• HABARI MPYA

    Sunday, July 01, 2012

    SUMAYE AISIKITIKIA SOKA YA TANZANIA, SIMBA, YANGA NDIO WAMTIA KICHEFUCHEFU KABISAAAA



    Waziri Mkuu wa zamani, Mh Frederick Sumaye akihutubia jana katika tuzo za washindi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, hoteli ya Double Tree, Masaki, Dar es Salaam.


    Na Prince Akbar
    WAZIRI Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye amesema kwamba soka ya Tanzania kwa sasa imepoteza umaarufu wake, tofauti na ilivyokuwa awali kuanzia miaka ya 1970.
    Akizungumza jana katika halfa ya kukabidhi tuzo za washindi mbalimbali wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, iliyofanyika katika hoteli ya Double Tree By Hilton, Masaki, Dar es Salaam, Sumaye alisema kwamba sababu ya kuporomoka kwa soka yetu ni mtazamo wa hapa hapa wa klabu zetu.
    Sumaye alitolea mfano vigogo wa soka nchini, Simba na Yanga na kusema kwamba timu moja ikimfunga mwenzake inaona imemaliza na haifanyi jitihada za ziada za kufika mbali zaidi.
    “Umefika wakati timu zetu zijifunze kwa timu za nje, hata timu nyingine hizi zinazosifiwa kuibuka kuja kuvipiku vigogo vya soka (Simba na Yanga), nazo zikifunga Simba au Yanga, zinaona zimemaliza, lazima tubadilike tufikirie kufika mbali zaidi,”alisema Sumaye.
    Waziri Mkuu huyo, ambaye kuna tetesi ataomba ridhaa ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CCM katika uchaguzi Mkuu ujao, mwaka 2015, alisema kwamba Watanzania kwa sasa wanaangalia zaidi soka ya nje kuliko ya nyumbani kutokana na kushuka kwa mchezo huo hapa nchini.
    “Ili turudishe heshima, lazima tupambane kurudisha kiwango, tufikirie kuwa kama timu nyingine za Afrika zinazofanya vizuri, sio kuishia kuangaliana hapa hapa wenyewe kwa wenyewe,” alisema.
    Aidha, Sumaye alisema anasikitishwa na desturi ya Simba na Yanga kuzomeana zinapocheza na timu za nje na akashauri wakati umefika sasa kuachana na desturi hiyo yenye kutia aibu.
    “Tuvuke huko, tuwe tunazomeana nyumbani tu, wewe unashangilia timu ya Burundi, una uhusiano nao gani? Tuwe na uzalendo na tutafika mbali,”alisema Sumaye, ambaye ni kipenzi cha Watanzania wengi, kutokana na kumbukumbu ya uongozi bora akiwa Waziri Mkuu wa Rais Benjamin Mkapa katika awamu ya tatu.
    Aidha, Sumaye pia alielezea kukerwa na migogoro katika soka ya Tanzania pamoja na viongozi wa klabu kutojali maslahi ya wachezaji na akaasa hayo yaepekwe ili kukuza soka yetu.
    “Mimi nachukizwa sana naposikia migogoro, tunagombea nini? Kama mimi nitaomba nafasi kwa maslahi ya jamii, siwezi kupambana kwa kufa na kupona, lakini kama nitaomba uongozi kwa maslahi binafsi, nitapambana kufa na kupona.
    Naomba viongozi wa sasa, amueni kutumikia klabu na kujali maslahi ya wachezaji. Wachezaji wetu wanaingia uwanjani tayari miguu haina nguvu, kwa sababu sisi viongozi tunawanyonya,” alisema Sumaye, ambaye ni mpenzi wa Simba SC.
    Pamoja na ukweli huo kwamba yeye ni ‘Simba damu’, ila Sumaye alisema anapenda timu ambayo inafanya vizuri uwanjani.
    Serikali ya awamu ya tatu, ambayo Waziri Mkuu wake alikuwa Sumaye, ilifanya mambo mengi katika sekta ya michezo ikiwemo kujenga Uwanja wa kisasa wa michezo, Uwanja wa Taifa  
    Katika sherehe hizo za utoaji tuzo kwa wanamichezo bora jana usiku, hoteli ya
    Double Tree By Hilton, Masaki, Dar es Salaam, beki Aggrey Morris anayechezea Azam aliibuka mchezaji bora wa ligi hiyo wakati Juma Kaseja anayedakia Simba alikuwa kipa bora.
    Kila mmoja alizawadiwa sh. 3,312,500 katika hafla hiyo ambayo mgeni rasmi alikuwa Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye. Kaseja aliwashinda makipa Mwadili Ally (Azam) na Deogratias Munishi (Mtibwa Sugar) wakati Morris aliwashinda Haruna Niyonzima (Yanga) na Haruna Moshi (Simba).
    John Bocco wa Azam aliyefunga mabao 19 ndiye mfungaji bora, refa bora ni Martin Saanya kutoka Morogoro ambaye aliwashinda Oden Mbaga (Dar es Salaam) na Amon Paul (Mara) wakati kocha bora ni Stewart Hall wa Azam aliyewashinda Charles Kilinda (JKT Ruvu) na Charles Mkwasa (Ruvu Shooting). Kila mshindi mepata sh. 3,875,000.
    Timu yenye nidhamu bora ni Azam iliyopata sh. 7,750,000, mshindi wa tatu Yanga sh. 15,500,000, makamu bingwa Azam sh. 22,000,000 na bingwa Simba sh. 50,000,000.
    Pia Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limewazawadia sh. 1,000,000 kila mmoja kwa wachezaji watatu vijana wenye umri chini ya miaka 20 waliofanya vizuri kwenye ligi hiyo.
    Wachezaji hao ambao walikuwa kwenye vikosi vya kwanza vya timu zao ni Frank Domayo (JKT Ruvu), Rashid Mandawa (Coastal Union) na Hassan Dilunga (Ruvu Shooting).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SUMAYE AISIKITIKIA SOKA YA TANZANIA, SIMBA, YANGA NDIO WAMTIA KICHEFUCHEFU KABISAAAA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top