• HABARI MPYA

    Friday, October 05, 2012

    SERENGETI BOYS KUCHEZA NA YANGA B KESHO KARUME

    Kocha wa Yanga B, Salvatory Edward na Msaidizi wake, Abubakar Salum nyuma, wakiwapa maelekezo wachezaji wao juzi.

    Na Prince Akbar
    TIMU ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys ambayo imefuzu kucheza raundi ya Tatu na ya mwisho katika michuano ya kutafuta tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Vijana wa umri huo, baada ya Misri kujitoa kesho itacheza na U20 ya Yanga kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam kuanzia saa 10.30 jioni katika mechi maalum ya kuvunjia kambi, ambayo kiingilio kitakuwa sh. 2,000.
    Yanga B, inayofundishwa na Salvatory Edward, juzi ilicheza soka ya kuvutia na kuwahenyesha mabingwa wa Kombe la BancABC Sup8R, Simba B kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa sare ya 2-2.
    Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniphace Wambura Mgoyo ameiambia BIN ZUBEIRY mida hii kwamba, Serengeti Boys ilikuwa icheze Raundi ya pili dhidi ya Misri; mchezo wa kwanza ukichezwa Oktoba 14 mwaka huu jijini Dar es Salaam na ule wa marudiano wiki mbili baadaye jijini Cairo, lakini wapinzani wao wamejitoa.
    Ikumbukwe, katika raundi ya kwanza pia, Serengeti Boys inayofundishwa na Jakob Michelsen kutoka Denmark ilipita bila jasho baada ya Kenya kujitoa mwezi uliopita na sasa njia inazidi kuwa nyeupe kwa timu hiyo kukata tiketi ya kucheza Fainali za U17 za Vijana zitakazopigwa mwakani nchini Morocco.
    Wambura alisema kwa matokeo hayo, sasa Serengeti Boys itacheza Raundi ya Tatu dhidi ya mshindi wa mechi kati ya Zimbabwe na Kongo Brazzaville, mechi ya kwanza ikichezwa Novemba 18 mwaka huu mjini Dar es Salaam na marudiano wiki mbili baadaye ugenini.
    Zimbabwe na Congo Brazzaville zitapambana zitapambana kati ya Oktoba 12-14 mwaka huu, Zimbabwe ikiwa mwenyeji wa mechi ya kwanza wakati ya marudiano itafanyika kati ya Oktoba 26-28 mwaka huu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS KUCHEZA NA YANGA B KESHO KARUME Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top