• HABARI MPYA

    Saturday, May 05, 2012

    AZAM IACHWE IIADABISHE SOKA YA TANZANIA


    Wachezaji wa Azam
    TUHUMA dhidi ya waamuzi kuchezesha kwa upendeleo kunako ashiria mazingira ya rushwa sio za leo ni za muda mrefu sana.
    Tuhuma za waamuzi kuchezesha chini ya kiwango na kwa upendeleo wa wazi zimechukua sura mpya kwenye msimu huu wa Ligi Kuu wa Soka Tanzania Bara kiasi cha kuonekana dalili njema ya suala lenyewe kushughulikiwa au kupatiwa ufumbuzi kudumu.
    Shukrani ziende kwa mmiliki wa klabu ya Azam Said Salim Bakhressa kuanzisha timu hiyo inayoonekana kuzizidi nguvu za kifedha miamba ya soka ya kihistoria nchini Simba na Yanga na ndio kiini cha kelele dhidi ya uamuzi mbovu unaofanywa na waamuzi wa soka hapa nchini.
    Kusingekuwepo timu yenye uwezo wa kifedha kama ya Azam kwenye Ligi Kuu ni wazi malalamiko haya dhidi ya waamuzi yasingefikia kiwango hiki kwani timu za Simba na Yanga zenye nguvu za kifedha zingeendelea kupendelewa na mashabiki wa soka nchini wangeendelea kuziweka tuhuma hizi kapuni.
    Haihitaji elimu ya chuo kikuu kubaini kuwa kama timu haina nguvu kubwa ya kifedha kama zilivyo Simba na Yanga suala la kuwa bingwa wa soka wa Tanazania Bara ni kama ndoto, kwani hata rekodi za ndani ya miaka 20 iliyopita zinaonesha timu hizo kubwa ndizo zilipokezana kutwaa ubingwa huo.
    Ukirudi nyuma kwenye miaka ya 1970 mpaka mwanzoni mwa miaka ya 1980 kiwango cha uchezeshaji cha waamuzi kilikuwa bora kidogo kutokana na maadili yaliyokuwepo kipindi hicho kiasi hata hao viongozi wa Simba na Yanga ilikuwa nadra kutuhumiwa kuzihonga timu ndogo zichukue ubingwa au hata waamuzi wenye kuzibeba timu kubwa.
    Lakini kuanzia mwishoni mwa miaka ya 1980 mpaka sasa ndani ya nchi mpira umekuwa ukichezwa zaidi nje ya uwanja hasa na timu hizi kubwa za Simba na Yanga kiasi cha kuzusha malalamiko ya mara kwa mara toka kwa timu ndogo kuwa zinaonewa zinapocheza na timu hizo.
    Lakini kwa kuwa timu hizo hazina uwezo mkubwa wa kifedha malalamiko yao ya kuonewa na timu hizo kubwa hayakuwa yanapewa uzito na matokeo yake soka la Tanzania linashuka kadiri miaka inavyokwenda mbele.
    Kupanda daraja na uwezo mkubwa wa kifedha wa Azam sasa unaonekana kuwakera mashabiki na wadau wa soka nchini na kuzusha tuhuma za rushwa dhidi ya timu hiyo, lakini ukweli ni kwamba nguvu za kifedha za timu hiyo kwa sasa zinazidi za Simba na Yanga ndio kiini cha tatizo.
    Azam imesajili wachezaji wenye uwezo mkubwa na inaonekana imedhamiria hasa kulifanyia soka la Tanzania mabadiliko kutoka kutawaliwa na Yanga na Simba kusikoleta tija kwa nchi hii.
    Na tayari dhamira ya timu hiyo imedhihirisha wazi kwani Yanga ambayo huwa ni mshiriki wa kudumu kwenye michuano ya kimataifa mwakani haitashiriki michuano hiyo na sababu kubwa ni Azam.
    Azam sasa inatoa presha kubwa kwa vinara wa ligi hiyo Simba kwenye mbio za ubingwa na ikitokea ikashinda kwa idadi kubwa ya mabao kwenye mchezo wake dhidi ya Mtibwa ulioamuliwa kurudiwa na ikaifunga mabao mengi kwenye mchezo wao wa mwisho dhidi Kagera Sugar na Yanga ikaifunga Simba leo basi timu hiyo itakuwa bingwa.
    Kama itakuwa bingwa Azam itakuwa imefanya mambo mawili makubwa ambayo wadau wa soka wa nchi hii hawako tayari kuona yanatokea kwanza kuinyima Yanga kushiriki michuano ya kimataifa na pili kuinyima kigogo kingine cha soka nchi hii ubingwa yaani Simba.
    Kwa hali hii ndio maana tuhuma dhidi ya timu hiyo kuhonga waamuzi ndipo zinapoanzia kwa sababu imezibana timu vipenzi za Watanzania walio wengi lakini wakati wadau wa soka hao wakirusha tuhuma hizo kwa Azam wajichunguze na wao wenyewe na timu zao hizo wanazozipenda.
    Kama wadau wa timu hizo ndio wameasisi msemo wa mpira fitina wakiwa na maana ya ushindi huanza kupatikana kwa mipango ya nje ya uwanja zaidi usafi wao uko wapi kiasi cha kuizonga na kuishambulia Azam.
    Haya yanayosemwa kufanywa na Azam yamekuwa yakisemwa kufanywa na Simba na Yanga muda mrefu sana, lakini hayakuwa kupata mguso kutoka kwa wadau wa soka nchini zaidi ya kusikia wanasifia viongozi wao kwa kujua fitina za mpira.
    Iachwe Azam irekebishe soka la bongo kidogo na ikibidi zitokee timu nyingine zenye uwezo kama wa Azam na ndipo umuhimu wa wadau wa soka kujikana nafsi zao kwa kutafuta matokeo ya nje ya uwanja utaonekana.

    Imeandikwa na Clecence Kunambi wa gazeti la Habari Leo..


    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM IACHWE IIADABISHE SOKA YA TANZANIA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top