• HABARI MPYA

    Thursday, May 17, 2012

    MANJI AWAPIGIE NGOMA GANI YANGA WAMUELEWE?


    Manji

    YUSSUF Mehboob Manji, ameibuka tena Yanga, baada ya kimya cha muda mrefu akijitokeza kwa nia ya kuokoa jahazi kutokana hali mbaya ya kiuchumi inayoikabili klabu kwa sasa.
    Waajiriwa wa Yanga, wakiwemo makocha, wachezaji na watendaji hawajalipwa mishahara kwa takriban miezi minne, hali inayoashiria uongozi wa klabu hiyo, chini ya Mwenyekiti wake, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga umeelemewa.
    Lakini mfanyabiashara kijana anayemiliki mamilioni ya fedha, Manji yu tayari kuokoa jahazi kwa kurejesha udhamini katika klabu.
    Hata hivyo, ili kurejea kuidhamini Yanga, Manji ametoa masharti matano.
    Masharti hayo ni; kufanyika uhakiki wa mahesabu ya akaunti za Yanga ndani ya siku 90 na wakaguzi wa hesabu wa kujitegemea kukagua hesabu za kipindi cha kuanzia mwaka 2006 hadi 2012 kwa ajili ya fedha zilizoingia klabuni.
    Sharti la pili ni kuchapishwa magazetini kwa akaunti za Yanga siku 15 baada ya kumalizika kwa robo ya mwaka, tatu ni
    kuendeshwa zoezi la kura ya maoni ndani ya siku  60 na kuamua kama wanachama wa Yanga wanataka klabu iwe Yanga au la na sharti la nne ni mabadiliko ya Katiba ndani ya siku 90.
    Kwa mujibu wa barua ya Manji kwa Mwenyekiti wa Yanga, Nchunga ambayo BIN ZUBEIRY imeipata nakala yake, ameutaka pia uongozi kuidhinisha mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa klabu, nafasi ambayo iko wazi baada ya Davis Mosha kujiuzulu mwaka jana.
    Sharti la mwisho la Manji ni kutaka kufanyika kwa Mkutano Mkuu wa wanachama ndani ya siku 30, ili kujadili mustakabali wa klabu.
    Hii ni mara ya pili kwa Manji tangu ajitoe Yanga, kuibuka na kutoa masharti ili arejeshe ufadhili wake, Yanga awali mwaka jana uongozi wa Yanga, chini ya Mwenyekiti wake, Nchunga ulimkatalia.
    Ikumbukwe Februari mwaka jana, Kamati ya Utendaji ya klabu ya Yanga iliona ni ngumu kutekeleza masharti manne ya Manji na kuridhia uamuzi wake wa kujitoa kwenye klabu hiyo kama Mfadhili na Mjumbe wa Baraza la Wadhamini la Klabu.
    Chini ya Mwenyekiti Wakili Lloyd Baharagu Nchunga na aliyekuwa Makamu wake, Davis David Mosha- historia iliandikwa, Manji alijitoa Yanga na kubaki kutekeleza mkataba wake na klabu hiyo tu wa kuendesha vyombo vya habari vya klabu, kupitia kampuni yake ya Quality Media Group.
    Wengi miongoni mwa wana Yanga hapana shaka watakuwa wanakumbuka kwamba, Manji alifikia uamuzi wa kujitoa Yanga, baada ya kuona sharti lake la kutaka ukaguzi wa hesabu ufanyike kwenye klabu hiyo, lakini ikawa inapigwa chenga na wakati huo huo wanatokea watu wa kumchafua kutokana na kutoa sharti hilo.
    Kimsingi hadi sasa haieleweki Yanga yenye viongozi waliokwenda shule, tena wa zama za leo za sayansi na teknolojia, kwa nini wanakwepa zoezi la ukaguzi wa hesabu za kilichoingia na kilichotumika klabuni.
    Awali, baada ya Manji kujitoa, Mwenyekiti wa klabu hiyo, Nchunga alimfuata kumuomba abadilishe uamuzi wake na aendelee kuifadhili Yanga, lakini naye akawapa masharti manne, mepesi na yenye lengo la kuisaidia klabu hiyo.
    Nitakumbusha masharti hayo; Manji alitaka ukaguzi wa hesabu za klabu hiyo ufanyike haraka na itolewe ripoti itakayoonyesha mapato na matumizi ya fedha zote za klabu hiyo ambazo zimeingia kupitia vyanzo mbalimbali.
    Pili, mdhamini huyo ameitaka Kamati ya Utendaji ya Yanga kuhakikisha wachezaji wa klabu hiyo wanalipwa fedha zao kama ilivyokubaliwa katika mikataba yao.
    Sharti la tatu ni uongozi wa Yanga kutomuingilia aliyekuwa kocha wa klabu hiyo, Sam Timbe katika benchi lake la ufundi na sharti la nne ni kuifanya klabu ijitegemee.
    Kufuatia masharti hayo, Kamati ya Utendaji ya Yanga ilikutana na kuridhia Manji aondoke- maana yake nini, masharti yake manne hayatekelezeki. Hakuna tafsiri nyingine ya uamuzi huo, zaidi ya hiyo kwa sababu Manji alikuwa wazi na kadiri walivyoweza viongozi wa klabu hiyo wamekuwa wazi pia.
    Ni hawa viongozi walioingia madarakani katika uchaguzi uliotawaliwa na mizengwe- tena uchaguzi uliokosa sifa za kuitwa huru na wa haki, walifikia maamuzi mazito kama hayo.
    Kwa wenye kuifahamu vema Yanga, watakuwa wanakumbuka namna klabu hiyo ilivyopitia kwenye wakati mgumu kiuchumi muongo uliopita kiasi cha kushuka kwa kiwango kikubwa kisoka.
    Yanga ilitamba kwenye soka ya Tanzania na Afrika kuanzia miaka ya 1960 mwishoni hadi 1970 kabla ya mgogoro wa kihistoria mwaka 1976 ambao ulikuwa chanzo cha kuzaliwa kwa Pan African na tangu hapo ilisota hadi mwaka 1981 ilipokuwa imara tena.
    Miaka yote ya 1980 kiwango cha Yanga hakikuyumba sana na hali ikawa nzuri zaidi miaka ya 1990 baada ya kujitokeza kwa wafadhili wa Kiasia, wakiongozwa na aliyekuwa Mbunge wa Kilombero, Morogoro, Abbas Gulamali (sasa marehemu) na wengine kama Murtaza Dewji aliyetokea Pan African.
    Huwezi kuacha kumtaja mtu kama Mohamed Virani ‘Babu’ aliyekuwa akiisaidia klabu hiyo tangu miaka ya 1980- enzi hizo Yanga ikimtangazia bidhaa zake kama sabuni za Bobby Soap na soda za Vimto kwa kuvaa jezi zenye nembo ya bidhaa hizo.
    Uchaguzi uliofanyika mwaka 1993 katika Uwanja wa Ndani wa Taifa, uliwaingiza madarakani Dk Jabir Katundu kama Mwenyekiti na George Mpondela ‘Castro’ kama Katibu Mkuu na hawa walijaribu kwa mara ya kwanza kutaka kuifanya Yanga ijitegemee.
    Mfanyabiashara Reginald Mengi alikuwa tayari kuisaidia Yanga kutekeleza azma ya klabu kuwa kampuni, lakini zikatokea hujuma tu za watu wenye kupenda kuona klabu hiyo inabakia kuwa kama ilivyo, ili waendelee kutimiza mambo yao.
    Zoezi hilo lilikwama na ukatokea mgogoro mkubwa tena Yanga, hata viongozi wakaondoka madarakani kabla ya kumaliza muda wao- wafadhili nao wakaingia mitini wote.
    Hadi Rashid Ngozoma Matunda (sasa marehemu) anachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa klabu mwaka 1996, Makamu wake, Mohamed Namanganya (sasa marehemu), Katibu Mkuu wake Frank Mutani, Yanga ilikuwa iko vibaya kiuchumi.
    Uongozi huu ulipata misukosuko mingi, kwanza kashfa za ubadhirifu za viongozi wenyewe kwa wenyewe zilizomfanya Mutani akaachia ngazi- baadaye hali ngumu ndani ya timu hadi wanachama wakakasirika na kuanza kuutia misukosuko uongozi huo- walikuwa wakiupindua kila siku na kuweka Kamati za Muda.
    Nakumbuka Salim Ngereza, Tarimba Abbas- kwa wakati tofauti hawa walikuwa Wenyeviti wa Kamati za Muda Yanga, katika kipindi cha mwaka 1998 hadi 2000, wakati huo bado uongozi unaotambulika Kikatiba ni wa Matunda.
    Hatimaye mwaka 2000 akina Tarimba wakafanikiwa kumtoa Matunda na kuifanya klabu kuwa kampuni, ingawa ilikuwa kampuni jina. Lakini kundi la wana Yanga wengine likiongozwa na Yussuf Mzimba liliingia msituni na kuanzisha kitu kinaitwa Yanga Asili, likiipinga Yanga Kampuni.
    Mgogoro uliendelea na hali ikazidi kuwa mbaya, hatimaye mwaka 2003 Tarimba akaondoka kwenye klabu hiyo, Mbaraka Igangula akakaimu na baadaye ukafanyika uchaguzi wa Yanga Kampuni, Francis Kifukwe akawa rais wa klabu.
    Wakati wote huo hali ilikuwa ni ngumu Yanga, klabu haina mfadhili- baada ya kupitia kwenye mikono ya udhamini wa Mobitel (sasa Tigo) na Shivacom kwa muda mfupi, fedha za mkononi za viongozi zikiihudumia timu.
    Hiki ndicho kipindi ambacho Yanga ilikuwa inaacha madeni kwenye hoteli mikoani ilipokwenda kucheza mechi zake za Ligi na kufika mwaka 2006 hali ilikuwa ngumu zaidi, hadi kikajitokeza kikundi cha wana Yanga kisichofungamana na upande wowote kuamua kuchangisha fedha za kuisaidia timu ikiwa kwenye mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame, mjini Dar es Salaam.
    Mkutano ulifanyika kwenye ukumbi wa Reli Gerezani Club na kuanzisha harambee ya Saidia Yanga.  Hapo ndipo walipojitokeza watu kutoa namba za matajiri maarufu nchini wanaowafahamu fika ni wapenzi au wanachama wa Yanga na katika staili hiyo alipatikana Manji.
    Manji alijitolea kwa moyo mmoja kuisaidia klabu hiyo na akasema pia angependa umoja ndani ya klabu, akaingia gharama kubwa kusuluhisha mgogoro wa Yanga Asili na Yanga Kampuni na hatimaye mwafaka ukapatikana na ukasainiwa na pande zote mbili, kwa makubaliano maalum.
    Mei mwaka 2007 ukafanyika uchaguzi wa kwanza halali Yanga, tangu ule wa mwaka 1996 uliomuweka madarakani marehemu Matunda na timu yake. Katika uchaguzi huo wa 2007, Wakili Imani Omar Madega akashinda Uenyekiti, Ngozoma Matunda makamu wake, Katibu Mkuu Lucas Kisasa.
    Kwa kuwa yaliyofikiwa kwenye mwafaka hayakutekelezwa, ikiwemo timu kukabidhiwa kwa kampuni na akina Madega wakabaki kuwa viongozi wa klabu, hali haikuwa shwari moja kwa moja Yanga, mivutano iliendelea, Manji akisisitiza klabu kujitegemea kwa kuwa na kampuni ya kuuza hisa, tena akitoa michanganuo ya kitaalamu, inayoainisha jinsi ambayo klabu hiyo itanufaika.
    Manji ameingiza fedha nyingi Yanga tangu mwaka 2006, nyingine zilikuwa ni za matumizi yasiyokuwa na maana, kama kusaidia matawi sijui- labda kwa lengo la kuwafurahisha wanachama, lakini hazikuisaidia klabu.
    Umefika wakati anataka kuona fedha zake zinaisaidia Yanga moja kwa moja na kutaka kuiwezesha klabu ijitegemee, lakini watu wanaleta vikwazo kiasi cha kufikia uamuzi wa kusema; Acha aende.
    Nimeeleza namna Manji alivyopatikana Yanga, haikuwa kazi rahisi na klabu ilipitia msoto wa muda mrefu, sijui wakati huo akina Nchunga na Mosha walikuwa wapi- walikuwa hawajui klabu ilivyokuwa inataabika? Na mbona hawakujitokeza wakati huo?
    Mwana Yanga wa kweli, daima lazima ataweka mbele maslahi ya klabu yake na kama hilo lingezingatiwa, Manji asingeondoka Yanga.
    Suala si Manji, bali ni mustakabali wa klabu baada ya Manji, kwani Yanga ya leo si ile ya miaka 10 iliyopita, mambo yamebadilika mno, ikiwemo bajeti ya uendeshwaji wake, kuanzia mishahara ya wachezaji na makocha.
    Tunaona sasa katika kipindi ambacho Manji amekuwa nje Yanga, hali imekuwa ngumu, wachezaji wanalia njaa, usajili wa kisanii ulishaanza, mchezaji anasaini makaratasi bila kupewa fedha sasa.
    Inafikia wachezaji wanagoma kwa sababu ya kucheleweshewa mishahara na pia wanalalamikia maji hayapandi juu klabuni.
    Hii ni safari ya klabu kurudi kule kule ilipotokea kwenye kutembeza mabakuli jukwaani kuchangisha fedha za kuhudumia timu, lakini ‘Mungu saidia’, Manji karudisha moyo wake nyuma na kutaka masharti yake yatekelezwe naye arejeshe udhamini wake klabuni.
    Mimi nastaajabu kitu kimoja, Yanga ni taasisi kubwa ambayo ipo kwa mujibu wa sheria- serikali inaitambua Yanga kama si mali ya mtu ni ya wananchi. Hofu ya Yanga kugeuzwa Kampuni inatoka wapi?
    England pale timu zote kubwa sasa zinaendeshwa na wageni, lakini bado wapenzi na mashabiki wake ni wale wale, zaidi wamenufaika kwa kufanyiwa klabu zao ziwe bora zaidi na zenye hadhi ya mwonekano na mafanikio.
    Miaka mitano iliyopita nani alikuwa shabiki wa Manchester City nje ya Manchester tu pale? Mimi sielewi hofu inatoka wapi na hasa linapokuja suala la ukaguzi wa hesabu watu wanapiga chenga, hii inaashiria nini?
    Kwa nini sasa Nchunga asikubaliane na masharti ya Manji- kwani ni mepesi tu na kimsingi suala la kujazwa kwa nafasi ya Mosha au mabadiliko ya Katiba ni muhimu, ili kupata Katiba bora zaidi kwa manufaa ya klabu, mbona ni masuala yanayowezekana?
    Au Nchunga anahisi nini nyuma ya masharti haya- na kama kuna hatari yoyote basi awaeleze wana Yanga wajue, lakini kinyume chake ataonekana yeye ndiye tatizo.
    Mimi sioni tatizo katika masharti ya Manji na yeyote mwenye mlengo wa maendeleo na kutaka kuiona Yanga ya kisasa- sidhani kama anaweza kutofautiana nami. Alamsiki.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MANJI AWAPIGIE NGOMA GANI YANGA WAMUELEWE? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top