• HABARI MPYA

    Tuesday, May 08, 2012

    SIMBA WAENDA SUDAN NA NDEGE YA KUKODI


    Kikosi cha Simba

    BAADA ya kumaliza Ligi Kuu bara kwa kishindo, Simba sasa inajipanga kwa safari ya kwenda Sudan kwa ajili ya mechi ya michuano ya kimataifa, na imepanga kuondoka kesho kwa ndege ya kukodi.
    Gazeti la Habari leo, limeandika kwamba Simba iliifunga Yanga mabao 5-0 juzi katika mechi ya mwisho ya Ligi hiyo na hivyo kunogesha furaha za kutwaa ubingwa ilioutwaa tangu Ijumaa iliyopita.
    Akizungumza Dar es Salaam jana, makamu mwenyekiti wa Simba Godfrey Nyange ‘Kaburu’ alisema kuwa timu yao itaondoka kesho kwa ndege ya kukodi kuelekea Sudan kwa ajili ya mchezo wa marudiano wa Kombe la shirikisho dhidi ya Al Ahly Shandy ya huko.
    Katika mechi ya kwanza ya raundi ya tatu ya michuano hiyo iliyochezwa Uwanja wa Taifa takriban wiki moja iliyopita, Simba ilishinda kwa mabao 3-0 na hivyo kuhitaji sare ama ushindi wa aina yoyote kwenye mechi hiyo ili kufuzu kwa hatua inayofuata.
    Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage amesema kuwa mafanikio ya timu yao msimu huu yanatokana na ushirikiano mzuri kati ya uongozi wa sasa, uongozi uliopita na marafiki wa klabu hiyo ‘Friends of Simba’.
    Rage akizungumza baada ya ushindi wa juzi dhidi ya Yanga, alisema kuwa mshikamano uliokuwepo ndani ya klabu hiyo kwa sasa ndio siri ya mafanikio ya timu yao.
    Alisema kuwa siku zote panapokosekana mshikamano madhubuti miongoni mwa wanachama wa klabu hiyo lazima timu yao inakuwa haifanyi vizuri, lakini kwa sasa kwa kuwa wako pamoja ndio maana mafanikio yanaonekana.
    Alisema ana furaha kuhitimisha furaha yao ya kutwaa ubingwa kwa kuifunga Yanga kwani ubingwa wao usingenoga kama wasingeibuka na ushindi dhidi ya timu hiyo yenye upinzani wa kihistoria na vijana hao wa Msimbazi.
    Aliongeza kuwa alijua fika kuwa wangeifungaYanga kwa idadi hiyo ya mabao kwani hata wakati anazungumza na kituo kimoja cha redio kabla ya mechi hiyo aliwaeleza wazi kuwa wataifunga
    Yanga kwa mabao matano.
    Aidha, alisema kuwa timu yao sasa imeiva kimazoezi na kwamba inaweza kuhimili dakika 90 za mchezo bila kuchoka tofauti na zamani ambapo baada ya kuingia kipindi cha pili vijana wao walikuwa wakionekana kuchoka haraka. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA WAENDA SUDAN NA NDEGE YA KUKODI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top