MICHUANO ya Copa Coca-Cola ngazi ya Taifa inaanza kutimua
vumbi Juni 24 mwaka huu kwenye mikoa ya Dar es Salaam na Pwani huku pambano la
ufunguzi likiwa kati ya Kigoma na Lindi litakalofanyika kwenye Uwanja wa
Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniphace
Wambura Mgoyo ameiambia leo BIN ZUBEIRY kwamba, upangaji ratiba
(draw) umefanyika leo (Juni 7 mwaka huu) kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) na kushuhudiwa na waandishi wa habari, makocha wa timu za
mikoa za Copa Coca-Cola na wadhamini kampuni ya vinywaji baridi ya Coca-Cola.
Amesema makocha 35 wa timu za Copa Coca-Cola kutoka mikoa
yote ya Tanzania Bara na Visiwani wako kwenye kozi ya Shirikisho la Kimataifa
la Mpira wa Miguu (FIFA) inayoendeshwa na wakufunzi Ulric Mathiot wa FIFA
kutoka Seychelles na wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), Sunday
Kayuni wa Tanzania.
Amesema mikoa 28 ya kimpira ya Tanzania itashiriki katika
mashindano hayo na imegawanywa katika makundi manne ya timu saba saba. Baadaye
timu zitapambana katika hatua ya robo fainali, nusu fainali na fainali
itakayofanyika Julai 15 mwaka huu.
Amesema Kundi A lina timu za Arusha, Ilala, Kigoma, Kusini
Pemba, Lindi, Rukwa na Ruvuma. Kundi B ni Iringa, Kaskazini Pemba, Manyara,
Mjini Magharibi, Morogoro, Mwanza na Tanga. Dodoma, Kaskazini Unguja,
Kinondoni, Mara, Mbeya, Mtwara na Temeke ziko kundi C wakati kundi D ni Kagera,
Kilimanjaro, Kusini Unguja, Pwani, Shinyanga, Singida na Tabora.
“Viwanja vitakavyotumika katika mashindano hayo ambapo mechi
zitakuwa zikichezwa asubuhi (saa 2.30) na jioni (saa 10.00) ni Uwanja wa Karume
na Tanganyika Packers (Kawe) kwa Dar es Salaam. Viwanja vya Mkoa wa Pwani ni
Tamco na Nyumbu. Timu zote katika mashindano hayo zitacheza katika viwanja
hivyo,”amesema.
Wambura pia amesema mbali ya Kigoma na Lindi, mechi nyingine
za ufunguzi Juni 24 mwaka huu ni kundi B Morogoro na Manyara (saa 2.30 asubuhi
Uwanja wa Kawe), kundi C ni Temeke na Kinondoni (saa 2.30 asubuhi Uwanja wa
Nyumbu) na kundi D ni Kilimanjaro na Kusini Unguja (saa 2.30 asubuhi Uwanja wa
Tamco).
Amesema wachezaji wanaotakiwa kushiriki kwenye michuano hiyo
ya umri chini ya miaka 17 ni wale waliozaliwa kuanzia Januari 1, 1996
0 comments:
Post a Comment