• HABARI MPYA

    Wednesday, September 05, 2012

    UNAMKUMBUKA PATRICK MBOMA, JENERALI MCHANA NYAVU?



    KWA mashabiki wa soka duniani kote, amezoeleka zaidi kwa jina la Patrick Mboma, ingawa jina lake halisi ni Henri Patrick Mboma Dem.
    Ni kati ya wachezaji ambao Afrika ina kila sababu ya kujivunia vipaji vyake na ingawa kwa sasa ametundika daluga, bado mambo yake ni mazuri, wakati huo akicheza soka ya ushindani yameendelea kuvuta hisia za wengi.
    Kwa sasa Mboma ni balozi maalumu wa Japan, nchi ambayo inatarajia kumtumia mchezaji huyo kutoka nchini Cameroon katika kuhakikisha inafanikisha juhudi za kuwa mwenyeji wa Kombe la Dunia 1922.
    Wakati akicheza soka ya ushindani, Mboma mbali na kutamba akiwa na timu ya Taifa ya Cameroon, lakini pia amezichezea klabu kadhaa barani Ulaya, zikiwamo klabu tatu maarufu za Japan katika Ligi Kuu ya nchini humo, maarufu J.League.
    Mboma, aliyezaliwa Novemba 15, 1970 katika mji wa Douala nchini Cameroon, kipaji chake cha soka kilianza kuonekana mbele ya wengi mwaka 1993 na kama ilivyo ada kwa wanasoka wa Afrika, baada ya kufanya vizuri nyumbani alianza harakati za kusaka ulaji barani Ulaya.
    Harakati hizo zilimwezesha kutua nchini Ufaransa, ambako akiwa huko aliweza kutamba na timu ya Chateauroux, ambayo ilitosha kumfanya adhihirishe uwezo wake wa kuzifumania nyavu, kwani katika mechi 48 alizocheza alifunga mabao 22.
    Baada ya hapo, Mboma alijiunga na Paris Saint-Germain mwaka 1994, lakini alishindwa kuonyesha makali aliyoyadhihirisha wakati akiichezea Châteauroux, hali iliyomfanya adumu na timu hiyo kwa msimu mmoja tu.
    Mambo yalipokwenda kombo, alijiunga na FC Metz, ambako alionekana kuzitumia vyema mechi chache alizocheza kwa kudhihirisha umakini na umahiri wake wa kuzifumania nyavu, hali iliyowashawishi viongozi wa Paris Saint-Germain kuamua kumchukua kwa mara ya pili mwaka 1996.
    Katika kilichoonekana kama kuwa na mikosi na timu hiyo, mambo yalionekana kwenda kombo kwa Mboma, kwani alishindwa kabisa kuonyesha umakini wa kuzifumania nyavu na katika mechi nane alizocheza, alifunga bao moja tu.
    Huo ukawa mwisho wa Mboma na klabu za Ufaransa, kwani baada ya hapo, alitimkia bara la Asia na kutua katika klabu ya Gamba Osaka mwaka 1997, ambako walau alianza kuibua upya makali yake ya kuzifumania nyavu.
    Aliifungia timu hiyo mabao 29 katika mechi 34, rekodi ambayo ilionekana kutoa picha nzuri kwa mshambuliaji huyo, lakini zaidi ya hilo kiwango chake cha soka pia kilikuwa kivutio kwa wengi.
    Haikushangaza alipotimkia nchini Italia mwaka 1998 na kujiunga na klabu ya Cagliari, kabla ya kuihama timu hiyo mwaka 2000 na kujiunga na klabu nyingine nchini humo ya Parma, ambayo aliichezea kwa msimu mmoja.
    Aliihama Parma mwaka 2001, baada ya kuifungia mabao matano katika mechi 24 na wakati ikiaminika kuwa makali yake yameanza kupungua katika soka ya kulipwa, Mboma alitimkia England na kujiunga na klabu ya Sunderland mwaka 2002.
    Hatua hiyo ambayo ilipokelewa kwa mtazamo tofauti mbele ya mashabiki na wachambuzi wa soka, baadhi wakiamini amefika mwisho na wengine wakiamini anatafuta makali, mwishowe kila kitu kilidhihirika, baada ya kufunga bao moja tu katika mechi tisa.
    Katika kilichotoa dalili kwamba Mboma alikuwa akielekea ukingoni, mwaka 2002 baada ya kuchemsha Sunderland alitimkia Afrika Kaskazini na kutua nchini Libya, ambako alijiunga na klabu ya Al-Ittihad ya huko.
    Akiwa na klabu hiyo bado hakuna lolote la maana alilolifanya katika kipindi cha mwaka 2002 na 2003, kwani hata kupata nafasi katika timu ilikuwa vigumu na hivyo aliishia kucheza mechi mbili tu na hakufunga hata bao moja.
    Wakati ikiaminika mbele ya wengi kwamba angeachana na soka ya kulipwa, bado Mboma hakuwa mchezaji wa kukata tamaa na badala yake, alirudi nchini Japan na kujiunga na klabu ya Tokyo Verdy, katika kilichoaminika kuwa ni kufufua upya kipaji chake.
    Akiwa na klabu hiyo, katika kipindi cha mwaka 2003 na 2004, kidogo Mboma alianza kuonyesha uhai kwa kuifungia mabao 17 katika mechi 35 na kuhamia klabu nyingine ya huko huko Japan ya Vissel Kobe, ambayo aliishia kuichezea mechi 10 na kufunga mabao mawili tu.
    Vissel Kobe ilikuwa klabu ya mwisho kwa Mboma, kwani Mei, 2005, alitangaza rasmi kustaafu soka ya kulipwa.
    Ukiachana na soka ya klabu, Mboma ni mmoja wa wachezaji waliotoa mchango mkubwa katika timu ya Taifa ya Cameroon, ambayo aliichezea kwa mara ya kwanza mwaka 1995 na hadi anastaafu kuichezea timu hiyo amecheza jumla ya mechi 57 na kufunga mabao 33.
    Ameiwakilisha Cameroon katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 1998 nchini Ufaransa na 2002 huko Japan na Korea Kusini na zaidi ya hayo, mwaka 2000 aliiwezesha Cameroon kutwaa medali ya dhahabu katika Michezo ya Olimpiki.
    Katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, Mboma ameiongoza vyema Cameroon kutwaa taji la michuano hiyo katika fainali za mwaka 2000 na 2002.
    Mboma ambaye pia anasifika kwa kufunga mabao kwa mashuti ya mbali, mwaka 2000 alitwaa tuzo ya mwanasoka bora wa Afrika na mwaka 2002 akawa mfungaji bora wa michuano ya Mataifa ya Afrika.
    Wakati hii leo akiwa ni mwanasoka mstaafu, mashabiki wanaendelea kumkumbuka Mboma kwa mambo mengi enzi zake akiwa katika soka ya ushindani na mojawapo ni staili yake ya kushangilia kama vile ameshika bastola mbili kwa mikono yake.

    WASIFU WAKE:
    JINA: Henri Patrick Mboma Dem
    KUZALIWA: Novemba 15, 1970 (Miaka 40)
    ALIPOZALIWA: Douala, Cameroon
    KLABU ALIZOCHEZEA:
    Mwaka            Klabu
    1990–1992      Paris Saint-Germain (aliishia benchi)
    1992–1994      LB Châteauroux (Mechi 48, mabao 22)
    1994–1995      Paris Saint-Germain (Mechi 8, bao 1)
    1995–1996      FC Metz (Mechi 17, mabao 4)
    1996–1997      Paris Saint-Germain (Mechi 8, bao 1)
    1997–1998      Gamba Osaka (Mechi 34, mabao 29)
    1998–2000      Cagliari (Mechi 40, mabao 15)
    2000–2001      Parma (Mechi 24, mabao 5)
    2002                Sunderland (Mechi 9, bao 1)
    2002–2003      Al-Ittihad (Mechi 2, hakufunga)
    2003–2004      Tokyo Verdy 1969 (Mechi 35, mabao 17)
    2004–2005      Vissel Kobe (Mechi 10, mabao 2)
    (Tangu 1995 hadi 2004, aliichezea Cameroon mechi 56, ameifungia mabao 33)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UNAMKUMBUKA PATRICK MBOMA, JENERALI MCHANA NYAVU? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top