• HABARI MPYA

    Saturday, May 05, 2012

    TUCHEZA LIGI KUU TUKIWA TUNATAMBUA KANUNI ZAKE


    Beki Chacha Marwa wa Yanga kulia, katika moja ya mechi Ligi Kuu 

    MASHINDANO yoyote yale ili yaendeshwe kwa ufanisi na ushindani wa haki ni lazima yawe na kanuni. Na si tu kuwa na kanuni, bali pia ziwe zinaeleweka kwa wahusika.
    Kama ilivyo kwa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) nalo linaendesha mashindano yake kwa kutumia kanuni. Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara ina kanuni zake kama ilivyo kwa Ligi Daraja la Kwanza, Ligi ya Taifa, Kombe la Taifa, michuano ya Copa Coca Cola na mingineyo.
    Ili timu iwe mshiriki na mshindani wa kweli katika michuano hiyo ni lazima iwe na ufahamu katika michuano husika. Ni rahisi timu kupoteza ushindi, kupigwa faini na hata kupokwa haki ikiwa haina ufahamu wa kanuni.
    Kama timu inashiriki mashindano halafu haifahamu kanuni za mashindano husika inawezaje kuwa mshindani wa kweli? Ni kawaida kwa klabu za Tanzania katika ngazi mbalimbali, hata mashindano ya kugombea mbuzi kuingiza timu bila kuomba, kupewa au kutaka kufahamu kanuni kwa mashindano husika.
    Hali hiyo husababisha vurugu katika mashindano kwa vile timu inaposhindwa mechi hulalamikia vitu vingine ambavyo kwa mujibu wa kanuni havikupaswa kulalamikiwa, lakini kwa upofu wa kanuni timu au klabu hulalamika.
    Hufika mahali klabu inaelekeza nguvu katika malalamiko au rufani kuliko kuwekeza katika timu ili iweze kufanya vizuri, ambapo matokeo yake ni kutokuwepo ushindani kutoka kwa timu husika au mashindano yenyewe kwa ujumla.
    Katika TFF chombo chenye mamlaka ya kupitisha au kurekebisha kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom ni Kamati ya Utendaji. Hata hivyo ni utaratibu wa TFF kukaa na klabu za Ligi Kuu kila yanapofanyika marekebisho kabla ya kuwasilishwa mbele ya Kamati ya Utendaji.
    Mfano Kanuni ya 61 kuhusu kocha wa timu inasema: “(1) Klabu inapaswa kuajiri kocha wa timu mwenye ujuzi wa kutosha na anayetambuliwa na Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu Tanzania (TAFCA), na mkataba wake kusajiliwa TFF.
    “(2) Kocha klabu ya Ligi Kuu anatakiwa awe na Stashahada au cheti cha ngazi pevu ya ufundishaji. (3) Kocha kutoka nje atathibitishwa na TFF kabla ya kuingia mkataba na klabu na kupewa kibali cha kuishi na kufanya kazi nchini.
    “(4) Kocha atatakiwa kuwa na leseni daraja A kutoka TFF kuweza kufundisha klabu ya Ligi Kuu. (5) Kocha wa timu ndiye mkuu wa shughuli zote za timu kuanzia usajili wa wachezaji, uandaaji wa timu, usimamiaji katika mashindano na mambo mengine yanayofanana na hayo.”
    Ni kocha wa sifa za aina gani anaweza kufundisha timu ya Ligi Kuu na kwa utaratibu upi. Kanuni hiyo ya 61 imeelezea hayo kwa lugha nyepesi na inayoeleweka. Lakini pamoja na kanuni kuwa wazi, bado ni kawaida katika klabu za Ligi Kuu kusikia matatizo kadha wa kadha kuwahusu makocha ambao ni muhimu katika timu zao katika utengenezaji wa aina ya uchezaji.
    Kwa kifupi aina ya uchezaji au mfumo wa uchezaji hupangwa au uamuriwa na kocha kutokana na aina ya wachezaji alionao, lengo siku zote ikiwa ni kuhakikisha timu inacheza vizuri. Mara nyingi matokeo ya kucheza vizuri ni ushindi.
    Licha ya kanuni kama hizo kutengenezwa bado yamekuwepo matatizo kwa makocha. Je, ni kipi chanzo cha matatizo hayo? Ukweli unabaki kuwa kutojua au kutozingatia kanuni ndiyo msingi wa migogoro isiyokwisha inayohusu makocha kwa upande mmoja na viongozi wa klabu kwa upande mwingine.
    Kanuni hiyo inayohusu makocha ni mfano tu kuonesha jinsi wadau wa mashindano husika walivyokosa umakini katika suala la msingi kama hilo. Kanuni ndiyo mwongozo wa kila kitu katika mashindano.
    Timu ikitaka iharibikiwe katika mashindano iache kuzingatia kanuni. Pia ikumbukwe kuwa kanuni zote katika mashindano ni sawa. Dhana kuwa kanuni hii ndiyo mama na ya msingi si sahihi hata kidogo, kwa vile kanuni zote zimewekwa au kutengenezwa kwa sababu maalumu.
    Ndiyo maana huwezi kukuta kanuni inayohusu Kombe la Dunia kwenye Ligi ya Taifa. Hiyo ni kutaka kuonesha kuwa kila kanuni ni muhimu kwa mashindano husika, hivyo haikutengenezwa kama mapambo.
    Klabu inayowajibika ni ile inayozingatia kanuni badala ya kufanya mambo kwa kubahatishakwa dhana kuwa wasimamizi wa mashindano au klabu pinzani haiwezi kubaini ukiukwaji wa kanuni husika.
    Ni kwa kucheza ligi huku tukifahamu kanuni ndiko kutatufanya tuongeze msisimko na kuifanya ligi yetu kuwa bora, hivyo kuvuta wadau wengine muhimu wa kurahisisha mambo yetu.

    *Makala haya imeandikwa na Boniface Wambura ambaye ni Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TUCHEZA LIGI KUU TUKIWA TUNATAMBUA KANUNI ZAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top