![]() |
Rais wa TFF, Leodegar Chillah Tenga kulia, akizungumza na Waandishi wa Habari leo ofisi za shirikisho hilo, Ilala, Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu wake, Angetile Osiah akiandika hadidu za rejea. |
RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Chillah
Tenga amemwagia sifa kocha wa sasa wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa
Stars, Mdenmark Kim Polulsen kwamba ni mtu wa kazi na hajui anasa.
Akizungumza na Waandishi wa Habari katika ofisi za TFF,
Ilala, Dar es Salaam mchana wa leo, Tenga alisema kwamba Kim akitoka nyumbani
kwake amekwenda sokoni au kazini na hajui baa wala sehemu za starehe.
Tenga amesema wana matumaini makubwa sana na Poulsen kwamba
ataifikisha mbali soka ya Tanzania, kwa sababu hata timu yake ya sasa inaundwa
na asilimia kubwa ya vijana walio na wastani wa umri wa miaka 23 na kwamba hata
wakubwa wachache, rika la akina Juma Kaseja na Haruna Moshi ‘Boban’ wana miaka
isiyozidi 27.
Tenga amempongeza Kim na vijana wake kwa ushindi wa mabao
2-1 dhidi ya Gambia, Jumapili katika mchezo wa kuwania tiketi ya kucheza
Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014 nchini Brazil na ameomba timu hiyo iungwe
mkono zaidi ili ifike mbali.
“Tumefika hapa baada ya jitihada kubwa, ikiwemo kubadilisha
kocha. Kupambana na nidhamu, tulimuambia mwalimu, tafadhali, hakikisha nidhamu,
utendaji na jitihada za mazoezi, usiogope mchezaji, ita mchezaji, nampongeza
sana na hakuna jambo la ajabu kwa sababu tunamjua Kim, ni mtu wa kazi, mwaka
mzima”alisema Tenga.
Tenga amesema kwamba tangu amewasili Kim Tanzania mwaka jana
alianzisha programu nzuri ya vijana ambao amekuwa akiwakusanya kila mwezi na kuwanoa-
jambo ambalo limesababisha hivi sasa awe na timu nzuri ya taifa, baada ya
kupandishwa kutoka kocha wa timu za vijana, hadi ya wakubwa, akirithi mikoba ya
Mdenmark mwenzake, Jan Poulsen.
“Wale vijana Sure Boy (Salum Abubakar) na Damayo (Frank) wamecheza
pamoja karibu mwaka mzima timu ya vijana chini ya Kim na wanaelewana sana. Sasa
tumekwishaanza kuandaa utaratibu wa kuwapatia vijana wataalamu wa saikolojia,
ili wawafundishe mambo, namna ya kuzungumza na Waandishi wa Habari, kuweza
kujiami na kadhalika.
“Na tumeboresha maslahi yao, wakishinda mechi wanapata
asilimia 15 ya mapato, wakitoa sare asilimia tano, ila wakifungwa hawapati
kitu. Tutawakatia bima pia, mambo yatakuwa mazuri,”alisema Tenga.
Taifa Stars hivi sasa inashika nafasi ya pili katika Kundi
C, kwa pointi zake tatu, mabao mawili ya kufunga na matatu ya kufungwa, nyuma
Ivory Coast inayoongoza kwa pointi zake nne, mabao manne ya kufunga na mawili
ya kufungwa, wakati Morocco inashika nafasi ya tatu kwa pointi zake mbili,
mabao matatu ya kufunga na matatu ya kufungwa na Gambia yenye pointi moja,
mabao mawili ya kufunga na matatu ya kufungwa inashika mkia.
Stars Jumapili itahamishia mawindo yake katika kinyang’anyiro
cha tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwakani Afrika
Kusini kwa kumenyana na Msumbiji mjini Maputo na inatarajiwa kuondoka nchini
Ijumaa. Katika mchezo wa kwanza, timu hizo zilitoka sare ya 1-1 Dar es Salaam
na Stars inatakiwa lazima kushinda ugenini ili kuitoa Mambas na kusonga mbele.
0 comments:
Post a Comment