• HABARI MPYA

    Saturday, May 12, 2012

    RAGE , KOCHA WALALA VARANDANI SUDAN, WANAKOMAJE HIVYO VISA!




    WAWAKILISHI wa Tanzania katika michuano ya Kombe Shirikisho, Simba wameendelea 'kuoga' manyanyaso na vitimbi vya kila aina toka kwa wenyeji wao Al Ahly Shandy, ambapo juzi baadhi ya watu kwenye msafara wa timu hiyo walilazimika kulala chumba cha mapokezi kufuatia kukosa vyumba kwenye hosteli waliyofikia.
    Gazeti la Mwananchi leo, limeandika kwamba miongoni mwa walioadhibiwa na vitimbi hivyo ni pamoja na Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage na kocha Msaidizi wa makipa, James Kisaka ambao baada ya kukosa vyumba walilazimika kulala kwenye makochi ya chumba cha mapokezi.
    Viongozi wengine wa Simba, Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Swedy Mkwabi na kiongozi wa msafara, Hussein Mwamba ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, pia walikosa sehemu ya kulala na hivyo wakalazimika kwenda kulala nje ya hosteli hiyo ya Shendi.
    Mbali na kufanyiwa vitimbi hivyo, pia Wekundu hao wa Msimbazi walilazwa kwenye hosteli badala ya hoteli hatua iliyopelekea kugoma na kutishia kurudi mjini Khartoum licha ya umbali wa zaidi ya kilomita 200 kwa gari kupitia barabara yenye jangwa kubwa na lisilo na makazi ya watu.
    "Hatuwezi kulala hapa, hii siyo hotel, ni hosteli na kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) haikidhi viwango", alilalama mwenyekiti wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage.
    Kwa mujibu wa kanuni ya CAF kifungu cha 7 (c), timu mwenyeji inatakiwa kuhakikisha kuwa timu mgeni inaishi katika hoteli ya daraja la kwanza na pia msafara mzima unakaa katika hoteli moja.
    Rage na viongozi wengine akiwemo mkuu wa msafara ambaye ni mjumbe wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Mwamba waliifanyia ukaguzi hosteli hiyo na kujiridhisha kuwa haikuwa na viwango.
    Akizungumzia hali hiyo, mwakilishi wa timu ya Shendi, Hamdy Ibn Hossein, alisema inatokana na ukweli kuwa mji wao ni mdogo na hakuna hoteli nyingine kubwa kuliko hiyo mji mzima.
    Hata hivyo, baada ya majadiliano kwa pamoja, Simba iliamua timu ilale kwa hofu ya kuendelea kuwachosha wachezaji.
    Hata hivyo, uongozi wa Simba unakusudia kuwasilisha malalamiko rasmi kwa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kutokana na unyama inaofanyiwa nchini Sudan inakosubiri pambano lake dhidi ya Al Ahly Shendi kesho.
    Tangu iwasili nchini Sudan juzi, Simba imekuwa ikifanyiwa vitendo visivyo vya kiungwana na wenyeji wake, Shirikisho la Soka Sudan (SAF) na Al Ahly Shendi.
    Jana, Simba ilifanyiwa vitendo hivyo kabla ya kwenda katika mji wa Shendi itakakochezwa mechi hiyo na baada ya kufika katika mji huo uliopo takribani kilomita 170 kutoka mji mkuu Khartoum.
    Simba pia itapeleka malalamiko kutokana na kuwekwa kwenye hosteli inayofanana na mabweni ya wanafunzi na imepewa vitanda 24 tu, huku msafara ukiwa na watu takribani 30.
    Wakati ilipokuja Tanzania, Simba ililipia gharama za watu 30 wa timu hiyo na kulikuwa na makubaliano kwamba na wao watafanya hivyo wakati Wekundu watakapokwenda Sudan
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RAGE , KOCHA WALALA VARANDANI SUDAN, WANAKOMAJE HIVYO VISA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top