Basi la Yanga |
Na Mahmoud Zubeiry
BAADA ya
kulazimisha sare ya bila kufungana na wapinzani wao wa jadi, Simba SC Jumatano,
Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Yanga inatarajiwa kuondoka kesho alfajiri
kwenda Bukoba kwa ajili ya mchezo wake wa sita wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania
Bara, dhidi ya wenyeji Kagera Sugar Jumapili.
Yanga leo
itafanya mazoezi kwenye Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam na
baada ya hapo itakuwa tayari kwa safari ya Bukoba na Kanda ya Ziwa kwa ujumla,
kwani baada ya kucheza na Kagera, itacheza na Toto African mjini Mwanza.
Katika mechi
nne za awali ilizocheza, Yanga imefungwa moja, sare mbili na kushinda mbili,
hivyo kujikusanyia pointi nane, ikizidiwa pointi tano na wapinzani wao wa jadi,
Simba wanaoongoza ligi hiyo.
Jumatano Yanga
ilitoka sare ya kufungana bao 1-1 na wapinzani wao hao wa jadi, Simba katika
mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, uliopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam, kuanzia saa 1:02 usiku.
Yanga ambao
walimaliza mechi hiyo wakiwa pungufu baada ya Simon Msuva kutolewa nje kwa kadi
nyekundu dakika ya 77 kwa kumrudishia rafu Juma Nyosso, ndio waliohaha
kusawazisha bao, baada ya kutanguliwa kwa bao la mapema la kiungo Amri
Kiemba.
Hadi
mapumziko Simba walikuwa tayari mbele kwa bao 1-0, lililotiwa kimiani na kiungo
Amri Kiemba dakika ya pili.
Simba
walicheza vizuri kipindi chote cha kwanza wakigongeana pasi za uhakika na
kuwazidi kasi uwanjani wapinzani wao, wakati Yanga pamoja na kuzinduka baada ya
kufungwa bao, lakini makosa yalikuwa mengi.
Pasi zao
zilikuwa nyingi hazifiki, walikuwa wanapokonyeka mipira kirahisi, wanazidiwa
nguvu na wapinzani wao katika kugombea mipira na hata mashambulizi yao hayakuwa
ya mpangilio, zaidi ya kuonekana kubahatisha zaidi.
Katika
kubahatisha huko, Mbuyu Twite alifumua shuti zuri dakika ya 38 kutoka wingi ya
kulia, ambalo lilitoka nje sentimita chache.
Kabla hata
ya dakika 45 za kipindi cha kwanza kumalizika, kocha Mholanzi Ernie Brandts
alimtoa Hamisi Kiiza na kumuingiza Frank Domayo ili kuimarisha safu ya kiungo,
ambayo ilionekana kuzidiwa na Simba inayofundishwa na Mserbia, Milovan
Cirkovick.
Kipindi cha
pili, Yanga walianza na mabadiliko, kocha Ernie Brandts akimtoa kiungo Nizar
Khalfan na kumuingiza mshambuliaji Didier Kavumbangu, ambaye alikwenda kuongeza
nguvu ya safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.
Angalau,
kipindi cha pili Yanga walionekana kucheza vizuri na kupeleka mashambulizi
yenye uhai langoni mwa Simba, ingawa safu imara ya ulinzi ya Wekundu wa
Msimbazi ilikuwa kikwazo.
Katika
dakika ya 63, beki Paul Ngalema aliunawa mpira katika harakati za kuokoa na
refa Mathew Akrama akaamuru penalti, ambayo ilikwamisha kimiani kiufundi na
Said Bahanuzi ‘Spider Man’.
Katika
dakika ya 77 Mathew Amkrama alimtoa nje kwa kadi nyekundu ya moja kwa moja
Simon Msuva, baada ya kumkita Juma Nyosso, aliyemkanyaga ‘kwa bahati mbaya’.
Msuva alichezewa rafu na Nyosso na tayari refa alikwishapuliza filimbi na kumpa
kadi ya njano beki huyo wa Simba, lakini kiungo huyo wa Yanga akaponzwa na
hasira za kitoto.
Pamoja na
Yanga kubaki pungufu, waliendelea kucheza vema na mashambulizi yalikuwa ya
pande zote mbili. Refa Akrama alishindwa kuumudu mchezo na maamuzi yake mengi
yalikuwa chungu kwa Yanga, mfano Haruna Moshi ‘Boban’ alipomchezea rafu mbaya
beki Kevin Yondan hadi akashindwa kuendelea na mchezo, na nafasi yake
ikachukuliwa na Juma Abdul alimpoza kwa kadi ya njano.
Hakumchukulia
hatua yoyote kipa Juma Kaseja aliyeonekana kupoteza muda tangu mwanzo, na
alimpa onyo tu zaidi ya mara tatu.
Alipoingia
Abdul alikwenda kucheza beki ya kulia na Mbuyu Twite akahamia katikati kucheza
na Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
Baada ya
mchezo huo, kocha wa Simba, Milovan alisema kwamba ulikuwa mchezo mzuri na
Yanga walicheza vizuri, lakini timu yake ilicheza vizuri na anajivunia. Alisema
Yanga imeimarika tofauti na ilivyokuwa awali na kwamba hizo ni dalili Ligi Kuu
msimu huu itakuwa ngumu.
Kwa upande
wake, kocha wa Yanga, mwanzoni hawakucheza vizuri, lakini baadaye walitulia na
kucheza vizuri. “Hii ni mechi ya kweli ya upinzani, unaweza kuona rafu na kadi
nyingi,”alisema Brandts.
0 comments:
Post a Comment