• HABARI MPYA

    Wednesday, August 15, 2012

    SIMBA NA AZAM TAIFA LEO MECHI YA KISASI BILA MASTAA WA TAIFA STARS KABLA YA NGAO

    Vikosi vya Simba (JUU) na Azam FC (CHINI) vilivyomenyana kwenye Robo Fainali ya Kombe la Kagame


    Na Mahmoud Zubeiry
    NYASI za Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, leo zinatarajiwa kuhimili mechi mbili kali za Nusu Fainali ya michuano ya BankABC Sup8r, Mtibwa Sugar ya Morogoro wakianza kumenyana na Jamhuri ya Pemba kabla ya Simba kukipiga na Azam FC.
    Mara ya mwisho timu hizo zilipokutana katika Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, Azam iliichapa Simba 3-0 na zitakutana tena kwenye mechi ya Ngao ya Jamii.
    Mtibwa inapewa nafasi kubwa ya kuitoa Jamhuri, lakini kuna hatari Azam FC wakapewa mshangao na Simba SC leo.
    Tangu mwanzo wa mashindano haya, Simba imekuwa ikitumia kikosi chake cha vijana, Simba B, kilicho chini ya kocha Suleiman Abdallah Matola, lakini kuna uwezekano leo, baadhi ya wachezaji wakatolewa kwenye kambi ya Simba A mjini Arusha kuja kuongeza nguvu.
    Uongozi wa Simba unahitaji fedha kufidia makovu ya usajili na Sh. Milioni 40 ni nyingi, wakitoa Sh. Milioni 10 kuwapa bonasi wachezaji kwa kutwaa Kombe, zinazobaki zinafidia kabisa makovu ya usajili- hivyo haitakuwa ajabu nyota waliopo kambini Arusha wakionekana Taifa leo.
    Lakini Matola mwenyewe alipozungumza na BIN ZUBEIRY alisema kwamba anawaamini sana vijana wake kwamba wanaweza kuitoa Azam inayotumia nyota wake wa Ligi Kuu wenye uzoefu.
    “Yaani katika mashindano haya siihofii timu yoyote. Na sihitaji mchezaji hata mmoja wa timu ya kwanza ili kuitoa Azam, hawa vijana nilionao nawaahidi wapenzi wa Simba kwamba watachukua Kombe hili,”alisema Matola.
    Matola amewataka wapenzi wa Simba SC kumiminika kwa wingi Uwanja wa Taifa, Jumatano ya leo katika Nusu Fainali hiyo, itayochezwa Saa 10:00 jioni baada ya Nusu Fainali ya Kwanza, kati ya Mtibwa Sugar na Jamhuri ya Pemba.
    Simba B ilitinga Nusu Fainali ya michuano ya BankABC Sup8r kwa kishindo, baada ya kuifunga Zimamoto ya Zanzibar mabao 2-0 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, mabao yake yote yakifungwa na kiungo chipukizi anayeinukia vema katika soka ya Tanzania, Christopher Edward kipindi cha pili.
    Christopher ambaye hukomazwa pia kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars na kikosi cha kwanza cha Simba, alifunga bao la kwanza penalti dakika ya 50, baada ya beki Miraj Adam kuangushwa kwenye eneo la hatari.
    Edward ambaye ni kipenzi cha kocha Mserbia wa Simba, Profesa Milovan Cirkovick, alifunga bao la pili dakika ya 55 baada ya kuwapiga chenga mabeki watatu wa Zimamoto kabla ya kumchambua kipa wa timu hiyo ya Zanzibar.
    Pamoja na Simba SC kuwania ubingwa wa michuano hiyo, lakini sasa Christopher ameingia kwenye mbio za kiatu cha dhahabu cha michuano hiyo, kwa kufikisha mabao manne, akiwa anaongoza.
    Katika michezo mingine ya kuhitimisha hatua ya makundi ya michuano hiyo, Uwanja wa Chamazi, Jamhuri FC iliichapa 4-0 Mtende, zote za Zanzibar mabao ya washindi yakifungwa na Sadik Rajab dakika ya 20, 44, Issa Achimwene aliyejifunga dakika ya 82 na Suleiman Khatib dakika ya 88.
    Kwenye Uwanja wa Ushirika mjini Moshi, Azam FC ilitoka nyuma kwa bao 1-0 na kuifunga Polisi Moro FC mabao 2-1, mabao yake yakitiwa kimiani na beki Said Mourad dakika ya 20 na Abdi Kassim ‘Babbi’ dakika ya 70, wakati la Maafande wa Morogoro lilitiwa kimiani na Mokili Rambo dakika ya kwanza. Polisi ilimpoteza mchezaji wake, Abdallah Rajab dakika ya 88 aliyetolewa nje kwa kadi nyekundu.
    Uwanja wa Amaan, Zanzibar, Mtibwa Sugar iliichapa 5-0 Super Falcon FC katika mchezo wa mwisho wa makundi. Mabao yake yakitiwa kimiani na Shaaban Kisiga ‘Malone’ mawili, Dickson Daud, Mohd Mpoki na Ally Mohd ‘Gaucho’.
    Katika Kundi A, Simba SC imeongoza kwa pointi zake nne, baada ya kutoa sare moja na kushinda moja, ikifuatiwa na Zimamoto na Mtende zinazofungana kwa pointi tatu kila moja, wakati Jamhuri inashika mkia kwa pointi yake moja.
    Kundi B, Mtibwa inaongoza kwa pointi zake tisa ikifuatiwa na Azam FC na Polisi Moro, zenye pointi tatu kila moja, wakati Falcon inashika mkia, ikiwa haina pointi hata moja.
    Kanuni za mashindano haya ni kushirikisha timu zilizoshika nafasi tatu za juu katika Ligi Kuu za Bara na visiwani na mbili zilioongoza katika kupanda Ligi Kuu zote mbili, lakini kwa Bara, Yanga waliokuwa washindi wa tatu msimu uliopita, walijitokea na nafasi yao ikachukuliwa na Mtibwa Sugar ambayo ilishika nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu.
    Bingwa wa michuano hiyo mipya itakayokuwa ikifanyika kila mwaka, ataondoka na Sh. Milioni 40, mshindi wa pili Sh. Milioni 20, wa tatu Sh. Milioni 15 sawa na wa nne, wakati washiriki wengine wataondoka na Sh. Milioni 5 kila moja.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA NA AZAM TAIFA LEO MECHI YA KISASI BILA MASTAA WA TAIFA STARS KABLA YA NGAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top