• HABARI MPYA

    Wednesday, May 09, 2012

    VITUO VYA LIGI YA TAIFA VYATAJWA


    KAMATI ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imepanga vituo vitatu vya Ligi ya Taifa inayoshirikisha mabingwa wa mikoa kwa ajili ya ligi hiyo itakayoanza Mei 26 mwaka huu.
    Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniphace Wambura Mgoyo ameiambia BIN ZUBEIRY mchana huu kwamba Kundi A lenye mabingwa wa mikoa ya Iringa (Kurugenzi Mufindi), Lindi (Lindi SC), Mbeya (Tenende FC), Morogoro (Mkamba Rangers), Mtwara (Ndanda SC), Pwani (Super Star), Rukwa (Mpanda Stars) na Ruvuma (Mighty Elephant) zitacheza mechi zake mjini Mtwara.
    Amesema Mji wa Kigoma utakuwa mwenyeji wa mabingwa wa mikoa ya Dodoma (CDA), Kagera (Bandari FC), Kigoma (JKT Kanembwa), Mwanza (Pamba SC), Shinyanga (Mwadui SC), Singida (Aston Villa) na Tabora (Majimaji).
    Amesema Kundi C lenye mabingwa wa mikoa ya Arusha (Flamingo SC), Dar es Salaam (Ashanti United ya Ilala, Red Coast ya Kinondoni na Tessema FC ya Temeke), Kilimanjaro (Forest FC), Manyara (Nangwa VTC), Mara (Polisi Mara) na Tanga (Korogwe United) watachezea mechi zao mkoani Mara.
    Amesema mwisho wa kuwasilisha fomu za usajili ni Mei 15 mwaka huu wakati kipindi cha pingamizi ni kuanzia Mei 16 hadi 22 mwaka huu. Mei 23 mwaka huu Kamati ya Mashindano ya TFF itakutana kupitia usajili huo. Wachezaji wanaosajiliwa ni wale wale waliochezea timu hizo katika ligi ya mkoa.
    Amesema Mei 14 mwaka huu ni mwisho kwa mikoa yenye pingamizi kwa mabingwa wao kuwa wameshashughulikia rufani husika. Kamati ya Mashindano imeagiza kuwa kwa mikoa itakayoshindwa kufanya hivyo mpaka baada ya tarehe hiyo mabingwa wao hawatashiriki ligi hiyo.
    Amesema timu tano zitapanda daraja kucheza Ligi Daraja la Kwanza msimu ujao. Mshindi wa kwanza kutoka kila kundi na washindwa wawili bora (best losers) kutoka kundi A na C ambayo yana timu nane kila moja.
    Wakati huo huo: Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limemteua Leslie Liunda wa Tanzania kuwa Kamishna wa mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia 2014 Kanda ya Afrika kati ya Lesotho na Sudan itakayochezwa jijini Maseru.
    Wambura amesema mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya pili itachezwa kati ya Juni 1 na 3 mwaka huu. Lesotho na Sudan ziko kundi D pamoja na Ghana na Zambia.
    Naye Hafidhi Ally ameteuliwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kuwa Kamishna wa mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Dynamos FC ya Zimbabwe na Esperance Sportive ya Tunisia.
    Mechi hiyo ya marudiano hatua ya 16 bora itachezwa Mei 13 mwaka huu kwenye Uwanja wa Rufaro jijini Harare. Esperance Sportive ilishinda mechi ya kwanza kwa mabao 6-0.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: VITUO VYA LIGI YA TAIFA VYATAJWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top