![]() |
Mwesigwa |
Na Mahmoud Zubeiry
KLABU za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara zinataka kukutana
haraka, kujadili kile wanachodai, kitendo cha Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),
kuingia mkataba mpya na wadhamini wa ligi hiyo, Vodacom Tanzania bila
kuzishirikisha klabu, BIN ZUBEIRY imeambiwa.
Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa klabu Tanzania, Celestine
Mwesigwa amesema leo katika mahojiano na BIN ZUBEIRY kwamba, kuelekea msimu mpya
wa Ligi Kuu kuna sintofahamu nyingi kutoka ndani ya TFF, likiwemo suala la
udhamini.
“Tupo katika mchakato wa kukutana klabu zote za Ligi Kuu
kujadili mambo mbalimbali juu ya maslahi yetu, kubwa ni suala la udhamini,
haiwezekani TFF iingie mkataba wa udhamini na Vodacom bila kutushirikisha,”alisema
Mwesigwa.
Lakini BIN ZUBEIRY, ilipowasiliana na
Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, ambaye ni mwakilishi wa klabu ndani ya
shirikisho hilo, Wallace Karia alisema kwamba bado shirikisho hilo halijaingia
mkataba mpya wa udhamini wa Ligi Kuu, bali mazungumzo yanaendelea.
“Nimesikia watakamilisha Agosti 31, na Mkurugenzi Mtendaji
wa Vodacom alimpigia simu rais wa TFF (Leodegar Tenga) akimuita kwenye kikao
cha kujadili hilo suala, Tenga akaamua ili kuepusha maneno aende na Mzee Said
Mohamed wa Azam, sasa waliyozungumza huko jana ndio bado sijayajua,”alisema
Karia.
Aidha, Karia aliwashutumu Yanga kwamba ndio wanakwamisha
kikao cha klabu za Ligi Kuu kujadili mambo mbalimbali, kutokana na kupiga
chenga kila wakiambiwa.
Mkutano Mkuu uliopita wa TFF, uliamua kuanzia msimu ujao
Ligi Kuu iendeshwe na kampuni, itakayoundwa na Klabu za ligi hiyo.
0 comments:
Post a Comment