• HABARI MPYA

    Tuesday, August 07, 2012

    MBUNGE AMUOMBA MANJI 6-0 DHIDI YA MNYAMA

    Mh Mgimwa

    Na Mahmoud Zubeiry, Dodoma
    MBUNGE wa Jimbo la Mufindi Kaskazini, Mahmoud Mgimwa amemtaka Mwenyekiti wa Yanga, Yussuf Manji kufanya lolote analoweza, lakini ahakikishe Simba SC inafungwa 6-0 ili kuwanyamazisha wapinzani wao hao wa jadi, wanaotambia ushindi wa 5-0 katika msimu uliopita wa Ligi Kuu.
    Mgimwa alitoa ombi hilo, wakati akitoa maoni yake kwa uongozi wa klabu hiyo jana katika ukumbi mdogo wa Bunge mjini Dodoma, wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa Tawi la Yanga Bungeni.
    “Kwa kweli mimi kilio changu ni kimoja tu, Yanga sasa hivi hatuna raha, zile 5-0 tulizofungwa hata tufanye nini, zinatuumiza, mimi nakuomba Mwenyekiti, fanya unavyoweza na jeshi lako, kuhakikisha tunawafunga 6-0 wale ili tuheshimiane,”alisema.
    Mbali na kufungwa 5-0 msimu uliopita, Yanga pia iliwahi kufungwa 6-0 na Simba mwaka 1977.
    Jana Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, ambao ni wapenzi wa Yanga waliafiki kuchangia Sh. 500,000 kila mwaka katika kuchangia maendeleo ya klabu hiyo, katika hafla fupi ya uzinduzi wa Tawi la Yanga Bungeni.
    Hiyo ilifuatia ombi la Mjumbe wa Baraza la Wadhamini la klabu ya Yanga, Mama Fatuma Karume, mke wa rais wa kwanza wa Zanzibar, Hayati Abeid Amaan Karume leo wakati akizindua tawi la Yanga Bungeni.
    Mama Karume alizindua mfuko huo kwanza yeye mwenyewe kutoa Sh. 500, 000 ambazo zilipokewa na Mweka Hazina wa Tawi la Yanga Bungeni, Martha Moses Mlala, Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Singida.
    Wabunge wengine waliotoa fedha zao hapo hapo ni Abbas Mtemvu (Temeke, CCM). Athumani Mfutakamba (Igalula, CCM) na Grace Kiwelu (Viti Maalum, CHADEMA).
    Awali, akisoma taarifa ya tawi hilo, Mwenyekiti Misanga ambaye amewahi kuwa Katibu Mkuu wa Yanga miaka ya 1970, chini ya Mwenyekiti Juma Shamte, alisema kwamba Julai 31 walifanya uchaguzi wa viongozi wa tawi la klabu hiyo Bungeni na mbali ya yeye kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti, Abadallah Ameir alichaguliwa kuwa Makamu wake.
    Alisema Nafasi ya Katibu Mkuu, ilikwenda kwa Godfrey Zambi, Katibu Msaidizi, Grace Kiwelu, Mweka Hazina Martha Mlala na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Abbas Mtemvu, Halima Mdee, Victor Mwambalaswa, Mohammed Chambo, Abdul Marombwa, Vicky Kamatta na Ritta Kabati.
    Aidha, alisema waliteua pia Kamati ya Ushauri ya Wajumbe wanne, ambao ni George Mkuchika, Zarina Madabida, Faki Makame na Chirtopher Chiza. 
    Pamoja na hayo, Misanga aliupongeza uongozi mpya wa Yanga chini ya Mwenyekiti wake Manji, na kuutaka uwe makini na wanachama wapandikiza sumu za migogoro klabuni.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBUNGE AMUOMBA MANJI 6-0 DHIDI YA MNYAMA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top