• HABARI MPYA

    Wednesday, June 20, 2012

    MAZOEZI YA SIMBA YASUASUA, WACHEZAJI ZAIDI BADO KUJITOKEZA


    Wachezaji wa Simba waliokuwa mazoezini juzi
    Na Prince Akbar
    HADI sasa kwenye Uwanja wa TCC Chango’ombe, Dar es Salaam ambako mabingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Simba SC wanaendelea na mazoezi kujiandaa na Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, hakuna mchezaji aliyeongozeka kutoka idadi ya juzi, wachezaji 13.
    Kwa mujibu wa Daktari wa Simba SC, Cossmas Kapinga ambaye muda huu tayari yuko maezoini TCC, wachezaji waliokuwa na timu ya taifa nchini Msumbiji na wengine wapya, akiwemo Danny Mrwanda bado hawajafika.
    Kwa maana hiyo, Kiggi Makassy aliyesajiliwa kutoka Yanga ndiye anaendelea kuwa mchezaji ‘lulu’ kwenye mazoezi hayo.
    Juzi BIN ZUBEIRY ilitembelea mazoezi ya Simba TCC na kukuta wachezaji 13 wakijifua chini ya Kocha Msaidizi, Mganda Hamatre Richard, akiwemo Kiggi Makassy ingawa mshambuliaji aliyesajiliwa kutoka Dong Tam Long An ya Vietnam, Danny Davis Mrwanda hakutokea.
    Mashabiki wengi wa Simba walifika mapema Uwanja wa TCC Chang’ombe, Dar es Salaam kuwashuhudia wachezaji wao, kiu zaidi ikiwa kumuona mpachika mabao wao wa zamani, aliyerejea kikosini Mrwanda, lakini Meneja wa Simba, Nico Nyagawa akaiambia BIN ZUBEIRY kwamba mchezaji huyo ni miongoni mwa waliotoa udhuru.
    Waliohudhuria ni pamoja na Salim Kinje, Abdalllah Juma, William Mweta, Hamadi Waziri, Abuu Hashim, Haroun Athumani, Haruna Shamte, Amri Kiemba, Paul Ngalema, Uhuru Suleiman, Patrick Kanu Mbivayanga na Abdallah Seseme.
    Mazoezi hayo yaliongozwa na Richard kwa sababu Kocha Mkuu, Mserbia Milovan Cirkovick bado anakula sikukuu kwao.
    Simba itaendelea na program ya mazoezi kwa jioni tu wiki hii na Nyagawa amesema anatarajia idadi ya wachezaji itakuwa ikiongezeka taratibu wiki hii, wakiwemo wachezaji waliokuwa na timu ya taifa Msumbiji nao pia wanatarajiwa kuungana na wenzao wakirejea kutoka nchini humo.    
    Mrwanda ambaye amesaini mkataba wa mwaka mmoja wa kuichezea Simba, ambao hauna kipengele cha kumruhusu kuuvunja kabla haujamalizika naye anatarajiwa kuanza maozezi wakati wowote wiki hii.
    Mrwanda, awali ilielezwa anataka kusaini mkataba ambao wakati wowote akipata timu nje, aondoke, lakini kwa mujibu wa mkataba aliosaini Simba ni kwamba akipata timu italazimika kumnunua kutoka kwa Wekundu wa Msimbazi, au isubiri hadi amalize mkataba.
    Habari za uhakika, kutoka ndani ya Simba SC ambazo BIN ZUBEIRY imezipata, zimesema kwamba Mrwanda ameridhika na mkataba huo na ameahidi kufanya vitu baab kubwa Msimbazi.
    Kwa upande mwingine, Simba SC imeamua kumtema kiungo Salum Machaku kwa makubaliano maalum ya pande zote mbili ya kuvunja mkataba. Simba ilitaka kumtoa kwa mkopo Machaku, lakini mwenyewe akasema bora aachwe moja kwa moja.
    Tayari Simba imemsajili kiungo wa Yanga, Kiggi Makassy kuziba nafasi ya Machaku. Machaku sasa ameingia kwenye mazungumzo na Yanga.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAZOEZI YA SIMBA YASUASUA, WACHEZAJI ZAIDI BADO KUJITOKEZA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top