• HABARI MPYA

    Saturday, May 05, 2012

    LIGI KUU HII INATIA KICHEFUCHEFU


    Emanuel Okwi wa Simba, mmoja wa wachezaji waliong'ara Ligi Kuu Bara

    BAADA ya miezi nane ya patashika ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara, kesho ligi hiyo inafikia tamati kwa timu zote 14 kushuka dimbani kwenye viwanja tofauti, huku kivutio kikubwa kikiwa mchezo wa watani wa jadi Simba na Yanga kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
    Ni mechi inayosubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka, na sababu kubwa ni kwamba, matokeo ya mechi hiyo yanaweza kuwa seheme ya kutoa bingwa wa ligi hiyo msimu huu.
    Mechi nyingine za kesho ni Oljoro JKT itakayoikaribisha Polisi Dodoma kwenye Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha wakati Ruvu Shooting itacheza na Villa Squad kwenye Uwanja wa  Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.
    Aidha, Coastal Union itacheza na Toto African Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, huku African Lyon ikicheza na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Manungu mkoani Morogoro.
    Timu ya Azam itaikaribisha Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Chamazi jijini Dar es Salaam na Moro United itakuwa ikicheza na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
    Kimahesabu, ni timu za Simba na Azam ndizo zenye nafasi ya kutwaa ubingwa ulioachwa wazi na Yanga.
    Kwa mujibu wa kanuni namba 4(2)(c) ya Ligi Kuu, timu tatu za mwisho katika msimamo wa ligi zitashuka daraja, ambapo tayari Moro United na Polisi Dodoma zimeshashuka, iliyobaki itajulikana baada ya mechi za kesho ambazo zote zitaanza saa 10 kamili jioni ili kuepuka upangaji wa matokeo.
    Katika hali halisi ya uendeshaji ligi, hakuna msimu uliowahi kupita bila kuwapo na upungufu, na ndivyo ilivyokuwa msimu huu unaofikia tamati kesho, ambapo tumeshuhudia malalamiko chungu mzima.
    Pamoja na kuwapo na malalamiko kila msimu, lakini kile kilichoshuhudiwa msimu huu, kimeonyesha sura mpya jinsi ligi hii inavyoendeshwa bila mpangilio wenye heshima ya mchezo wa soka.
    Tatizo kubwa linaloendelea kuzungumzwa mpaka sasa, ni suala la waamuzi ambao wamekuwa wakilalamikiwa kila kona kwa sababu ya, aidha kuchezesha kwa upendeleo au kutosimamia ipasavyo sheria za mchezo huo.
    Ingawa hatuwezi kukubali moja kwa moja malalamiko yote yaliyoelekezwa kwao waamuzi yalikuwa na msingi, lakini bado pia hatuwezi kuficha ukweli kwamba hakukuwa na upungufu.
    Eneo lingine lililoongoza kupokea malalamiko ni kamati mbalimbali za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ambazo kuna wakati zilipinga waziwazi katika kutoa uamuzi wa masuala kadhaa yaliyoletwa mezani kujadiliwa.
    Kutokana na udhaifu wa kiutendaji wa kamati hizi, ilifika wakati zililazimika kuuleta mchezo wa soka mezani na kutoa matokeo badala ya viwanjani kama taratibu zinavyoonyesha.
    Kwa jumla kamati hizi zilivuruga sana ligi, ziliwachanganya wadau na wapenzi wa soka na pia zilichangia kushusha heshima ya mchezo wa soka kwa kufuta matokeo ya uwanjani na kutoa matokeo ya mezani.
    Hakuna shaka kwamba, kwa aina ya uamuzi uliokuwa ukitolewa na kamati hizi katika mambo mbalimbali waliyojadili, wadau wamepoteza imani na utendaji wake.
    Lakini pia suala la usalama kwenye viwanja nalo ni tatizo kubwa msimu huu, ambapo mara nyingi tumeshuhudia mashabiki wakifanya uharibifu kwenye Uwnaja wa Taifa hasa kwenye mechi zinazohusu timu za Simba na Yanga.
    Aibu nyingine kubwa ni kukosekana kwa magari ya huduma ya kwanza viwanjani kwa ajili ya kutoa usafiri wa haraka kwenda hospitali iwapo kutakuwa na tatizo lolote.
    Isitoshe, viwanja vilivyotumika katika mechi za ligi navyo vimelalamikiwa kwa kiasi kikubwa kutokana na kuwa chini ya kiwango kwa mashindano makubwa kama ya Ligi Kuu.
    Tumeona pia upungufu wa utawala bora kwa baadhi ya viongozi wa timu za Ligi Kuu uliopelekea baadhi ya makocha kuacha kufundisha timu hizo.
    Baadhi ya viongozi wa klabu wamekuwa chanzo kuendesha klabu bila kuzingatia kanuni, jambo ambalo mara kwa mara limekuwa likileta maelewano finyu kati ya wanachana na viongozi.
    Tunaamini TFF na klabu zetu za soka zimeona upungufu huu na hii iwe changamoto ya kufanya marekebisho ili msimu ujao ligi iwe na sehemu kubwa ya ushindani kuliko kiyume chake.
    TFF kwa kushirikiana na kamati zake, inapaswa kukaa chini na kuweka mambo sawa, kwani sehemu kubwa ya malalamiko toka kwa wadau msimu huu yanagusa moja kwa moja utendaji wa shirikisho hilo. 

    GAZETI LA MWANANCHI
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LIGI KUU HII INATIA KICHEFUCHEFU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top