• HABARI MPYA

    Saturday, August 17, 2013

    YANGA SC YAICHAPA AZAM 1-0 NA KUBEBA NGAO

    Na Mahmoud Zubeiry, IMEWEKWA AGOSTI 17, 2013 SAA 12:00 JIONI
    BAO pekee la kiungo Salum Abdul Telela jioni hii Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam limeipa Yanga SC ushindi wa 1-0 dhidi ya Azam FC na kutwaa Ngao ya Jamii.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Oden Mbaga, aliyesaidiwa na Hamisi Chang’walu na Omar Kambangwa wote wa Dar es Salaam, hadi mapumziko Yanga SC walikuwa mbele kwa bao 1-0.
    Yanga ilipata bao hilo mapema tu dakika ya pili, mfungaji kiungo Salum Abdula Telela aliyeunganisha pasi ya Didier Kavumbangu.
    John Bocco wa Azam akienda chini baada ya kuchezewa rafu na Nadir Haroub 'Cannavaro' wa Yanga kushoto. Mwingine kulia ni Haruna Niyonzima.

    Baada ya bao hilo, Yanga iliongeza kasi ya mashambulizi langoni mwa Azam na kipa Aishi Manula alifanya kazi ya ziada kuokoa.
    Dakika ya 11, Yanga ilipata pigo baada ya beki wake Kevin Yondan kuumia kufuatia kugongana na mshambuliaji wa Azam FC, John Bocco ‘Aedebayor’. Yondan alitibiwa kwa dakika nne, lakini akashindwa kurejea uwanjani na nafasi yake ikachukuliwa na Mbuyu Twite dakika ya 15.
    Dakika tano baadaye Yanga ikapata pigo lingine baada ya kipa wake, Ally Mustafa ‘Barthez’ kuumia kufuatia kugongana na Kipre Tchetche.
    Barthez ‘alijitoa muhanga’ kuutokea mpira miguuni mwa mshambuliaji huyo wa Ivory Coast baada ya kuwatoka mabeki wake, Juma Abdul na Nadir Haroub ‘Cannavaro’- hivyo kugongwa kifuani na mguu wa Kipre.
    Salum Telela kushoto akikimbia na Jerry Tegete baada ya kufunga. Mwingine kushoto ni Haruna Niyonzima 

    Barthez alitibiwa kwa dakika nne kabla ya kumpisha Deo Munishi ‘Dida’.  Azam waliongeza kasi ya mashambulizi langoni mwa Yanga na dakika ya 30 Kipre Tchetche alifumua shuti kali likagonga mwamba na kutoka nje akiwa ndani ya 18 baada ya kupokea pasi ya Bocco.   
    Aishi Manula alikuwa majaribuni tena dakika ya 30 baada ya krosi maridadi ya Simon Msuva kumponyoka kabla ya kuondoshwa hatarini na Erasto Nyoni.
    Dakika ya 38 Dida alidaka shuti kali la mfungaji bora wa Ligi Kuu msimu uliopita Kipre Tchetche kutoka umbali wa mita 17 na kupigiwa makofi na mashabiki.
    Kipindi cha pili, Yanga SC waliendelea kucheza vizuri na kukosa mabao zaidi, huku sifa zaidi akistahili kipa chipukizi Aishi Manula.
    Dakika ya 67 Telela alikarbia kufunga tena baada ya kuunganishia nje krosi nzuri ya Haruna Niyonzima.
    Dakika ya 81 Niyonzima alikaribia kufunga mwenyewe kwa mpira wa adhabu, lakini shuti lake liligonga mwamba wa juu na kudondokea chini kabla ya beki Aggrey Morris kuondosha katika hatari.  
    Kikosi cha Yanga SC leo kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’/Deo Munishi ‘Dida’ dk15, Juma Abdul, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan/Mbuyu Twite dk15, Athumani Iddi ‘Chuji’, Simon Msuva, Salum Telela, Jerry Tegete/Hussein Javu68, Didier Kavumbangu na Haruna Niyonzima.
    Azam FC; Aishi Manula, Erasto Nyoni/Joackins Atudo dk46, Waziri Salum, David Mwantika, Aggrey Morris, Himid Mao, Kipre Tchetche, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, John Bocco ‘Adebayor’/Gaudence Mwaikimba dk74, Kipre Balou/Ibrahim Mwaipopo dk62 na Khamis Mcha.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: YANGA SC YAICHAPA AZAM 1-0 NA KUBEBA NGAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top