• HABARI MPYA

    Saturday, May 05, 2012

    YANGA WATAMBUE KUMPIGA CHURA SI KUMKOMOA


    Amir Mhando,
    Mwandishi wa Makala hii, ambaye pia
    ni Katibu Mkuu wa TASWA

    YANGA inapita kipindi kigumu hivi sasa, kipindi ambacho ni maumivu makubwa kwa mashabiki wake.
    Hatua hiyo inatokana na timu hiyo kukosa nafasi ya kuwakilisha nchi katika michuano ya kimataifa mwakani inayoandaliwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
    Tayari wana-Yanga wamegawanyika katika makundi mawili, moja likiwashutumu viongozi na lingine likiwatetea kutokana na kuvurunda kwa timu yao kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara ambayo inamalizika kesho, hali hiyo inafanya ionekane kama kuna mgogoro, ambao kama wasipokuwa makini athari zake zitakuwa kubwa.
    Ilianza kama utani kwa wazee na baadhi ya wanachama kuhoji mwenendo mbaya wa klabu yao, lakini hali ikafika pabaya wiki iliyopita pale Baraza la Wazee la klabu hiyo lilipotangaza kwamba limechukua timu na siku moja baadaye uongozi wa Yanga ukakanusha jambo hilo na kwamba timu itaendelea kuwa chini ya uongozi.
    Pande hizo mbili karibu wiki moja sasa zimekuwa zikitupiana maneno ambayo yanaashiria hakuna amani, lakini kilinichonisukuma zaidi kuandika makala haya ni kauli ya Jumanne wiki hii, ambapo Baraza la Wazee lilitoa tamko kwamba kwa sasa limejiweka kando na kwamba mambo ya Yanga yatabaki kuwa chini ya uongozi.
    Wazee hawa hawakutoa kauli hiyo kwa nia njema, bali wamesusa. Maana walifikia hatua mpaka ya kuvua kofia zao kuwalaani viongozi wa Yanga, kwamba lolote litakalotokea wao halitawahusu.
    Kwa lugha rahisi wazee hawa wamesema: “Tutaona sasa kama watafanikiwa.” Ni kauli ambayo ukiwa na kiburi unaichukulia kwa lugha rahisi na nyepesi, lakini ukiwa na busara unaiona ni nzito na yenye kuhitaji busara zaidi ili kurudi katika msimamo mmoja.
    Kwa mtazamo wangu wana- Yanga huu si wakati wa kutengeneza migogoro, badala yake wajitahidi kwa kadri ya uwezo wao kujiepusha nao kwani kauli hiyo ina maana kama Yanga itafanya vibaya basi wazee wataibuka kidedea hasa kwenye mchezo wa kesho dhidi ya Simba na kama Yanga watashinda basi uongozi utakuwa umeibuka kidedea na hivyo heshima za wazee zitakuwa zimetetereka.
    Uzoefu wangu kunapokuwa na mgogoro katika klabu za Simba na Yanga ni rahisi sana kuwahusisha hata wachezaji wa timu hiyo na haikuwa ajabu miaka ya nyuma kusikia kuwa wachezaji wametekwa na upande fulani katika mgogoro.
    Mara nyingi sehemu panapokuwa hakuna umoja, basi hata kufanya vizuri inakuwa nadra, hivyo lazima hili lifikiriwe kwa makini.
    Kwa mtazamo wangu wazee wa Yanga hawakupaswa kuchukua hatua ya kuwasusa viongozi, kwani binafsi naamini kumpiga chura teke si kumkomoa, bali unamuongezea mwendo. Kama walifanya hivyo kwa imani kwamba uongozi wa Yanga utatetereka hilo halipo, bali wenzao ndiyo wamezidi kufurahia.
    Ingekuwa vyema wazee wa Yanga wangehakikisha wanakaa chini na uongozi kwa nia njema ya kujenga umoja kwa maslahi ya Yanga.
    Ufike wakati sasa klabu zifanye mambo kisayansi zaidi badala ya kukurupuka katika jazba na chuki ambazo hazina msaada wowote kwa maendeleo ya mchezo huo.
    Hivyo kila hatua ambayo itachukuliwa na kundi lolote ndani ya Yanga lazima itazamwe kwa umakini na upeo wa hali ya juu kwani ninavyojua mimi Simba na Yanga, kila zinapofanya vibaya huwa hazikosi sababu ambazo si za kitaalamu na zaidi ni kutupiana lawama zisizo na msingi.
    Huwa naamini gari ya fundi makanika hailali njiani ikipata matatizo, atajitahidi kuikorokochoa iendelee na safari.
    Hivyo hata kwa Yanga wajitahidi kadri wawezavyo kumaliza tatizo hili kwa pamoja. Kwa vyovyote iwavyo Yanga hawatakiwi kususiana, kufanya hivyo si kuijenga timu lakini pia watambue kukimbia tatizo si suluhisho, bali walikabili kwani mlevi huwa hasusiwi pombe, Nawasilisha.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WATAMBUE KUMPIGA CHURA SI KUMKOMOA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top