• HABARI MPYA

    Saturday, September 15, 2012

    YANGA ITATOKA SALAMA KWA PRISONS, VIPI SIMBA KWA LYON NA AZAM KAITABA?

    Hamisi Kiiza ataiongoza Yanga dhidi ya Prisons leo Sokoine

    Na Mahmoud Zubeiry
    LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inaanza leo kwa timu zote 14 kujitupa kwenye viwanja saba tofauti, kuwania pointi za kuanza vema msimu mpya.
    Mabingwa watetezi Simba wataikaribisha African Lyon kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mjini Morogoro, Polisi Dodoma watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri wakati jijini Tanga, Mgambo JKT ambayo imepanda daraja msimu huu itaumana na Coastal Union kwenye Uwanja wa Mkwakwani.
    Tanzania Prisons ambayo nayo imerejea VPL msimu huu itaialika Yanga kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya. JKT Ruvu na Ruvu Shooting zitapambana kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam huku Azam ikiwatembelea Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Katiba.
    John Bocco 'Adebayor' ataiongoza
    Azam dhidi ya Kagera Kaitaba leo
    Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans dhidi ya Oljoro JKT. Mechi zote zitaanza saa 10.30 jioni.
    Wakati msimu huo unaanza leo, bado Simba, ambao ni mabingwa watetezi, Azam washindi wa pili na Yanga washindi wa tatu zinapewa nafasi kubwa ya kuendelea kutawala kwenye ligi hiyo- kwa kifupi Ligi Kuu itakuwa mbio za farasi watatu, wengine wanatarajiwa kuwa wasindikizaji.
    Kocha Mkuu wa Azam FC, Mserbia Boris Bunjak amesema timu yake ipo tayari kwa Ligi Kuu, lakini tu amehadharisha marefa wachezeshe kwa haki.
    Bunjak alikerwa mno na marefa waliochezesha mechi ya Ngao ya Jamii Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam juzi kwamba waliwabeba wapinzani wao Simba SC.
    Mechi hiyo ilichezeshwa na Martin Sanya, aliyeisaidiwa na Omar Kambangwa na Ephron Ndissa, wakati refa wa akiba alikuwa Oden Mbaga na Kamisaa Omary Kasinde.
    Bunjak alisema kwamba marefa hao walionyesha mapungufu makubwa kwa kuwapendelea wazi wazi Simba na hata wakafanikiwa kutoka nyuma kwa mabao 2-0 na kushinda 3-2.
    “Nafikiri tulicheza mechi nzuri, tukaongoza 2-0, baada ya hapo tukapoteza nafasi nzuri za kufunga, lakini siamini kwa nini refa alitoa penalti dakika ya mwisho(kipindi cha kwanza), kwa sababu ule mpira ulikuwa kwenye himaya ya wachezaji watatu kutoka nyuma, unaweza kuonaje nani aliucheza kwa mkono.
    Bao la pili, pia ulikuwa msaada mkubwa, niliandaa timu yangu kucheza dhidi ya wachezaji 10, siyo wachezaji zaidi, mimi si kocha nayeandaa timu kucheza dhidi ya wachezaji wengi, naweza kufanya nini, tulicheza vizuri, tulipoteza nafasi, refa alitunyima penalti mbili, asilimia 100, naweza kufanya nini, labda hii ni soka ya Tanzania tu.
    Mrisho Ngassa ataiongoza Simba dhidi ya African Lyon leo
    Nitafanya nini, huu ni uzoefu wangu wa kwanza ofisini tena, lakini nimeshangazwa sana, Simba ni timu kubwa, Simba ni timu nzuri, lakini leo Azam imecheza vizuri, Azam ilistahili kushinda taji,”alisema.
    Kocha huyo alionyeshwa kuridhishwa na bao moja tu la Simba, la tatu ambalo alisita kulizungumzia kabisa katika malalamiko yake.
    Nayo Simba, inayofundishwa na Mserbia Profesa Milovan Cirkovick, itashuka dimbani kumenyana na Lyon, ikiwa na kumbukumbu ya ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Azam FC na kutwaa Ngao ya Jamii, kwa mara ya pili mfululizo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam Jumanne wiki hii.
    Shujaa wa Simba siku hiyo alikuwa ni kiungo Mwinyi Kazimoto aliyefunga bao la ushindi dakika ya 78 kwa shuti kali la mbali baada ya kumchungulia kipa wa Azam, Deo Munishi ‘Dida’ amekaaje.
    Hadi mapumziko, Azam walikuwa mbele kwa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na John Raphael Bocco ‘Adebayor’ na kipre Herman Tchetche, wakimtungua kipa namba moja Tanzania, Juma Kaseja.
    Bocco alitangulia kufunga dakika ya tano ya mchezo huo, baada ya kupigiwa kona fupi na Abdi Kassim ‘Babbi’, akatoa pasi kwa Abdulhalim Humud ambaye alimrudishia mfungaji huyo akafumua shuti kali la chini likajaa nyavuni pembezoni mwa lango kulia.
    Bocco ambaye aliendekea kuwa mwiba mchungu kwa safu ya ulinzi ya Simba SC, alimtoka Amir Maftah upande wa kulia wa Uwanja na kuingia ndani kabla ya kutoa krosi fupi kwa Kipre aliyemtungua Kaseja na kuipatia Azam bao la pili dakika ya 35.
    Simba ilipata bao lake la kwanza dakika ya kwanza ya muda wa nyongeza, baada ya kutimu kwa dakika 45 za kipindi cha kwanza, mfungaji Daniel Akuffo kwa penalti, baada ya Said Mourad kuunawa mpira kwenye eneo la hatari.
    Kipindi cha pili Simba walirudi na nguvu zaidi na kuamua kushambulia kwa mipira ya pembeni, ikiwatumia Mrisho Ngassa na Emanuel Okwi ambao walikuwa wakibadilishana reli. 
    Kwa staili hiyo, haikushangaza Simba ilipotumia dakika 45 za mwisho kwa kufunga mabao mawili yaliyowatoa nyuma kwa 2-1 na kuibuka kidedea kwa ushindi wa 3-2.
    Emanuel Okwi alimchambua kama karanga Erasto Nyoni na kuingia ndani kabisa akiwatoka mabeki wengine wa Azam, kabla ya kuujaza mpira nyavuni kwa shuti kali na Kazimoto akamaliza kazi dakika ya 78.
    Kwa ujumla katika mchezo huo, Azam ilitawala kipindi cha kwanza na ilikosa mabao mawili zaidi ya wazi kupitia kwa Himid Mao na Kipre, lakini kipindi cha pili Simba walitawala mchezo na kama wangekuwa makini, nao wangeweza kuvuna mabao zaidi. 
    Kocha Mkuu wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintfiet amesema kwamba mechi dhidi ya Prisons itakuwa ngumu kwa sababu anaamini wapinzani wao watakamia na watasaidiwa na kucheza nyumbani.
    Lakini pia, Saintfiet alisema Prisons haina presha ya kufungwa na Yanga kwa sababu ni timu kubwa, hivyo watacheza kwa utulivu, wakipata sare ni safi, wakifungwa hakuna tatizo na wakishinda kwao itakuwa ‘sikukuu’.
    Mtakatifu Tom ametua Mbeya na wachezaji 22 kwa ajili ya mechi hiyo ambao ni makipa; Yaw Berko, Ally Mustafa ‘Barthez’, mabeki Shadrack Nsajigwa, Juma abdul, Godfrey Taita, Mbuyu Twite, Kevin Yondan,  Nadir Haroub ‘Cannavaro’, David Luhende, Oscar Joshua na Stefano Mwasyika, viungo ni Athumani Iddi ‘Chuji’, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Rashid Gumbo, Nizar khalfan, Shamte Ally na Simon Msuva na washambuliaji ni Jerry Tegete, Didier Kavumbangu, Said Bahanuzi na Hamisi Kiiza.
    Jumamosi iliyopita Yanga ilicheza mechi ya mwisho ya kujipima nguvu kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu na kushinda mabao 4-0 dhidi ya Moro united, Mrundi Didier Kavumbangu akifunga mawili, mengine beki Juma Abdul na kiungo Shamte Ally. 
    Saintfiet alitaka mechi moja dhidi ya timu inayocheza kama wapinzani wao wa kwanza katika Ligi Kuu, Prisons na pia katika Uwanja mbaya kama ambao atachezea mechi ya kwanza ya ligi hiyo, Sokoine mjini Mbeya na ndiyo maana timu hiyo ilicheza na Moro United Uwanja wa Shule ya Msingi Kijitonyama.
    Hiyo ilikuwa mechi ya 11, Saintfiet anashinda Yanga katika mechi 12 tangu ajiunge nayo miezi miwili iliyopita, mbali ya ziwe za mazoezini dhidi ya Sinza Stars na Kijitonyama Stars.
    Ndani ya mechi hizo kuna mechi sita za Klabu Bingwa ya soka Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, ambalo aliiwezesha Yanga kutwaa ubingwa wa tano wa michuano hiyo, ikipoteza mechi moja tu ya kwanza dhidi ya Atletico ya Burundi, kwa kufungwa 2-0, mabao yote ya Kavumbangu, ambaye baadaye ikamsajili.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA ITATOKA SALAMA KWA PRISONS, VIPI SIMBA KWA LYON NA AZAM KAITABA? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top