• HABARI MPYA

    Tuesday, May 08, 2012

    WAZEE YANGA 'WAMESHIKIA UDHU NAJISI'


    Katibu wa Baraza la Wazee wa Yanga, Mzee Ibrahim Ally Akilimali katikati

    WAZEE wa klabu ya Yanga na wanachama maarufu kwa migogoro, wakiongozwa na Mzee Ibrahim Ally Akilimali na Bakili Makele, leo wameibuka wakimpiga mkwara Mwenyekiti wa klabu hiyo, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga, asithubutu kufukuza mchezaji yeyote, bali aondoke yeye.
    Nchunga alikaririwa jana akisema kipigo cha mabao 5-0 kutoka kwa wapinzani wao wa jadi, Simba Jumapili kilitokana na hujuma iliyofanywa na wana Yanga wenzao- kiasi kwamba akaustaajabu u-Yanga wana wana Yanga hao.
    Nilifurahishwa na kauli ya jemedari wa migogoro, Bakili, akisema kwamba Nchunga asifukuze mchezaji yeyote kwa sababu, hii si mara ya kwanza Yanga kufungwa tano.
    Ukifuatilia historia ya mechi hii, kabla haijachezwa, kauli za wazee hao kabla ya mechi na sasa baada ya mechi unaweza kupata picha fulani, kwamba Nchunga yuko sahihi kusema kuna hujuma.
    Wazee hawa walisema kabla ya mechi, hata Yanga ikiifunga Simba, lazima Nchunga aondoke. Walisema hivyo kwa sababu wanajua Nchunga amekuwa na rekodi nzuri ya kuifunga Simba na kutwaa mataji makubwa, likiwemo Kombe la Kagame, ambalo mara ya mwisho klabu ililitwaa mwaka 1999.
    Lakini kusema; Hata akiifunga SImba, lazima aondoke- maana yake nini?
    Walitengeneza mazingira ya timu kufungwa ili kuhalalisha safari ya Nchunga? Kama hivyo ndivyo wamefanikiwa- lakini nataka kuwaambia wazee hao na wote walioko nyuma yao kwamba, wameshika udhu kwa najisi.
    Najisi ni nini?  Ni uchafu unaomfanya muumini wa dini ya kiislamu apoteze udhu- kiasi kwamba hata ibada yake haiwezi kuswihi.
    Kwa mfano, maji masafi, lakini kumbe mtu aliyakojolea, japo tone dogo tu la mkojo, likazidiwa na maji- ila hayo maji mfuate Mufti kamuulize yanaswihi kushikia udhu? Atakuambia hapana usithubutu.
    Sasa wazee wa Yanga wameshika udhu kwa najisi. Je, ni safi hao?
    Lengo ni kumng’oa Nchunga. Sadakta. Lakini kitendo cha kufanya jitihada zozote, bila kujali maslahi ya klabu yao, ili mradi tu wamuondoe Nchunga klabuni ni kosa kubwa.
    Naamini dhambi hii, itawatafuna wahusika- kama historia haitafutika, Yanga ilifungwa 5-0, Mei 6, 2012.
    Kitendo cha uongozi wa Yanga, chini ya Mwenyekiti wake Nchunga kuthubutu kumtumia beki Nadir Haroub Cannavaro katika mechi na Coastal Union ya Tanga, kilikuwa kinatosha kabisa kama sababu ya kuwawajibisha viongozi katika Mkutano Mkuu.
    Lakini kwa sababu hawakuwa wenye kujiamini kama wanweza kuwa na hoja za kupambana naye kwenye mkutano Mkuu, wakaona waongeze sababu. 5-0.
    5-0 hajafungwa Nchunga, imefungwa Yanga. Wajukuu wa Bakili wakikua wataikuta historia hiyo.
    Siku hizi kuna Yanga maslahi, na Yanga damu na huu ndio wakati mwafaka kuanza kuwachanganua yupi ni yupi.
    Bakili anasema Nchunga asifukuze mchezaji kwa sababu hii si mara ya kwanza Yanga kufungwa 5-0.
    Popote alipo Bakili ajiulize hatua gani ilichukuliwa na Yanga, chini ya Mwenyekiti wake Jabir Idrisa Katundu Julai 2, mwaka 1994, baada ya Yanga kufungwa 4-1 na Simba?
    Kama hajui nitamkumbusha, walifukuzwa wachezaji karibu wote, wakabaki wachache tu kama Kenneth Mkapa, Constantine Kimanda, Sekilojo Chambua, Sanifu Lazaro ‘Tingisha’ na Mohammed Hussein ‘Mmachinga’, wengine wote walitimuliwa kwa tuhuma za hujuma.
    Baada ya hapo, Yanga iliundwa na wachezaji waliokuwa wakiandaliwa na Tambwe Leya (sasa marehemu) katika kikosi cha pili, ambao ni pamoja na Godwin Mashoto (sasa marehemu), Mzee Abdallah, Anwar Awadh, Maalim Saleh ‘Romario’, Nonda Shaaban na wengineo, waliosajiliwa kutoka timu mbalimbali kuimarisha kikosi kama Bakari Malima, Reuben Mgaza waliotoka Pan African.
    Sasa iweje leo Bakili anazungumza tena nyumbani kwa Mzee Katundu aliyekuwa Mwenyekiti wa Yanga wakati wa 4-1 akimzuia Nchunga kufukuza wachezaji wasio waaminifu?
    Na kwa nini sasa akina Bakili awatetee wachezaji? Inatia shaka. Lakini mimi nawashangaa wana Yanga wa leo, wanaokubali kuibeba fedheha hii kwa urahisi tu.
    Inasikitisha, Yanga imefikia hapa- na kwa mtaji huu daima wataendelea kukodolea macho mafanikio ya Simba. Na baada ya muda mrefu wa kuizungumzia 6-0 kama kipigo cha kihistoria, inapoelekea Yanga vipigo kama hivyo, vitakuwa vya kawaida.
    Kumkubali au kumkataa kiongozi ni demokrasia, lakini tena inafikia hadi watu wanahujumu timu zao wenyewe? Hapa ilipofikia sasa tukae mkao wa kula, maana huwezi jua baada ya hili lingine lipi litafuata.
    Zamani wazee wetu walikuwa wanasema mtoto akikunyea mkononoi, hauukati, unausafisha, lakini wazee wa leo wa Yanga wanachoma moto nyumba yao, kisa adui kaingia. Nani anapoteza? Nachoweza kusema tu, wazee wa Yanga wameshikia udhu najisi. Alamsiki!
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAZEE YANGA 'WAMESHIKIA UDHU NAJISI' Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top