IMEWEKWA JUNI 7, 2013 SAA 7:00 USIKU
MSHAMBULIAJI wa Brazil, Hulk amethibitisha Jose Mourinho anamtaka Stamford Bridge na ametoa ofa ya Pauni Milioni 35 kumng'oa Zenit St Petersburg.
Zenit kwa sasa imeichunia ofa ya Chelsea na wanataka kiasi cha karibu Pauni Milioni 50 walizolipa kwa Porto kumpata mshambuliaji huyo mwenye kasi msimu uliopita.
Hulk anataka kuondoka Urusi na anahusishwa na kuungana na Mourinho na aliweka wazi hilo mbele ya Waandishi wa Habari kwamba anajua Chelsea wametoa ofa kwa ajili yake.
Anayetakiwa: Hulk (kulia) anatakiwa na kocha mpya wa Chelsea, Jose Mourinho
Alipoulizwa kuhusu hilo na Waandishi nchini Brazil jana mchana, alijibu: "Ikiwa nitasema hakukuwa na kitu juu ya hili, nitakuwa nadanganya. Lakini hiyo si kwa sasa. Kwa sasa, Kwa asilimia 100 akili yangu nimeielekeza Selecao (Kireno, maana yake timu ya taifa ya Brazil), na natumaini nitakuwepo na kushinda na timu yangu kwenye Kombe la Mabara.
"Ni jambo la kujivunia mno kwangu kucheza nimevaa jezi za njano, karibu mno na familia yangu. Matatizo mengine itabidi yasubiri hadi wakati wake utakapofika.’