• HABARI MPYA

    Friday, May 11, 2012

    DINO ZOFF ALIYESIMAMA LANGONI DAKIKA 1142 BILA KUTUNGULIWA


    HUWEZI kuzungumzia makipa waliowahi kung’ara zaidi duniani, bila kumtaja na Dino Zoff (pichani kushoto) wa Italia aliyezaliwa Februari 28, mwaka 1942 mjini Mariano del Friuli.
    Kipa huyo wa zamani wa kimataifa wa Italia, amewahi kuidakia Azzuri hadi kuiwezesha kutwaa Kombe la Dunia, akiwa na Nahodha wa kikosi hicho mwaka 1982 katika fainali zilizofanyika nchini Hispania, wakati huo akiwa ana umri wa miaka 40 na miezi minnena siku 13.
    Zoff alikuwa kipa wa uhakika, mwenye uwezo mkubwa wa kuokoa michomo kiasi kwamba aliteuliwa kuwa kipa namba tatu kwa ubora duniani kihistoria katika karne ya 20, nyuma ya Lev Yashin na Gordon Banks.
    Anashikilia rekodi ya kusimama langoni muda mrefu zaidi bila kuruhusu bao katika michuano ya kimataifa, akiwa amesimama kwenye milingoti mitatu dakika 1142 kati ya mwaka 1972 na 1974 bila kwenda kuokota mpira nyavuni.
    Akiwa amedeaka mechi 112, anashika nafasi ya tatu nyuma ya Fabio Cannavaro na Paolo Maldini katika kucheza mechi nyingi zaidi kwenye kikosi cha Azzurri.
    Mwaka 2004, Pele alimuingiza kipa huyo katika orodha ya wanasoka ‘babu kubwa’ 125 kuwahi kutokea duniani.
    Dino Zoff alizaliwa Mariano del Friuli, Friuli-Venezia Giulia nchini Italia na kisoka alianza kuibuka akiwa ana umri wa miaka 14 alipokuwa akifanya majaribio kwenye klabu ya Inter Milan na Juventus F.C., kabla ya kupigwa chini kutokana ufupi wake.
    Miaka mitano baadaye akiwa ameongezeka urefu kwa sentimita 33,  alifanikiwa kucheza mechi ya kwanza ya Ligi Kuu ya Italia, Serie A akiwa na klabu ya Udinese, ingawa katika kipindi chote cha kuwa na klabu hiyo Zoff alicheza mechi nne tu kabla ya kutimkia Mantova mwaka 1963.
    Mwaka 1968, Zoff alihamishiwa Napoli. Mwaka huo huo, aliichezea Italia mechi ya kwanza katika mechi dhidi ya Bulgari, ikiwa ni Robo Fainali ya ya Euro mwaka 1968.
    Alianza vizuri kwa kuiwezesha Italia kutwaa taji hilo nyumbani, Zoff baada ya kucheza mechi nne tangu hapo.
    Aliachwa katika kikosi cha kwanza cha Italia kilichocheza fainali za Kombe la Dunia mwaka 1970, ingawa Zoff alirejea kwenye mafanikio baada ya kusaini Juventus mwaka 1972.
    Katika miaka 11 ya kuwa na Juventus, Zoff alitwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Italia, Serie A mara sita, Coppa Italia mara mbilina Kombe la UEFA mara moja.
    Hata hivyo, mambo makubwa zaidi Zoff aliyafanya katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 1982, akiwa Nahodha wa Italia alipoiwezesha kutwaa taji hilo katika umri wa miaka 40, akiweka rekodi ya kuwa kipa mzee zaidi kutwaa ubingwa wa dunia wa kandanda.
    Alifuatia mafanikio ya Giampiero Combi, kuwa kipa wa pili kuwa Nahodha wa kikosi cha ubingwa wa Dunia.
    Aidha, alichaguliwa pia kuwa kipa bora wa michuano hiyo na kocha wa kikosi hicho, Enzo Bearzot alisema; “Alikuwa kipa wa kiwango cha juu mno, alifanya shughuli nzuri sana akiokoa michomo ya hatari na kuisaidia timu. Mwishoni mwa mchezo dhidi ya Brazil, alikuja kunipiga busu shavuni, bila kusema neon lolote. Kwangu, ulikuwa wakati mzuri sana katika Kombe la Dunia,”.
    Zoff, Gianpiero Combi na Iker Casillas aliyeiwezesha Hispania kutwaa Kombe la Dunia mwaka 2010 hao ndio makipa pekee hadi sasa kuwa Manahodha wa vikosi vya ubingwa wa Kombe la Dunia. Rekodi yake ya kutofungwa muda mrefu katika mechi za kimataifa ilitibuliwa na mchezaji wa Haiti, Manno Sanon aliyemtungua bao tamu katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 1974.
    Anashikilia pia rekodi ya kuwa mchezaji ‘mzee’ zaidi kucheza Serie A na pia alikuwa anashikilia rekodi ya kucheza mechi nyingi zaidi kwenye ligi hiyo, akiwa amedaka mechi 570 kwa miaka zaidi ya 20, hadi msimu wa 2005–2006 rekodi hiyo ilipovunjwa na kipa wa S.S. Lazio, Marco Ballotta na beki wa A.C. Milan, Paolo Maldini.
    Baada ya kustaafu soka, Zoff kama wanasoka wengi wengine alihamia kwenye ukocha, akiingia kwenye benchi la ufundi la klabu ya Juventus, ambako aliteuliwa kuwa Kocha Mkuu kuanzia mwaka 1988 hadi 1990.
    Mwaka 1990 alitupiwa virago, licha ya kuiwezesha timu hiyo kutwaa Kombe la UEFA. Akajiunga na Lazio, ambako aliteuliwa kuwa rais wa klabu hiyo mwaka 1994.
    Mwaka 1998, Zoff aliteuliwa kuwa kocha wa timu ya taifa ya Italia, akitambulisha mfumo wa kushambulia ‘mwanzo mwisho’, ambao haswa ndio mfumo wa Azzuri na aliiwezesha timu hiyo kuwa mshindi wa pili kwenye Euro mwaka 2000.
    Alikaribia kutwaa taji kama si Ufaransa kupata bao la kusawazisha dakika za majeruhi kwenye fainali. Siku chache baadaye Zoff alijiuzulu, kutokana na kutupiwa ‘madongo’ na rais wa A.C. Milan, Silvio Berlusconi aliyekuwa pia Waziri Mkuu wa Italia, ambaye naye hivi karibuni amejiuzulu nafasi yake ya kisiasa kwa shinikizo la wananchi.
    Zoff alirejea Lazio, lakini alistaafu kutokana na matokeo mabaya mwanzosni mwa msimu wa 2001–2002. Mwaka 2005, alipewa Ukocha wa Fiorentina.
    Lakini baada ya kuwasaidia kuepuka kushuka daraja siku ya mwisho ya msimu, Zoff alionyeshwa mlango wa kutokea. Kwa muhtasari huyo ndiye Dino Zoff, kipa mwenye rekodi kibao za kipekee duniani.

    WASIFU WAKE:
    JINA: Dino Zoff
    KUZALIWA: Februari 28, 1942 (Miaka 69)
    ALIPOZALIWA: Mariano del Friuli, Italy
    NAFASI: Kipa
    KLABU ALIZOCHEZEA:
    Mwaka         Klabu
    1961–1963 Udinese (Mechi 38)
    1963–1967      Mantova (Mechi 131)
    1967–1972      Napoli (Mechi 143)
    1972–1983      Juventus (Mechi 330)
    JUMLA: Mechi 642
    (Tangu 1968 hadi 1983 aliidakia Italia mechi 112)
    TIMU ALIZOFUNDISHA:
    1988–1990      Juventus
    1990–1994     Lazio
    1996–1997      Lazio
    1998–2000    Italia
    2001                  Lazio
    2005                 Fiorentina
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DINO ZOFF ALIYESIMAMA LANGONI DAKIKA 1142 BILA KUTUNGULIWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top