Ilikuwa bahati mbaya, kijana ameomba radhi |
Na Mahmoud Zubeiry
KIUNGO wa
Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ amewaomba radhi wapenzi wa soka Tanzania kwa
kitendo chake cha kumchezea rafu mbaya mchezaji mwenzake wa timu ya taifa ya
Tanzania, Taifa Stars, Kevin Yonda jana. Akizungumza na BIN ZUBEIRY leo, Boban
alisema kwamba wengi wanaweza kudhani alikusudia, lakini ukweli hadi anafika
kwa Yondan hakuwa na dhamira ile. “Nia yangu ilikuwa kuukita mpira, lakini
Yondan naye fundi, akautuliza ukahama, na mimi wakati huo nishauinua mguu wangu
ndio unatua sasa, ukatua kwenye mguu wake.
Binafsi iliniumiza
sana na kama utaona kuanzia pale sikucheza vizuri kabisa, sikuwa na raha
kabisa. Yondan ni rafiki yangu sana, nimempokea Simba, nimeondoka nimemuacha,
nimerudi, amenipokea, tumeishi vizuri, kwa kweli inaniumiza sana,”alisema
Boban.
Aidha, Boban
alisema kwamba atakwenda kumjulia hali Yondan na kumuomba msamaha. “Nawaomba
msamaha zaidi mashabiki wa Yanga, mimi ni binadamu, wanisamahe,”alisema Boban.
Yondan atakuwa
nje kwa wiki mbili, kutokana na kuumizwa na kiungo huyo wa Simba, katika mchezo
wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Daktari wa
Yanga, Sufiani Juma ameiambia BIN ZUBEIRY kwamba beki huyo tegemeo
wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, tangu jana alikuwa anasikia
maumivu makali na baada ya kufanyiwa vipimo katika Kitengo cha Mifupa cha
Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili (MOI), imeelezwa anatakiwa kupumzika wiki mbili.
Lakini Yondan
pia anaweza kukaa nje ya Uwanja kwa zaidi ya muda, huo kwani majibu hayo
yanatokana na uchunguzi wa awali.
Yondan aliumizwa
jana wakati Yanga ikitoka nyuma na kulazimisha sare ya kufungana bao 1-1 na
wapinzani wao wa jadi, Simba SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania
Bara, uliopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kuanzia saa 1:02 usiku.
Yanga ambao
walimaliza mechi hiyo wakiwa pungufu baada ya Simon Msuva kutolewa nje kwa kadi
nyekundu dakika ya 77 kwa kumrudishia rafu Juma Nyosso, ndio waliohaha
kusawazisha bao, baada ya kutanguliwa kwa bao la mapema la kiungo Amri
Kiemba.
Hadi
mapumziko Simba walikuwa tayari mbele kwa bao 1-0, lililotiwa kimiani na kiungo
Amri Kiemba dakika ya pili, wakati Yanga ilisawazisha dakika ya 63, baada ya beki
Paul Ngalema kuunawa mpira katika harakati za kuokoa na refa Mathew Akrama
akaamuru penalti, ambayo ilikwamisha kimiani kiufundi na Said Bahanuzi ‘Spider
Man’.
Katika
dakika ya 77 Mathew Amkrama alimtoa nje kwa kadi nyekundu ya moja kwa moja
Simon Msuva, baada ya kumkita Juma Nyosso, aliyemkanyaga ‘kwa bahati mbaya’.
Msuva alichezewa rafu na Nyosso na tayari refa alikwishapuliza filimbi na kumpa
kadi ya njano beki huyo wa Simba, lakini kiungo huyo wa Yanga akaponzwa na
hasira za kitoto.
0 comments:
Post a Comment