• HABARI MPYA

    Sunday, July 01, 2012

    YANGA WANA KAZI KUBWA KABLA YA KUWA NA TIMU NZURI


    Na Mahmoud Zubeiry

    NI katika makala yangu iliyopita, nilipowaambia Yanga, kwamba kusajili wachezaji wazuri siyo kuwa na timu nzuri na ni jana tu lilipodhihirika hilo, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati timu hiyo ilipokuwa ikimenyana na Express ya Uganda katika mchezo wa kirafiki.
    Pamoja na Yanga kushinda mabao 2-1, lakini mapungufu makubwa yalionekana- kubwa timu haichezi kwa muundo (formation) wenye kueleweka, haina mipango kabisa, ingawa kweli wachezaji walikuwa wakionana uwanjani.
    Kuna mambo mawili ambayo yanawatatiza mashabiki wengi wa soka nchini- kwanza kucheza kwa uelewano na pili wachezaji kuonana uwanjani.
    Kucheza kwa uelewano kunatokana na muundo, ambao unatokana na mafundisho ya mwalimu- lakini wachezaji kuonana uwanjani na kupeana pasi ni jambo ambalo linaweza kufanywa na timu yoyote, hata isiyo na mwalimu ili mradi tu wanajijua wanacheza dhidi ya wapinzani.
    Siyo kila kugongena pasi, basi ni timu kucheza kwa uelewano- hapana na kwa sasa hicho ndio kitu ambacho Yanga inakosa. Yanga wamegonga pasi jana, lakini zilikuwa za kupoteza muda tu kwa sababu hazikuwa na dhamira yoyote iliyoonekana.
    Lakini wachezaji bado hawana pumzi na stamina ya kutosha- ndiyo maana walitawala mchezo kwa dakika 45 tu za kwanza, lakini kipindi cha pili mambo yalikuwa magumu upande wao.
    Muundo; Yanga lazima wawe na namna yao ya kucheza katika mpangilio, wakijua wanaanzaje katika kuelekea eneo la wapinzani hadi kupata bao.
    Yanga lazima wawe na uelewa na mbinu za kukaa na mpira kwa muda mrefu mchezoni bila kupoteza, ili kupunguza makali ya wapinzani.
    Yanga lazima wawe na mipango ya kuwahadaa wapinzani wa aina yoyote, iwe wenye kushambulia au kupaki basi.
    Yanga lazima wawe na mipango ya kutengeneza nafasi, lazima wawe na mipango ya kutumia hizo nafasi wanazopata pia. Haiwezekani timu inapiga kona nane, bila bao hata moja.
    Haiwezekani Yanga wanapiga mipira ya adhabu zaidi ya mitano nje ye eneo la mita 18, bila ya kulenga lango.
    Niwapongeze kwa mabao mawili waliyopata jana yalitokana na mipira ya pembeni na katika soka ya dunia ya leo, mbali na mipira ya adhabu mabao mengi hutokana na mipira ya pembeni.
    Lakini haikutokana na mipango zaidi ya uwezo binafasi wa wachezaji wake bora iliyowasajili tena wote waliocheza jana walikuwa wazawa- faraja iliyoje na unaweza kuiona timu bora ya taifa ya baadaye ikiundwa na wachezaji wa Yanga.
    Ni kweli, Yanga inasifiwa kufanya usajili mzuri kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, miongoni mwa wachezaji iliyowasajili wakiwemo Kelvin Yondan, Ally Mustafa ‘Barthez’ kutoka Simba na Frank Damayo kutoka JKT Ruvu.
    Kulingana na hali halisi ya uwezo wa wachezaji hao kwa sasa, hususan Yondan, wenyewe wanamuita Vidic na Damayo, mashabiki wa Yanga wamesuuzika mno na nafsi zao. Wanaamini wachezaji hao na wengineo, wataifanya timu yao iwe tishio msimu ujao.
    Jerry Tegete anampiga tobo kipa wa Express, Didi Mahmoud kufunga bao la kwanza jana
    Yanga sasa wana ndoto nyingi sana juu ya timu na japokuwa mwakani hawatashiriki michuano ya Afrika, lakini wanaona kabisa wamekwishatetea Kombe la Kagame, Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati.
    Yanga tayari wa ndoto za kulipa zile 5-0 walizopigwa na watani wao wa jadi, Simba msimu huu. Wanaota kurejesha ubingwa wao wa Ligi Kuu na kwa ujumla heshima yao katika soka ya Tanzania, waliyoipoteza msimu uliopita.
    Kwa ujumla wana matumaini makubwa sana, hasa wakizingatia Mwenyekiti wao atakuwa Yussuf Manji, Makamu wao Mwenyekiti Clement Sanga na Wajumbe kama Abdallah Bin Kleb, Peter Haule na wengineo- wana Yanga, wana matumaini makubwa sana na kikosi chao kipya.
    Lakini pamoja na ukweli huo, bado nasistiza Yanga wanatakiwa kutambua kwamba; Kusajili wachezaji wazuri ni suala moja na kuwa na timu nzuri ni suala lingine.
    Yanga wamefanikiwa mtihani wa kusajili wachezaji wazuri, na sasa wanatakiwa wapitie katika zoezi gumu zaidi la kutengeneza timu nzuri ya ushindani kwa mashindano ya ndani na nje.
    Bahati nzuri, Yanga wana muda wa kutosha kwa sababu msimu wote ujao utakuwa wa kutengeneza tu timu yao kwa kuwa hawashiriki michuano ya Afrika- hivyo kama watafanikiwa kufuzu na mtihani huo pia, tegemea kabisa Yanga ya 2014 itakuwa tishio hadi Afrika.
    Lakini hiyo timu nzuri inatengenezwaje? Kwanza kuwa na mwalimu bora, atakayepeta fursa na wasaa mzuri na wa kutosha wa kuwaandaa wachezaji. Haitoshi tu kusajili wachezaji wazuri na kisha unawakabidhi kwa msimamizi wa mazoezi, ni hatari kwa vipaji vyao.
    Yanga wanatakiwa kutengeneza sera nzuri za benchi la ufundi, ambalo litakuwa na nguvu na kuheshimiwa na wachezaji, tofauti na ilivyo hivi sasa, mchezaji anamuheshimu Seif Magari, anamdharau Freddy Felix Minziro.
    Yanga inatakiwa kuwa wazi kwa wachezaji wake, kuwaambia imewasajili kwa ajili ya kufanya kazi na wasilewe sifa na kuanza kupandisha mabega juu, uwanjani hawajitumi, matokeo yake wanarudi kule kule, kwenye kununua mechi.
    Haiwezekani, usajili huu wa Yanga naomba niseme mapema ulikuwa makini mno, tofauti na usajili wa miaka miwili, mitatu iliyopita na timu iliyopewa jukumu hilo, ililifanikisha kwa umakini wa hali ya juu.
    Kwa sababu hiyo basi, wachezaji lazima wacheze soka uwanjani, watengeneze matokeo mazuri kwa uwezo wao. Wadumishe viwango vyao, ili waendelee kuwapo timu ya taifa. Lakini kubwa na la msingi ni mashabiki wa Yanga kuwa na subira kabla ya kupata timu nzuri.
    Yanga watawaona wachezaji wao wazuri katika Kombe la Kagame na watafanya sana vitu adimu binafsi na ikibidi, kweli watatetea hadi Kombe lao- lakini kuwa na timu nzuri kwa maana ya timu inayocheza soka ya kuelewana, iliyotokana na mafundisho, wana Yanga wanatakiwa kuwa na subira.
    Vema imekwishaelezwa kocha kutoka Ubelgiji wamekwishafikia naye makubaliano na atatua wakati wowote nchini kuanza kazi.
    Kama atakuwa mwalimu mzuri, naamini wakimpa fursa na wasaa mzuri na wa kutosha, kuanzia mzunguko wa pili Yanga itakuwa inacheza ‘kitenisi’ cha kutisha- ila kama ubabaishaji utaendelea na hakutakuwa na sera nzuri za benchi la ufundi, mafunzo, nidhamu na kujali maslahi ya wachezaji, basi wachezaji hawa Desemba tu wataonekana hawafai.
    Simon Msuva kulia
    Nataka nimalizie kwa kuwaambia Yanga, wapeleke timu ya kambini, waepuke mechi za kirafiki zilizo nje ya program ya walimu, watumie vizuri wiki mbili hizi zilizobaki kabla ya kuanza kwa Kombe la Kagame. Alamsiki!
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WANA KAZI KUBWA KABLA YA KUWA NA TIMU NZURI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top