• HABARI MPYA

    Saturday, January 19, 2013

    FEDHA ZA KUMUUZA OKWI ZISIISHIE KULIPIA MADENI

    Okwi

    Na Frank Sanga
    SIMBA imemuuza mchezaji wake wa Uganda, Emmanuel Okwi kwa timu ya Etoile du Sahel ya Tunisia kwa kitita cha Dola za Marekani 300,000 (Sh 480 milioni).
    Ni jambo la faraja kuona kuwa klabu za Tanzania zinaweza kunufaika kutokana na biashara ya wachezaji na hata kufikia uwezo wa kuuza wachezaji kwa bei kubwa kiasi hicho.
    Si faraja kwa Simba tu, lakini ni jambo zuri kwa mchezaji mwenyewe kwani amepata changamoto mpya ya maisha ikiwa ni pamoja na kupata mshahara mzuri tofauti na aliokuwa akiupata Simba.
    Katika mkataba mpya wa Simba, Okwi alitakiwa awe analipwa dola 3,000 (sh 4.8 milioni) kwa mwezi, lakini akiwa Etoile du Sahel atalipwa dola 15,000 (Sh 24 milioni) kwa mwezi kitu ambacho ni mafanikio makubwa kwa maisha ya mchezaji mwenyewe.
    Simba imemuuzwa mchezaji huyo huku ikiwa ni miaka miwili tu tangu iwauze Mbwana Samatta na Patrick Ochan kwa klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa thamani ya dola 200,000 (Sh 300 milioni).
    Kilichotusukuma kuandika maoni haya ni kuhoji jinsi fedha za kuwauza wachezaji hao zinavyotumika. Ukiuliza jinsi fedha za kuwauza Samatta na Ochan zilivyotumika utapewa maneno mengi ambayo hayana kichwa wala miguu.
    Tunahoji hivyo kwa sababu tayari tumesikia kuwa baadhi ya viongozi ndani ya Simba wameibuka na kudai kuwa wanaidai klabu hiyo fedha. Sisi tunadhani hii ni aibu kubwa kwa viongozi wa Simba kutaka kutumia fedha za mauzo ya Okwi kwa ajili ya kulipana madeni.
    Mashabiki wa Simba watataka kuona fedha hizo zikifanya jambo fulani zuri iiwezekana hata kujenga hatua za mwanzo za uwanja au kitega uchumi chochote ambacho kitaonekana mbele ya kila mmoja.
    Lakini tunapata wasiwasi kama hayo yatafanyika na hasa tukikumbuka kuwa fedha za Samatta na Ochan hazikufanya lolote zaidi ya viongozi kudai kuwa walitumia kusajili wachezaji wengine.
    Ni jambo ambalo linatia aibu na linachukiza kuona kuwa klabu zinapata fedha kwa kuuza wachezaji, lakini matumizi yake yanazua maswali mengi huku viongozi wakilipana kwa madai kuwa wanaidai klabu hiyo.
    Ni wakati sasa, wanachama wa Simba kuamka na kuhoji jinsi fedha za kuwauza wachezaji zinavyotumika katika klabu hiyo ya Msimbazi badala ya kukaa kimya na kuwaacha viongozi wakilipana madeni.
    Viongozi wa Simba nao wanapaswa kujua kuwa fedha hizo si za kwao, ila ni mali ya klabu ambayo inaundwa na wanachama na wadau mbalimbali hivyo panapokuwa na keki kama hiyo ni vizuri ikagawiwa kwa wote.
    Unaweza vipi kugawa fedha hizo kwa wanachama? Ni jambo jepesi ni kujenga uwanja ambao utaifanya klabu hiyo kuwa na uwanja wake tofauti na sasa ambapo imekuwa ikifanya mazoezi katika viwanja vya kubangaiza.
    Inatia hasira kuona baadhi ya viongozi wamegeuza klabu kuwa mali zao binafsi na kuzifanya kuwa vitega uchumi kwa ajili ya kuendeleza familia zao badala ya kuzifaidisha klabu zenyewe. (Kutoka gazeti la Mwanaspoti leo).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: FEDHA ZA KUMUUZA OKWI ZISIISHIE KULIPIA MADENI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top