• HABARI MPYA

    Friday, May 11, 2012

    SOCRATES ALIYEWALIZA WABRAZIL


    Marehemu Socrates

    WAPENZI wa soka duniani walizipokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa gwiji wa zamani wa soka nchini Brazil, Socrates aliyefariki dunia Desemba 4, mwaka jana akiwa ana umri wa miaka 57.
    Utanashati wake na kitendo chake cha kujiingiza kwenye siasa kwa undanikilimfanya awe mtu wa kipekee katika soka ya Brazil, akijitofautisha mno na wasanoka wa enzi zake hata wa sasa.
    Alifahamika zaidi pale alipokuwa Nahodha wa kikosi cha Brazil katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 1982, ikichukuliwa na wengi kama timu bora daima ya Brazil ambayo haikuwahi kutwaa taji kubwa la michuano ya kandanda.
    Lakini pia alikuwa maarufu mno kwa kuutandika mtindi, yaani kilevi, jambo ambalo inaelezwa limechangia kifo chake katika umri huo.
    Taarifa kutoka hospitali ya Albert Einstein ilisema kwamba Socrates alifariki kutokana na mshituko majira ya saa 4:30 asubuhi saa za Brazil.
    Rais wa Brazil, Dilma Rousseff alisema Brazil imepoteza mmoja wa watoto wake adimu.”
    “Ndani ya Uwanja, kwa kipaji chake na harakati zake, alikuwa mweledi,” alisema katika taarifa yake. “Nje ya Uwanja, … alikuwa mwanasiasa haswa, aliyejihusisha na nchi yake na watu wake.”
    Rais wa zamani, Luiz Inacio Lula da Silva pia alielezea machungu yake kutokana na msiba huo.
    “Socrates’ alikuwa ana mchango mkubwa kwa Corinthians, kwa soka na jamii ya Wabrazil haitaweza kumsahau daima,” alisema Silva, mpenzi wa Corinthians, klabu ambayo Socrates aliichezea miaka ya 1980.
    Socrates alikimbizwa hospitali siku chache kabla ya kifo chake akiwa mwenye hali mbaya na kuwekewa uangalizi maalum. Hiyo ilikuwa mara ya tatu ndani ya miezi minne kwake kulazwa hospitalini chini ya uangalizi maalum, mara ya mwisho ikiwa Septemba, mwaka jana.
    Mara mbili za mwanzo ilielezwa kwamba alikuwa ana tatizo lililosababishwa na presha ambayo ilitokana na damu kubadilisha mwelekeo wake na kuelekea kwenye ini.
    Socrates hakuwahi kukanusha tuhuma za ‘ulevi mbwa’ enzi zake akicheza miaka ya 1980, lakini alisema aliacha kuutandika mtindi mapema mwaka jana baada ya kufikishwa hospitali.
    “Socrates alionekana kama mchezaji wa zamani nyingine,” alisema mshambuliaji wa zamani wa Italia, Paolo Rossi. “Huwezi kumuweka katika kipengele chochote — ndani na nje ya Uwanja.
    Kila mmoja alijua juu ya Shahada yake katika dawa za tiba za wanadamu na alikuwa ana tamaduni nyingi na aliyejihusisha na mambo ya kijamii pia. Alikuwa wa kipekee kwa kila mtazamo.”
    Socrates aliangukia kwenye udaktari baada ya kustaafu soka na baadaye akwa mchambuzi na mwana safu maarufu wa kwenye TV, wakati wote akiwa mwenye mawazo ya kipekee na maoni ya kutatanisha.
    Tangu zake za kucheza, Socrates hakuwahi kukaa nayo moyoni mawazo yake ya kisiasa, alikuwa akiandika kwenye safu yake. Alifahamika kama Dk. Socrates kwa sababu ya utaalamu wake dawa, na alikuwa hodari wa kufanya mahojiano na vyombo vya habari.
    Akiwa Corinthians, Socrates alianzisha harakati za kutetea haki za wachezaji katika klabu hiyo zilizojulikana kama Corinthians Democracy.
    Mweledi huyo alikuwepo kwenye kikosi cha Brazil kwenye fainali za Kombe la Dunia mwaka 1986 nchini Mexico, lakini zilikuwa fainali za mwaka 1982 nchini Hispania aliweka historia akiwa na Brazil, ambayo Brazil pamoja na kuwa na kikosi kikali zaidi kihistoria haikushinda taji.
    Akiwa na wachezaji kama Zico na Falcao, walifungwa na Italia 3-2 katika Raundi ya Pili licha ya kuhitaji sare tu ili watinge Nusu Fainali.
    Kifo chake kiliwahuzunisha wengi wakiwemo wachezaji wenzake kama Rossi, ambaye alifunga mabao matatu peke yake katika mechi hiyo.
    Wachezaji kibao wa Brazil wameelezea majonzi ya kutokana na msiba huo.
    “Machungu ni tangu siku ile,” alisema mshambuliaji mstaafu wa Brazil, Ronaldona kuongeza. “Pumzika kwa amani Dk. Socrates.”
    Socrates aliandika makala kibao katika safu yake wakati wa michuano ya Copa America nchini Argentina mwaka jana, akielezea maoni yake kuhusu mashindano hayo, ikiwemo suala la kiuchumi na masuala ya kisiasa Latin America.
    Socrates, ambaye jina lake halisi ni Socrates Brasileiro Sampaio de Souza Vieira de Oliveira, pia alichezea klabu za Flamengo and Santos.
    Socrates alikuwamo kwenye orodha ya wanasoka 125 bora wanaoishi ya FIFA, orodha ambayo ilitayarishwa na gwiji mwingine wa zamani wa Brazil, Pele.
    Socrates aliichezea mechi 63 timu ya taifa ya Brazil na kuifungia mabao 25.
    Socrates pia aliifundisha na kuichezea kwa muda mfupi klabu ya Garforth Town nchini England mwaka 2004.
    Mdogo wa Socrates, Rai alikuwa kiungo mahiri wa Brazil na aliisaidia timu hiyo kutwaa Kombe la Dunia mwaka 1994 Marekani.
    Mazishi yake yalifanyika nyumbani kwao Ribeirao Preto, huko Sao Paulo na ameacha mke na watoto sita. Mungu aiweke pema peponi roho ya marehemu. Amiiin.

    WASIFU WAKE:
    JINA KAMILI: Sócrates Brasileiro Sampaio de Souza Vieira de Oliveira
    KUZALIWA: Februari 19, 1954
    ALIPOZALIWA: Belém do Pará, Brazil
    KUFARIKI DUNIA: Desemba 4, 2011 (Miaka 57)
    ALIPOFIA: São Paulo, Brazil
    NAFASI YAKE: Kiungo mshambuliaji
    TIMU ALIZOCHEZEA:
    Mwaka               Timu
    1974–1978            Botafogo-SP (Mechi 57, mabao 24)
    1978–1984            Corinthians   (Mechi 297, mabao172)
    1984–1985            Fiorentina     (Mechi 25, mabao 6)
    1986–1987            Flamengo      (Mechi 11, mabao 3)
    1988–1989            Santos         (Mechi 5, mabao 2)
    1989                   Botafogo-SP (Aliishia kusugua benchi)
    2004                       Garforth Town (Mechi 1, bao 1)
    JUMLA)               (Mechi 396, mabao 207)
    (Tangu 1979 hadi 1986, aliichezea Brazil mechi 60, akaifungia mabao 22)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SOCRATES ALIYEWALIZA WABRAZIL Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top