es Salaam )
1966
: Sunderland (Dar es Salaam )
1967
: Cosmopolitans (Dar es Salaam )
1968
: Yanga
1969
: Yanga
1970
: Yanga
1971
: Yanga
1972
: Yanga
1973
: Simba
1974
: Yanga
1975
: Mseto SC
(Morogoro)
1976
: Simba
1977
: Simba
1978
: Simba
1979
: Simba
1980
: Simba
1981
: Yanga
1982
: Pan African
1983
: Yanga
1984
: Simba
1985
: Yanga
1986
: Tukuyu Stars (Mbeya)
1987
: Yanga
1988
: Coastal Union (Tanga)
![]() |
| Nahodha wa Yanga, Nsajigwa Shadrack akiwa na Kombe la ubingwa wa Ligi Kuu 2011 |
1989
: Yanga
1990
: Simba
1991
: Yanga
1992
: Yanga
1993
: Yanga
1994
: Simba
1995
: Simba
1996
: Yanga
1997
: Yanga
1998
: Yanga
1999
: Mtibwa Sugar (Morogoro)
2000
: Mtibwa Sugar (Morogoro)
2001
: Simba
2002
: Yanga
2003
: Simba
2004
: Simba
2005
: Yanga
2006
: Yanga
2007
: Simba (Ligi Ndogo)
2008
: Yanga
2009: Yanga
2010:
Simba SC
2011:
Yanga SC
2012:
Simba SC
2013:
???????














.png)
0 comments:
Post a Comment