![]() |
| Na Mahmoud Zubeiry |
SHIRIKISHO la Soka
Tanzania (TFF), hivi sasa lipo katika mgogoro na klabu bingwa mara nne Afrika,
Tout Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)- chanzo kikiwa
na washambuliaji wawili, Mbwana Ally Samatta na Thomas Emmanuel Ulimwengu.
TP Mazembe haikumruhusu
Ulimwengu kurejea nyumbani kuichezea timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa
miaka 20, Ngorongoro Heroes katika mechi dhidi ya Nigeria na haikumruhusu
Samatta na mwenzake huyo pia kurejea nyumbani kujiunga na timu ya taifa ya
wakubwa, Taifa Stars kwa ajili ya mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya
Botswana leo mjini Gaborone.
Hii ni mara ya kwanza
kwa Mazembe kufanya hivyo, wakati wachezaji wote hao wapo katika msimu wa pili
kwenye klabu hiyo.
Kwa sababu hiyo, TFF
imesema inapeleka mashitaka Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kwa klabu hiyo kutowaruhusu
wachezaji kuchezea timu yao ya taifa, jambo ambalo kweli kwa mujibu wa kanuni
zilizowekwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) ni kosa.
TFF wameikasirikia mno
Mazembe- na hata kocha wa Taifa Stars, Mdenmark Kim Poulsen ameikasirikia mno
klabu hiyo. Binafsi, nimeumizwa na uamuzi huo wa Mazembe kutowaruhusu wachezaji,
hasa nikizingatia Ngorongoro imetolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania tiketi
ya kucheza mashindano ya U-20 Afrika, baada ya kufungwa jumla ya mabao 4-1 na
Nigeria, ikianza kuchapwa 2-1 nyumbani na baadaye 2-0 ugenini.
Naamini, kama Ulimwengu
angeshiriki mechi zote mbili dhidi ya Nigeria, timu yetu ingekuwa na uhai zaidi-
lakini kukosekana kwake, kumetusababisha siyo tu tumetolewa, bali tumetupwa nje
ya mashindano kinyonge mno.
Lakini kabla ya
kuwahukumu Mazembe, tunapaswa kutafuta sababu juu ya kilichosababisha ghafla
mabingwa hao wa zamani Afrika wakapuuza wito wa TFF kutuma wachezaji Dar es
Salaam.
Mara kadhaa nimekuwa
nikiwaona makcha wa nchi jirani, ambazo wachezaji wake wanacheza hapa Tanzania
wakija nchini kuwafuatilia wachezaji wao, mfano Mserbia Milutin Sredojevic ‘Micho’
wa Rwanda au Msoctland, Bobby Williamson wa Uganda.
Wanapokuwa hapa
hujionea wachezaji wao namna wanavyocheza na kufanya uteuzi kwa ajili ya timu
taifa, juu ya wachezaji ambao wanawajua fika. Micho anakwenda hatua kadhaa
zaidi, anawahangaikia wachezaji wa Rwanda kupata timu Ulaya, au nchi nyingine
Afrika, ambako watakusanya uzoefu zaidi na baadaye kuisaidia Amavubi.
![]() |
| Ulimwengu |
Lakini sijawahi kusikia
hata siku moja kocha wa timu ya taifa si Kim Poulsen, tangu Mdenmark mwingine, Jan
Poulsen aliyemrithi Marcio Maximo kutoka Brazil akisafiri kwenda DRC
kuwafuatilia Samatta na Ulimwengu, ama Kenya ambako katika Ligi Kuu tuna mtu
anaitwa Idrisa Rajab au Angola ambako tuna mtu anaitwa Said Maulid.
Huwezi kuniambia eti
leo SMG ana uzee wa kutekelezwa moja kwa moja timu ya taifa bila kuzingatia
uwezo wake unaomuweka katika moja ya ligi kubwa Afrika, Girabola, wakati mwaka
2000 mchezaji huyo akisajiliwa Simba SC kutoka Kigoma, Shaaban Nditi alikuwa
anacheza Singida United Ligi Kuu na akina Kipanya Malapa na Edward Rodgers
Kayoza.
Wakati fulani, Jan
Poulsen alikwenda Sweden kumfuatilia Athumani Machuppa, kwa kuwa ni pua na
mdomo na Denmark- lakini zaidi makocha wa Taifa Stars wamekuwa na desturi ya
kusubiri sifa za wachezaji kupitia vyombo vya habari ndipo wawaite, ndio maana historia
inamtaja Amy Ninje kama mmoja wa wachezaji wa zamani wa Taifa Stars.
Baada ya mechi ya
kwanza dhidi ya Nigeria, Flying Eagles, kocha wa Ngorongoro Heroes, Mdenmark
Jakob Michelsen alisema kwamba ataongeza nguvu katika kikosi chake kwa kumuita kiungo
Adam Nditi wa Chelsea ya vijana ya England, ambaye tayari ameingia kwenye programu
za kukomazwa kwenye kikosi cha wakubwa cha mabingwa hao wa Ulaya.
Sijui jitihada gani za
dhati zilifanyika- lakini nachokiona hapa kocha anatakiwa kusafiri hadi London
na kufika Stamford Bridge kukutana na makocha wa Nditi kuzungumza nao kuhusu
huyo mchezaji na kuzungumza naye mchezaji mwenyewe pia, kuliko kuzungumza
kwenye vyombo vya habari.
![]() |
| Samatta akikabiliana na Kolo Toure wa Ivory Coast |
TFF inapaswa kumpa
fungu hata Kim akafuatilie na kujua kuhusu Nditi kama yupo kwenye nafasi ya
kuchezea Tanzania, kulikoni kuamua kwa kudhani tukiwa hapa nyumbani.
Kama sakata la Mazembe.
TFF inataka kupeleka malalamiko CAF, lakini imekwishazungumza kwa kina na
uongozi wa klabu hiyo ili kujua tatizo ni nini? Au inataka kutumia mabavu tu
kwa sababu kanuni za FIFA zinasema klabu lazima ziwaruhusu wachezaji kuchezea
timu zao za taifa?
Nauliza hivyo, kwa
sababu miezi miwili iliyopita nilifanya mahojiano na Makamu wa Rais wa Tout
Puissant Mazembe, Mohamed Kamwanya ambaye alisema kwamba Ulimwengu anachelewa
kuingizwa kwenye kikosi cha kwanza cha klabu hiyo, kwa sababu kiwango chake
bado kidogo.
Alisema kwamba,
Ulimwengu kila anapopewa ruhusa ya kurejea Tanzania kujiunga na timu za taifa,
kwanza huchelewa kurudi Lubumbashi na pia hurudi akiwa hayuko fiti.
“Hicho ndio
kinamchelewesha, lakini kama siyo hivyo angekuwa anacheza tu kama mwenzake. Na
nyinyi watu wa vyombo vya habari mtusaidie, kwa sababu wachezaji wakija huko
wanafanya anasa, wanarudi huku hawako fiti, sasa inakuwa mbaya,”alisema
Kamwanya.
Akiwa anaingia msimu wa
pili tangu asajiliwe na Mazembe, lakini Ulimwengu bado yupo kwenye kikosi cha
wachezaji wa akiba wa timu hiyo na hachezi Ligi Kuu wala Ligi ya Mabingwa, kama
mwenzake Mbwana Ally Samatta ambaye anang’ara.
Mimi najua kama Ulimwengu
anapotoka kambini ama Ngorongoro au Taifa Stars, hubaki Dar es Salaam kwa zaidi
ya wiki moja au zaidi akijirusha na kuna mtu aliwahi kunisumulia ‘balaa lake’,
nilikoma mwenyewe. Bado kijana mdogo, bado hajajitambua kwa sababu yeye ni
Mtanzania kama wachezaji wengine waliomtangulia akina Athumani China, Edibily Lunyamila
na wengineo.
Kuhusu Samatta, alisema
huyo anaendelea vizuri na hawana tatizo naye. Lakini Samatta huyu huyu, kuna
wakati Jan Poulsen alimtema timu ya taifa baada ya kutoridhishwa na kiwango chake
na kipindi ambacho alimfungia vioo kilimsaidia mchezaji huyo siyo tu kujihakikishia
namba ya kudumu kwenye kikosi cha kwanza cha Mazembe mbele ya washambuliaji
hodari kama Given Singuluma na Tressor Mputu Mabi, bali pia kupandisha kiwango
chake.
Naona TFF na makocha wa
timu za taifa, wana wajibu wa kufuatilia maendeleo ya wachezaji. Kwa sasa
wachezaji wa nje, ambao wanategemewa timu za taifa ni wawili, tu hao wa TPM-
sioni ugumu wa kutengeneza mawasiliano na uongozi wa klabu hiyo, ikiwa
kitaasisi kidogo tu (bongostaz.blogspot.com) kinaweza kuwasiliana na uongozi wa
juu wa klabu hiyo.
Sioni sababu ya kuingia
kwenye mgogoro na Mazembe ambao wanatulelea vijana wetu vizuri na wanaendelea
vizuri kwa matumaini makubwa. Naona, vema TFF ifanye mazungumzo na uongozi wa
Mazembe, kutatua suala hili kuliko kufikiria kwanza kuanza kushitakiana CAF na
FIFA. Nawatakia mfungo mwema wa mwezi mtukufu wa Ramadhan katika siku hizi za
ukingoni. Wasalam.





.png)
0 comments:
Post a Comment