Nchunga kushoto |
SWALI moja nalojiuliza kwa sasa, wako wapi
Ridhiwani Kikwete na Joel Bendera wakati huu wa vurugu zinazoendelea zenye
lengo la kumng’oa Wakili Lloyd Baharagu Nchunga Yanga?
Kwa nini najiuliza? Hawa ndio ambao
walipigana kuhakikisha huyo anakuwa Mwenyekiti wa Yanga- wakifanya jitihada za
kuwashawishi wanachama wa klabu hiyo wamchague.
Mgombea Uenyekiti aliyekuwa anapewa nafasi
kubwa ya kushinda, Francis Mponjoli Kifukwe alijitoa kwa hasira na kusababisha
vurugu kubwa kwenye ukumbi wa Mkutano, PTA, Saba Saba, Dar es Salaam.
Baada ya tukio lile niliandika makala- Nchunga
hatakaa kwa raha Yanga- na kweli, sasa yametokea. Yametimia.
Nchunga anapigwa vita- kwa sababu hakuwa
chaguo la hiari la wana Yanga katika uchaguzi.
Alijitahidi kujenga umoja ndani ya klabu na
kuvunja makundi kwa maana ya kambi za uchaguzi, baada ya kuchaguliwa,
akiwachagua wapinzani wake Mbaraka Igangula na Kifukwe katika Kamati mbalimbali.
Aliingia madarakani na watu ambao si wa
kambi yake- watu ambao wameendelea kutamani kufanya kazi na watu wao walioanguka,
akiwemo Kifukwe.
Huo ndio mwanzo au chanzo cha mgogoro
unaoendelea hivi sasa Yanga- kwamba makovu ya uchaguzi yanaitafuna Yanga.
Watu wamepania kuhakikisha Nchunga anaondoka
Yanga kwa gharama zozote, bila kuzingatia klabu itaingia katika matatizo gani.
Kukosa ubingwa wa Ligi Kuu, kufungwa 5-0 na
wapinzani wao wa jadi si kitu kwa waliopania kumng’oa Nchunga madarakani- kwani
wanataka aonekana ameshindwa.
Wanamhujumu, huo ndio ukweli ambao dalili
zake zinatokana na kauli za wanaompiga vita.
Kujiuzulu kwa Wajumbe mbalimbali mfululizo
wakiwemo Ally Mayay, Seif Ahmad Magari na Abdallah Bin Kleb na kauli ya leo ya
kocha Fredy Felix Minziro kwamba hatafanya kazi hadi alipwe malimbikizo ya
misharaha yake- yote hii ni vita ya kumchafua Nchunga aonekane ameshindwa ang’oke
kwa urahisi.
Hii ni fitina iliyotengenezwa kitaalamu na
inahitaji mweledi wa mambo haya ili kuing’amua. Matatizo ya Yanga yanayoainishwa
hivi sasa si wa mwezi mmoja- ni ya muda mrefu hata kabla akina Seif, Bin Kleb
hawajajiuzulu- lakini kwa nini iwe lawama ya Nchunga na si uongozi?
Hatakiwi na anatakiwa tu ajiuzulu, ili
wajipange upya na amini nakuambia Francis Mponjoli Kifukwe atakuwa Mwenyekiti
pale Yanga, mara tu Wakili Nchunga akisalimu amri.
Hakuna jinsi- hiki ndicho kipindi cha Yanga
kujipanga kwa ajili ya msimu ujao, wakianzia Julai kutetea taji la Klabu Bingwa
Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, hivyo katika hali ya vurugu
zinazoendelea, itawezekana vipi?
Nchunga hana ‘sapoti’ na bahati mbaya ana
fedha ya kulisha familia yake na kusaidia ndugu na jamaa zake tu- lakini si
kununua wanachama wa kumuunga mkono, ataweza vipi hii vita?
Na atawezaje wakati wapinzani wake
wanaonekana wana nguvu kubwa ya fedha na wenye kujua kupangilia fitina- kama
hizi za makocha na wachezaji kudai wanaidai klabu Milioni 270, wakati huo huo
wao wanasema aondoke wana Milioni 750 za kumaliza matatizo ya klabu.
Umeona hiyo? Nini suluhisho hapa? Wakati
mwingine hata kujitoa kwenye mapambano kwa manufaa ya wengi ni ushindi pia. Nchunga
anangoja nini? Kuendelea kuukumbatia wembe ambao mapema tu aliambiwa anaachiwa
umkate?
Na umekwishamkata sasa- kwa nini asiuachie akatibu
majeraha?
Waliombeba kwenye uchaguzi Ridhiwani na
Bendera ni kama hawasikii kinachoendelea kwa sasa na mbaya zaidi TFF inayosistiza
Katiba za klabu kuheshimiwa na kupiga vita mapinduzi, wamekaa kimya. Nini maana
yake, wanasubiri kuifungia Yanga wanachama wakifanya mapinduzi? Sijui!
Huu ndio wembe alioulilia Nchunga, wakamuachia
na sasa umemkata, anangoja nini kuachia ngazi Yanga?
0 comments:
Post a Comment