IMEWEKWA MEI 14, 2013 SAA 12:28 ASUBUHI
BAADA ya kufukuzwa kocha, Roberto Mancini anatarajiwa kulipwa kiasi cha Pauni Milioni 7 na Manchester City kutokana na kuvunja mkataba wake aliosaini baada ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu msimu uliopita.
City imetoa taarifa rasmi ya kumfukuza Mtaliano huyo na sasa Msaidizi wake, Brian Kidd atamalizia msimu wakati inaendelea na mpango wa kumtwaa kocha wa Malaga ya Hispania, Mchile, Manuel Pellegrini.
Kwaheri: Roberto Mancini ametimuliwa Manchester City
Inaaminika Mancini alipewa taarifa za kufukuzwa jana usiku na Ofisa Mtendaji Mkuu, Ferran Soriano na kisha akapigiwa simu na Mwenyekiti, Khaldoon Al Mubarak, ambaye yuko Abu Dhabi.
Pellegrini, mwenye umri wa miaka 59, amekubali kutua City kwa mshahara wa Pauni Milioni 3.3. Lakini pia anafuatiliwa na Barcelona akachukue nafasi ya Tito Vilanova, ambaye anasumbuliwa na maradhi ya saratani.